Wednesday, December 30, 2009

WHO yasema, ni mapema mno kutangaza ushindi dhidi ya virusi vya H1N1


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani WHO amesema kuwa ni mapema mno kuweza kutangaza ushindi dhidi ya virusi vya homa ya mafua ya nguruwe akiashiria uwezekano wa virusi hivyo kubadili sura yake na kuwa hatari kubwa zaidi kwa mwanadamu. Margaret Chan amesema kuwa virusi vya H1N1 bado vinaendelea kuzagaa na tayari vimewasibu mamilioni ya watu. Mkuu wa Shirika la Afya Duniani amesema habari njema ya kitiba kuhusu virusi hivyo ni kupungua kasi yake licha ya kwamba vimekwisha sababisha vifo vya watu 12 elfu wengi wao wakiwa wanawake waja wazito, watoto wadogo na watu wenye maradhi sugu. Chan amesema idadi hiyo rasmi ya watu waliofariki dunia kutokana na virusi vya mafua ya nguruwe haiakisi ukweli wa mambo na kwamba idadi kamili ya wahanga wa ugonjwa huo itajulikana baada ya kupita miaka miwili.

Sukari kupimwa kupitia lensi za macho



Wanasayansi wamegundua teknolojia mpya itakayowezesha kupimwa kiwango cha sukari katika damu bila ya kuhitajia mgonjwa kutolewa damu kila siku. Wataalamu hao wa Chuo Kikuu cha Ontario magharibi huko Hamilton, wamegundua teknolojia hiyo mpya ambapo sukari huweza kupimwa kwa kutumia lensi za macho za aina ya hudrogel zilizotengenezwa kwa vipendo vidogo vidogo vya nano. Wagonjwa wa kisukari watakaovaa lensi hizo wataweza kujua kuhusana na kiwango cha sukari mwilini mwao, kutokana na mabadiliko ya rangi ya lensi hizo za macho. Vipande vya nano vilivyotumika kutengeneza lensi hizo, hubadilika kwa kuzingatia molekuli za glukosi zilizoko kwenye machozi, suala ambalo husababisha mabadiliko ya kikemia na mabadiliko ya rangi. Wanasayansi wana matumaini kwamba, kwa kugunduliwa lensi hizo mpya na kuanza kutumika, katika siku zijazo kutakuwa hakuna tena haja ya wagonjwa wa kisukari kudungwa sindano na kuchukuliwa damu kila siku ili kujua kiwango cha sukari mwilini.

Saturday, December 26, 2009

Kujiingiza katika mapenzi kwenye umri mdogo husababisha kensa ya mlango wa kizazi


Huko nyuma iliaminiwa kuwa, virusi aina ya papiloma au (HPV) pamoja na vipimo duni ndio sababu kuu inayopelekea ugonjwa wa kensa ya mlango wa kizazi, lakini uchunguzi mpya umeonyesha kuwa kuna sababu nyinginezo muhimu zinzosababisha ugonjwa huo. Kwa mujibu wa uchunguzi uliochapishwa katika jarida la Kensa la Uingereza, mahusiano ya kijinsia yanayofanywa katika umri mdogo huongeza uwezekano wa kupata kensa ya mlango wa kizazi mara dufu. Suala jingine lililohesabiwa kuchangia maambukizo hayo, ni muda mwanamke anapopata mtoto wake wa kwanza.
Katika uchunguzi huo, imeonekana kuwa wanawake wanaoishi maisha ya kimasikini, huanza kujiingiza katika masuala ya kimapenzi miaka minne mapema kuliko wengineo. Hivyo kuna uwezekano wa kupata maambukizo ya virusi vya HPV mapema zaidi, na hivyo kuvipa muda zaidi virusi hivyo kuzaliana kwa muda mrefu na baadaye kusababisha kensa ya kizazi. Wanasayansi waliofanya uchunguzi huo wamependekeza kwamba ni bora chanjo dhidi ya virusi vya HVP itolewe mapema, hasa kwa wasichana wanaoishi katika jamii masikini, ili kuwakinga na ugonjwa wa kensa ya mlango wa kizazi.
Inafaa kujua kuwa, kensa ya mlango wa kizazi au kwa kimombo cervical cancer, ni saratani inayoshambulie lango la uzazi, sehemu ya chini kabisa na nyembamba ya kizazi. Ugonjwa huo unaweza kugunduliwa kirahisi kwa kufanya kipimo cha Pap smear. Ni muhimu kufahamu kwamba ugonjwa wa kensa ya kizazi ni ugonjwa hatari lakini unaweza kuzuiwa na kutibiwa kwa urahisi. Naahidi kuelezea kwa undani juu ya ugonjwa huo hapo baadaye.

Friday, December 25, 2009

X-Mass Njema Wadau


Leo ni sikukuu ya Christmas, kwanza kabisa blogi ya Kona ya Afya inatoa mkono wa heri na baraka kwa mnasaba wa kuzaliwa masihi, Issa Bin Maryam, (Yesu Kristo) kwa wafuasi wote wa dini hiyo ya mwenyezi Mungu. Ni matumaini yetu kuwa katika wakati huu wa sikukuu ya X-mass wadau wote huku wakisherekea sikukuu na kuwa mapumzikoni, hawatazembea pia kuzitunza afya zao. Kwa ajili hiyo basi zifuatazo ni nukta kadhaa za kufuata ili kuepusha wasiwasi na mfadhaiko wa mawazo (stress) wakati huu wa mapunziko na sikukuu, na zinazosadia kuhakikisha kwamba tunabaki katika afya njema kimwili, kiakili na kihisia.
• Jitahidi kushikamana na ibada. Kushikamama na ibada za kiroho wakati huu wote wa sikukuu, na kuwa karibu na muumba ( kwa kutegemea imani na dini ya mtu) kwa kufanya ibada kama kusali, kwenda kanisani au msikitini husaidia kumfanya mtu ajisikie vizuri kiroho.
• Pata hewa nzuri. Kila unavyojitahidi kuwa nje ya nyumba na kufanya shughuli mbalimbali ndivyo mwili wako unavyopata nishati zaidi. Kuvuta hewa safi na salama kutaufanya ubongo wako upate oksijeni zaidi na kuupa mwili wako nishati. Hivyo wakati huu wa sikukuu jitahidi kufanya michezo kama vile kukimbia, kusketi, kupanda baiskeli, kutembea kando ya bahari au mto na kadhalika.
• Jishughulishe na masuala ya sikukuu kama vile kuwanunualia watu zawadi madukani, kuwatembela ndugu jamaa na marafiki na hata wagonjwa, kualika au kwenda katika mialiko mbalimbali na kadhalika. Vitendo hivyo ni bora kuliko kukaa tuu nyumbani na kula na kunywa peke yako huku akiangalia tv au filamu.
• Pata usingizi wa kutosha na pumzisha mwili wako. Unaweza ukalala kidogo mchana au kuamka kwa kushelewa kidogo wakati wa asubuhi.
• Tenda kile moyo wako inachopenda. Kuwa na afya njema wakati wa X-mass ni pamoja na kufanya kile kinachoburudisha moyo wako. Imba kama unapenda kuimba, cheza kama unapenda kucheza, andika, tembea, chora picha, pika nakadhalika, ilimradi utende chchote kili kinachofaurahisha moho wako.
• Kula na kunya kusizidi kiasi, na bila kusahau vyakula visivyo na mafuta mengi au sukari nyingi ambavyo ni salama kwa afya zetu. Wale wenye magonjwa mbalimbali sugu wasijisahau na kuvunja miiko ya vyakula wasivyotakiwa kula. Usisahau kuwa, sikukuu itapita lakini afya yako ni muhimu sana kwa maisha yako yote… Sikukuu njema wadau huku tukitunza afya zetu!

Wednesday, December 23, 2009

Jeli ya nyanya ni bora kuliko aspirini


Utafiti mpya uliofanywa kwa majaribio umegundua kuwa katika mbegu za nyanya kuna mada asilia, inayoweza kusadia mzungumzo wa kawaida wa damu na kuzuia damu isigande. Mada hiyo iliyoko kwenye mbegu za nyanya iligunduliwa mwaka 1999 na Profesa Adim Dutta-Roy. Jeli hiyo inayozunguka mbegu za nyanya, hunaweza kusaidia mzunguko wa damu.
Jeli hiyo isiyokuwa na rangi wala ladha, huzuia chembe za damu aina ya platelets zisishikane, suala ambalo hupunguza uwezekano wa damu kuganda, kama inavyofanya aspirini lakini bila kuwa na madhara.
Wachunguzi wa Uingereza wamesema kwamba, athari za geli hiyo huanza masaa matatu tangu inapoanza kutumiwa na kudumu kwa masaa 18, hivyo inahitaji kutumiwa kila siku.
Wataalamu hao wamependekeza kwamba, kuongeza jeli hiyo katika vyakula mbalimbali kunaweza kuepusha matumizi ya aspirini kwa ajili ya kuzuia hatari ya magonjwa ya mishipa ya moyo.

Mshituko wa moyo mara nyingi hutokea saa tatu asubuhi


Wataalamu wa magonjwa ya moyo wamesema kuwa hatari ya kupatwa na mshituko wa moyo hutokea zaidi mapema asubuhi, hasa saa tatu asubuhi.
Utafiti huo uliotangazwa katika Kongress ya 4 magonjwa ya moyo ya Mashariki ya Kati imesema kuwa, watu wanaokabiliwa na hatari ya kupatwa na mshituko wa moyo, hutokewa na ugonjwa huo mapema asubuhi kwa sababu ya mabadiliko ya homini ambayo huongeza hitajio la oksijeni la mishipa ya moyo katika wakati huo, na kusababisha mshituko wa moyo. Uchunguzi huo umeelezea pia kuwa, ripoti zinaonyesha ongezeko la matukio ya mshituko wa moyo katika siku za Jumatatu, suala ambalo huenda likawa linachangiwa na kiasi kikubwa na kula kupita kiasi siku za wikiendi. Wataalamu hao pia wamesema kuwa, mishipa ya juu ya mwili huwa inasinyaa msimu wa baridi, hali ambayo ni kinyume na utendaji wa mishipa ya moyo na husababisha kupungua kiwango cha oksijeni inayohitajiwa na misuli ya moyo. Wamesema hii ndio sababu, watu hupata mishtuko wa moyo kwa wingi wakati wa mapukutiko (fall) na baridi (winter).
Uchunguzi huo pia umeachiria kwamba, umri wa watu wanaopatwa ugonjwa huo imeshuka na hata kufikia chini ya miaka 55 katika baadhi ya nchi.

Monday, December 21, 2009

Ujuwe ugonjwa wa Kifua Kikuu au TB ....sehemu ya kwanza



Karibuni wapenzi wadau wa Kona ya Afya katika mfululizo mwingine wa
kujadili magonjwa mbalimbali. Leo tumepata fursa ya kuzungumzia ugonjwa wa kifua kikuu, ambacho maambukizo yake yanaongezeka kwa kasi kubwa ulimwenguni, khususan katika nchi zinazoendelea. Kwa kuzingatia kuwa ugonjwa wa kifua kikuu huathiri watu wa rika zote na hasa vijana kati ya miaka 15 hadi 45 ambayo ndiyo nguvu kazi katika nchi nyingi za dunia, kunapaswa kufanyika jitihada kubwa za kudhibiti maambukizo ya ugonjwa huo. Kifua Kikuu ambao kitaalamu hujulikana kama Tuberculosis ni ugonjwa wa kuambukiza ambao huenezwa kwa njia ya hewa. Kifua kikuu husababishwa na bacteria au kimelea aina ya Mycobacterium tuberculosis au (tubercle bacterium). Ugonjwa huu kwa kawaida huathiri mapafu, lakini pia huweza kushambulia viuongo vingine vya mwili kama vile tezi za limfu, ubongo na mifupa.
Tb inambukizwa kwa namna gani? :
Mtu mwenye kifua kikuu au Tb ambaye hajatibiwa, anapokohoa, kupiga chafya, kutema mate au makozi husambaza bacteria au vimelea hivyo vya ugonwja huo hewani. Kwa hivyo mtu mwingine akivuta hewa yenye vimelea hivyo anaweza kuambukizwa kifua kikuu. Kwa mfano takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa nchini Tanzania ugonjwa wa Kifua Kikuu umekuwa ukiongezeka kwa kasi kubwa ambapo watu elfu 65,000 hivi sasa wanaugua kifua kikuu nchini humo. Kati yao asilimia 50 pia wana ukimwi. Hapa linajitokeza swali kwamba dalili za Kifua Kikuu ni zipi?
Mtu ambaye amepatwa na ugonjwa wa Tb au Kifua Kikuu huwa na dalili au husumbuliwa na hali zifuatazo:
Kukohoa kwa muda usiopungua wiki mbili na mara nyingine kukohoa damu, homa za jioni za mara kwa mara, kutokwa na jasho usiku, kukosa hamu ya kula, kupungua uzito kwa kiasi kikubwa na kadhalika.
Kundi ambalo liko kwenye hatari kubwa ya kuambukizwa Tb au kifua kikuu ni la wale wanaoishi kwa karibu na kwa muda mrefu na mtu yule aliyekwisha ambukizwa ugonjwa huo. Kwa hiyo hapa nitaorodhesha makundi ambayo yako kwenye hatari na ya uwezekano mkubwa wa kuambukizwa Tb iwapo watakuwa karibu na mgonjwa. Watu hawa ni rahisi kupatwa na kifua kikuu kwa sababu kinga zao za mwili huwa ni za kiwango chini: Watoto wadogo na wazee, wale wote wanaougua kisukari, watu wnaotumia dawa aina ya steroids au dawa nyinginezo zinazoathiri mfumo wa kinga ya mwili, waathirika wa ukimwi na HIV, wale wote wanaoishi maeneo yenye msongamano mkubwa watu yaliyoduni kiafya, wanaoishi kwenye sehemu zisizokuwa na hewa ya kutosha, watu wanaotumia dawa mbalimbali, au pombe na mwisho wale wenye lishe duni.
Usikuko muendelezo wa makala hii, na daima linda afya yako.

Sunday, December 20, 2009

Njia za kuondoa makovu


Kuna matatizo malimbali ya ngozi yanayoweza kuwapata watu ambapo makovu ni mojawapo ya matatizo hayo.Makovu baadhi ya wakati hajawezi kuepukika hasa iwapo makovu hayo yamesababishwa na magonjwa au ajali mbalimbali. Makovu katika sehemu mbalimbali za mwili huweza kufunikwa na kufichwa kwa urahisi iwapo hayapo katika sehemu zinazoonekena. Lakini iwapo makovu yatakuwa usoni, mikononi au kifuani, huwa si rahisi kuyaficha na mara nyingi huwakera wale walio na makovu. Watu wengi wangependa kujua ni njia gani ambazo mtu anaweza kutumia ili kuondoa makovu. Ili kulijibu swali hilo ni bora kwanza tujue kovu ni nini hasa. Kovu katika mwili hutokea pale tishu aina ya fibrous inapojikusanya juu ya ngozi ili kusaidia kukarabati seli na ngozi iliyoharibika. Wakati kunapotokea jeraha, ngozi kutoa seli ziitwazo fibroblasts ambazo hutoa kitu kiitwacho collagen na kujaza sehemu yenye jeraha. Collagen ni ngumu, iko kama ufumwele unaopatikana katika protini ambayo hujaza eneo lote le kovu. Collagen ipo pia katika ngozi ya kawaida lakini katika kovu huwa nyingi na iliyojipanga katika mpangilio holela. Hii ndio sababu kovu huwa na rangi iliyokolea na huonekana kwa urahisi. Baadhi ya makovu huondoka kwa urahisi, baadhi huchukua miezi na hata miaka, huku makovu mengine yakibadilika polepole rangi na muonekano wake. Kovu huenekana kirahisi juu ya ngozi kwa sababu seli zilizotumika kuunda kovu hutofautiana na seli za mwanzo za ngozi. Kwa mfano makovu yaliyo juu ya ngozi hayawezi kuota vinyeleo kwa kuwa seli zake hazina matundu ya vinyeleo. Pia makovu hayana uwezo wa kuzuia miale ya jua. Kwa bahati mbaya ni vigumu kidogo kuweza kuondoa baadhi ya makovu moja kwa moja katika ngozi. Ingawa kuna njia kama vile vipodozi vinavyoweza kuziba makofu na njia nyinginezo za kitiba, lakina hata hivyo njia zote hizo mara nyingi huwa haziwezi kuondoa baadhi ya makovu kabisa, hasa yale makovu yaliozama katika ngozi na kuharibu kwa ngozi kwa kiasi kikubwa. Njia za tiba zinazoweza kutumiwa kuondoa makovu ni kama vile operesheni ya Laser (laser sugery), sindano za steroid, kubandua ngozi ya juu (dermabrasion) na radio therapy.
Lakini hata hivyo kuna njia mbalimbali za tiba asilia ambazo zinaaminika kuweza kusaidia kuondosha makovu. Njia hizo ni kama
1. Majani ya Aloe Vera. Majani haya yanapatikana kila sehemu hasa kwetu Tanzania na kwingineko Afrika. Majani hayo pia ni dawa nzuri ya kutibu magonjwa mbalimbali ya ngozi kama vile kiba au kishilingi. Kata majani hayo na utumie utomvu wake kupaka katika makovu. Baada ya muda polepole itapunguza na kuondoa makovu. Aleo Vera ni majani ambayo yanasifika hivi sasa ulimwenguni kote kwa ajili ya ngozi na yanatumiwa katika vipondozi mbalimbali. Basi zaidi ya kukuondoa makovu, yatasaidia pia kuifanya ngozi yako iwe nyororo.
2. Njia nyingine ni kutumia tango. Twanga tango na tumia mchanganyiko wake kupaka juu ya kovu. Husaidia kulainisha makovu na unapotumia kwa muda mrefu huondoa makovu pia.
3. Kupaka asali juu ya kovu na kuiacha usiku kucha. Njia hii inaweza kurudiwa mara kwa mara hadi pale kovu litakapotoweka.
4. Kula vyakula vyenye vitamin E, ambavyo ni ni muhimu katika kusaidia ngozi kupona na kurudia katika hali yake ya kawaida. Vitamin E iko katika mayai, nyungu za aina mbalimbali kama karanga, mayai, mafuta ya nafaka na vinginevyo. Kama huwezi jitahidi utumie vidonge vya vitamin E lakini baada ya kupata ushauri wa daktari.
5. Kupaka baking soda kidogo na maji sehemu yenye kovu na kuikanda sehemu hiyo kwa dakika moja. Mara mbili kwa siku. Kisha safisha kwa maji ya vuguvugu halafu paka mafuta ya zaituni.
6. Kutumia cream zenye vitamini E nad C na upake moja kwa moja katika kovu. Husaidia ngozi kuota tena katika kovu. Unaweza kumuona mtaalamu wa magonjwa ya ngozi naye akakushauri ni cream gani utumie ili kuondoa makovu yako. Pia jitahidi kupata lishe nzuri bila kusahau matunda na mboga mboga ambayo ni muhimu kwa ajili ya afya ya ngozi. Kunywa maji ya kutosha kwani maji pia kulainisha ngozi yako na kufanya makovu kutoka kwa urahisi.

Inafaa kujua kuwa baadhi ya makovu kama vile yaliyosababishwa na kuungua au kuchanjwa ni vigumu kuyaondoa kwa kutumia njia hizo zilizotajwa.

Friday, December 18, 2009

Mmh!... watafiti wasema ukoma unaweza ukawa ugonjwa wa kumbukiza!


Watafiti wamegundua geni ambazo zinahusiana na ugonjwa wa ukoma, suala ambalo linaondoa fikra ya huko nyuma kwamba ukoma si ugonjwa wa kuzaliwa au wa kuridhi. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa huko China na kuchafishwa katika Jarida la Tiba la Uingereza, mabadiliko ya geni 7 mwilini yanaweza kuwa ndio chanzo cha uwezekano wa baadhi ya watu kupatwa na ukoma. Wataalamu hao wamesema kuwa, tangu kale imekuwa ikifikiriwa kuwa ukoma ulikuwa ukisababishwa tu na vijidudu lakini uchunguzi wao umeonyesha kuwa maambukizo ya ugonjwa huo yansababishwa pia na genetiki. Wamesema kwamba, iwapo mzazi ana ugonjwa huo, basi kuna uwezekano mkubwa mwanaye naye akapatwa na ugonjwa huo. Hata hivyo wataalamu hao wamesema, cha kushangaza ni kuwa, iwapo mmoja kati ya mke na mume wana ukoma, mwingine hawezi kuambukizwa ugonjwa huo kwa miaka mingi. Geni 5 kati ya hizo 7 zinazosababisha ugonjwa huo, inaaminiwa kuwa zinauhusiano wa karibu na mfumo wa kulinda mwili.
Uchunguzi huo unaleta matumaini ya kuweza kukingwa mapema wale wanaodhaniwa kuwa wana uwezekano wa kupatwa na ugonjwa huo. Vilevile utafiti huo unaweza kutumika kuchunguza zaidi vijidudu vya magonjwa mengine ambavyo vinakaribiana na vijidudu vinayosababisha ukoma, kama vile vijidudu vya kufua kikuu ugonjwa ambao husababisha vifo vya watu milioni 1.8 duniani.
Sio vibaya kujua kuwa, ugonjwa wa ukoma au Leprosy kwa kiingereza na kitaalamu Hansen's disease, unaosabaishwa na bacteria waitwao Mycobacterium Lapracea na Mycobacterium Lepromatosis huathiri ngozi, utando telezi (mucous membranes), neva za ukingoni (peripheral nerve) pamoja na macho.
Kuharibika daima neva au mishipa ya fahamu kunakosababishwa na ugonjwa wa ukoma, humzuia mtu anayepona ugonjwa huo kuhisi maumivu, suala ambalo huwafanya wagonjwa wa ukoma kuwa wenye kupata kwa urahisi majeraha madogo madogo na vidonda ambayo baadaye huwa makovu ya kudumu.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limeripoti kuwa, kuna kesi 254,525 mpya za ugonjwa wa ukoma katika nchi za tropiki na zilizo chini ya jangwa la sahara.
Kumbuka kuwa ugonjwa wa ukoma unatibika na unapotibiwa mapema huweza kumuepusha mgonjwa kupata madhara makubwa ya kukatika viungo na kuwa mkoma!

Wednesday, December 16, 2009

Sumu ya Ndani ya Chakula au Food Poisoning…sehemu ya mwisho


Mambo mengi yanaweza kufanywa ili kuzuia vijidudi maradhi na sumu kuchafua chakula chetu. Mosi, safisha mikono yao kwa utaratibu, kabla na kila mara unapotayarishah chakula, funika kwa sashi au bandage sehemu yoyote ya yenye mchubuko au uliojikata katika mkono wako kabla ya kuanza kuandaa chakula,safisha sehemu zote utakazotumia wakati wa maandalizi ya chakula, brashi na sponji za kuoshea vyombo kwa kiasi kikubwa huwa na uwezekano wa kubeba bacteria. Kwa hivyo ni lazima zioeshwe mara kwa mara baada ya kutumia. Vyakula aina ya nyama na mayai vinapaswa kupikwa barabara na vipoti kupashwa moto vizuri kabla yakuliwa. Hakiisha jokofu au friji lako lina nyuzi joto 40 na freeza ikiwa nyuzi 0 au chini ya hapo, kiporo cha chakula kisikae ndani ya jokofu kwa zaidi ya siku nne, usiache ovyo nyama bila ya kuihifadhi, na vyema uichemshe kwa zaidi ya nyuzi joto 140, kuwa mwangalifu wakati wa kuhifadhi vyakula kama vile samaki, nyama mbichi na mayai, hivyo vyote vinaweza kuchafuliwa na bacteria wa maradhi. Usivue samaki kutoka kwenye maji yaliyochafuka, safisha mboga mbichi na matunda kabla ya kula au kupika, unanunuji vyakula vinavyouzwa ndani ya makopo, mikebe n.k unapaswa kwanza kuangalia muda wa matumizi yake unakwisha lini, usile uyoga wa mwituni, ambao haujaidhinishwa na mtaalamu kuwa ni salama kwa mwanadamu na mwisho hakikisha kuwa bidhaa zote zinazotokana na maziwa ambazo nyingi huuzwa madukani ni lazima ziwe zimeondolewa vijidudu hasa bacteria kwa njia ya kitaalamu ijulikanayo kama pasteurization. Maziwa ya ng'ombe ambayo hayajapitia katika njia hiyo ya pasteurization, yanapaswa kuchemshwa vizuri kabla ya kutumia.
Itakumbukwa kuwa watoto, wazee na wale wote wenye magonjwa ya muda mrefu au wenye kinga ya dhaifu ya mwili huwa na hali mbaya wakati wakila chakula kilichoharibika au kuchafuliwa na vimelea vya maradhi. Kwa hiyo ili kukabiliana na tatizo hili, watu wazima wanapaswa kubeba jukumu kuu la kuepukana na suala hilo na vile vile kuwaelekeza watoto pia nini cha kufanya.

Monday, December 14, 2009

Oooh! Jeli ya HIV ya kina mama imeshindwa kuzuia Ukimwi!


Jaribio kubwa la jeli ya ukeni ya kuzuia vijidudu limeonyesha kuwa, hakuna ushahidi kwamba inapotumiwa huuzuia hatari ya maambukizi ya Ukimwi kwa wanawake. Jeli jiyo inayoitwa PRO 2000, ilikuwa inakusudiwa kutumiwa kabla ya kujamiiana ili kusaidia kupunguza maambukizo ya Ukiewi. Jaribio hilo lilifanywa kwa kuwashirikisha wanawake 9,385 katika nchi 4 za Kiafrika. Ilikuwa inatarajiwa kuwa jeli hiyo ya kuzuia vijidudu ingeweza kuwa njia muhimu ya kupunguza kuenea kwa virusi vya HIV, huku wataalamu wakikiri kwamba kuenezwa kondom pekee hakujasaidia kupunguza maambukizo ya ugonjwa huo. Wataalamu wanasema kuwa bado njia mpya zinahitajika zaidi ili kupambana na gojwa hilo hatari, hasa katika nchi zilizo chini ya jangwa la Sahara barani Afrika, ambapo zaidi ya asilimia 70 ya wale walioambukizwa ugonjwa huo ni wanawake. Wanawake mara nyingi wamekuwa wakilazimika kufanya ngono zembe, na wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi ya kupatwa na ugonjwa wa Ukimwi kuliko wanaume, hivyo inafikiriwa kuwa iwapo itapatikana jeli ambayo wataweza kutumia ili kuzuia maambukizo hayo, suala hilo litawalinda zaidi.
Huko nyuma jaribio dogo lilionyesha kwamba jeli aina ya PRO 2000 ingeweza kupunguza hatari ya mambukizo ya HIV kwa asilimia 30.

Haya tena…. kukoroma kuna uhusiano na kisukari!


Uchunguzi mpya umeonyesha kwamba, wale wanaokoroma wakati wakilala, wanakabiliwa na hatari kubwa ya kupatwa na ugonjwa wa kisukari kuliko wale wanaolala kimya. Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliofanywa kwenye chuo kikuu cha Yale, wale wanaokoroma sana wanapolala, wanakabiliwa na uwezekano wa kupata kisukari kwa asilimia 50. Wataalamu wanasema pia kuwa, kushindwa kupumua usingizini au kitaalamu kunahusiana na kisukari aina ya pili, bila kujali sababu nyinginezo kama vile umri, jinsia, uzito na hata asili anayotoka mtu.
Kukoroma sugu, au kitaalamu sleep apnea ni hali ambayo inasababishwa kushindwa kufanya kazi njia ya hewa, suala ambalo humfanya mtu aamke mara kadhaa usingizini wakati anapolala. Hali hiyo inahusiana na baadhi ya mabadiliko ya umetaboli au hali ya ujenzi wa seli na uvunjaji vunjaji wa kamikali mwilini, kwa kimombo ‘metabolism’.

Sunday, December 13, 2009

Afya njema inaongeza uwezo wa akili au IQ


Utafiti mpya umeonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya afya njema ya mwili wa vijana na watu wazima pamoja na kufanya kazi vyema ubongo, na uwezo wa kupata maksi za juu katika vipimo vya akili au IQ test. Utafiti huo uliochapishwa katika jarida la Akademia la sayansi umeeleza kwamba, kuwa na afya nzuri ya mwili katika umri wa miaka 15 na 16 kunaongeza uwezekano wa kuwa na uwezo wa akili wa juu. Wataalamu wamesema vijana wa aina hiyo wana uwezo mkubwa wa kufanikiwa kusoma elimu ya juu na kupata kazi nzuri maishani. Kuwa fiti kimwili inaamisha pia kuwa na moyo unaofanya kazi vizuri na uwezo mkubwa wa mapafu, vilevile kuwa na ubongo wenye kupokea vyema hewa ya oxygen, suala ambalo wataalamu wanasema linatofautiana na kuwa na nguvu za misuli. Wanasayansi wanaamini kuwa, sababu za kimazingira zinaathiri zaidi afya ya mtu na kiwango cha akili kuliko sababu za kurithi.

Saturday, December 12, 2009

Sumu Ndani ya Chakula au Food Poisoning...sehemu ya kwanza


Neno food poisoning ni ugonjwa unaosababishwa na ulaji na unywaji wa chakula kilichochafuliwa au kuguswa na aidha sumu za bacteria au vimelea vya maradhi na kumsababishia mtu maumivu ya tumbo (tumbo kukata) kuhara, kutapika n.k. Nnnaposema unywaji ninamanisha vinywaji kama vile maji, maji ya matunda, maziwa n.k. Kesi nyingi za kuchafuliwa huko kwa chakula zinatokana na ulaji wa vyakula vilivyochafuliwa na bacteria wengi wanaosababisha madhara, hata hivyo food poisoning inaweza pia kusababishwa na virusi, kemikali, mimea na samaki wenye sumu. Ni wazi kuwa, tumezungukwa na bacteria kila upande, kwa hiyo kutokea kwa baadhi ya kesi za uchafuzi wa chakula ni jambo la kawaida. Vimelea hao wanaotuzunguka wanapatikana pia kwenye chakula na wakati mwingine wanaweza kuwa wa manufaa kwetu. Hata hivyo bacteria wale ambao wako katika vitu vilivyooza na mabaki ya vyakula, si wazuri kwetu. Mtu aliye kula chakula kilichochafuliwa au kugusana na vijidudu maradhi hao, huwa na dalili kuu zifuatazo: kutapika, kuhara na maumivu ya tumbo(kitaalamu hujulikana kama stomach flu). Aidha dalili hizo mara nyingi huambatana na maumivu ya misuli, homa, kutetemeka mwili na kuihisi kuchoka. Hatua ya kuhara na kutapika mtu, husaidia mwili kuondoa mada zenye sumu au athari katika mfumo wa mmeng'enyo wa chakula (digestive tract) na hivyo kuzizuia sumu au vijidudu maradhi hivyo kuingia katika mfumo wa damu. Vyakula vinavyotokana na wanyama, vyakula vibichi na vile vya jamii ya mboga ambavyo havioshwi, vyote vinaweza kuwa na vidudu maradhi au Germs na kuchafua chakula au kusababisha food poisoning. Vyakula hivyo ni kama vile nyama, kuku, mayai maziwa na samaki aina ya kama wadogo. Bacteria kama vile Salmonela na Listeria ni miongoni mwa vimelea vinavyopatikana katika vyakula vilivyoharibika au kuoza.
Wakati mwingine inakuwa vigumu kueleza iwapo umekumbwa na hali hiyo baada ya kula chakula kilichoharibika. Sasa iwapo mtu atakuwa na mojawapo ya dalili hizo zilizotajwa, kama vile tumbo kukatakata, ni vyema awaulize watu wengine wa familia iwapo kuna wengine walio na dalili kama hiyo na kama wamekula chakula kama hicho alichokula yeye. Na iwapo kutakuwa hakuna yeyote mwenye dalili kama yake, basi kwa kiasi kikubwa huwenda akawa amepatwa na maradhi hayo. Wakatimwingine mtu huanza kujisikia mgonjwa katika muda wa masaa machache baada ya kula chakula kilichochafuliwa na sumu za bacteria au na vimelea vya maradhi. Dalili huanza kujitokeza kuanzia muda wa saa moja hadi matatu baada ya kula chakula kisichofaa. Na wakati mwingine mtu hawezi kujisikia mgonjwa, hadi kupita siku kadhaa baadaye. Na iwapo mtu atakuwa amekula chakula chenye kiasi kidogo cha sumu au toxin, muda wake wa kuuugua utakuwa mfupi na mara moja ataanza kujisikia vizuri. Katika hali kama hiyo mtu anapoona ana dalili hizo nilizozitaja, ni vyema amuone daktari mapema kwa ajili ya matibabu. Iwapo utakwenda kwa tabibu au daktari, atakuuliza masuali mengi kama vile unajisikiaje, umeanza kuumwa lini, ulikula nini hapo kabla na je kuna mtu yoyote wa karibu yako au unaemfahamu aliye na dalili kama zako? Nk. Aidha daktari anaweza kukuandikia vipimo vya haja kubwa na ndogo ili kuona kama vijidudu hivyo maradhi ndivyo vimesababisha hali hiyo iliyokusibu. Na iwapo utaona damu ndani ya kinyesi, unashauriwa kumuona daktari mara moja pasina na kuchelewa……. Makala hii inaendelea.

Thursday, December 10, 2009

Watu milioni 5 hufariki dunia kila mwaka kutokana na tumbaku



Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza kwamba kila mwaka watu milioni 5 hufariki dunia kutokana na kutumia tumbaku, na kusisitiza kuwa hatua muhimu zinapaswa kuchukuliwa ili kukabiliana na uvutaji wa sigara. Tumbaku inaongoza duniani katika kusababisha magonjwa mbayo yanawezekana kuzuilika. Kuwa karibu na mazingira ya wanaovuta sigara au uvutaji sigara usio wa moja kwa moja (second hand smoking) pia kunasababisha vifo vya watoto 600,000 wanaozaliwa bila kufikia muda wao kila mwaka, huku karibu asilimia 95 ya watu duniani wanaishi katika sehemu ambazo hazina sheria zozote zakupiga marufuku ufutaji sigara. Mkurugenzi wa WHO anayeshughulikia marufuku ya tumbaku Douglas Bettcher amesema kwamba, watu wanapaswa kuelemishwa zaidi juu ya madhara ya tumbaku ambayo ni mabaya kwa afya ya binadamu. Maafisa wa afya wanatabiri kwamba, ifikao mwaka 2030, tumbaku inaweza kusabbaisha vifo vya watu milioni 8 kwa mwaka, hasa katika nchi zilizoendelea, iwapo hatua muhimu hazitochukuliwa ili kupambana na suala hilo.
….Wapenzi wadau wa blogi ya Kona ya Afya, leo wakati nikiandika habari hii nimekuwa nikifikiria ni kwa nini binadamu baadhi ya wakati tushindwe kujizuia kufanya masuala ambayo tunajua fika kuwa ni hatari kwa afya zetu?. Pengine tumesikia mara nyingi kuwa uvutaji sigara una madhara makubwa na tumeshashuhudia hata watu wa karibu yetu wakipata madhara hayo. Labda pia kwa kuwa uvutaji sigara ni suala la kawaida katika nyumba zetu, ofisi zetu, majumba ya starehe, katika mitaa yetu na kote kulikotuzunguka basi tumelizoea suala hilo na kuliona ni la kawaida. Lakini ukweli usiopingika ni kwamba, ufutaji sigara una madhara, sio tu kwa wavutaji sigara peke yao, bali hata kwa sisi tulio karibu ya wavutaji hao. Nafikiri muda umewadia sasa wa kujiuliza kwa undani swali hili kuwa: Je? kama kuna magonjwa yenye madhara kwa afya na uzima wa miili yetu ambayo yanaweza kuepukika, basi kwa nini tusijiepushe nayo!??
Daima tuzitunze afya zetu!

Wednesday, December 9, 2009

Kunywa kawaha kunaweza kupunguza hatari ya kupatwa na kensa ya korodani


Utafiti uliofanywa nchini Marekani umeonyesha kuwa, kunywa kahawa kunaweza kusaidia kupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa kensa ya korodani au prostate cancer.
Uchunguzi huo umeonyesha kwamba, wanaume wanaokunywa kahawa kwa wingi, hunguza hatari hiyo kwa asilimia 60 ikilinganishwa na wanaume ambao hawanywi kahawa kabisa. Kahawa inaathiri jinsi ambavyo mwili unayeyusha sukari, pamoja na kiasi cha homoni za jinsia, masuala ambayo yanahusiana moja kwa moja na kensa ya korodani. Watalamu hao wamesema kuwa, kampaundi za kibayolojia zilizoko katika kahawa zinazuia tishu kuharibika na hivyo kupunguza uwezekano wa kensa ya korodani kukua.
Inafaa kufahamu kwamba, kensa ya korodani ni kensa ya pili inayowapata kwa wingi wanaume duniani na kusababisha vifo. Kati ya wanaume 6 mmoja kati yao hupatwa na saratani ya korodani.

Monday, December 7, 2009

Usafi na Utunzaji wa meno ya watoto…sehemu ya 2



Wapenzi wadau na leo tunaendelea kujadili usafi wa meno ya watoto. Imeelezwa kuwa kwa watoto wadogo yaani wale wa chekechea, wazazi wanashauriwa kutumia kiwango kidogo cha dawa ya meno yaani dawa hiyo iwekwe kwenye shashi au kitambaa na wasafishe meno ya watoto wao kwa utaratibu. Na ikiwa meno yote ya mbele ya mtoto wako yameota, unashauriwa kutumia mswaki mdogo wa watoto. Njia nyepesi ya kumsafisha mtoto ni kuhakikisha kuwa kichwa chake kimejiegemeza kwenye mapaja yako, ili uweze kuona vyema ndani ya kinywa chake na kuyasafisha kama inavyotakikana, huku mtoto akiwa katika hali ya utulivu. Na iwapo mtoto atakuwa mkubwa kuanzia miaka saba anaweza kusimama mkabala na mzazi wake huku ukikiinua kichwa chake ili kuweza kufikia na kuona vizuri meno yote. Mara nyingine wazazi wamekuwa akishuhudia watoto wao wakitokwa na damu kwenye fizi wakati wakipigwa mswaki. Jambo hili lisiwazuie wazazi kuwasafisha meno watoto wao. Kuvuja damu fizi ni ishara ya kuathiriwa na maradhi. Kwa hiyo uvujaji huo wa damu utatokomea iwapo utando unaong'ang'ania kwenye meno na bacteria au vijidudu maradhi vitaondolewa.
Kwa kuzingatia kuzagaa aina mbalimbali za dawa za kusafisha meno (au tooth paste) katika maduka mbalimbali hivi sasa, wazazi wanakabiliwa na hali ngumu katika kuchagua dawa ipi ni bora kwa usafi na utunzaji wa meno ya watoto. Lililo umuhimu hapa ni kufahamu kiasi kinachotakikana kutumika katika mswaki wa mtoto wako na si aina ya dawa. Kiasi kidogo tu cha dawa ya meno kinatakikana kwa mtoto wako na si kurundika lundo la dawa, hiyo haina faada yoyote ghairi ya kumletea madhara. Dawa ya meno haipaswi kumezwa. Hatua ya kumeza au kula kiasi kikubwa cha dawa ya kusafishia meno inazidisha hatari ya kuoza meno ya muda ya watoto yaani (permanent teeth) khususan kwa watoto walio na umri chini ya miaka mitano. Kwa sababu hiyo wataalamu wa meno hawashauri kutumia dawa za kusukutulia kinywa yenye kampaundi ya fluoride kwa watoto chini ya miaka sita, kwa sababu hawawezi kujizuia kumeza na hivyo huwa na uwezekano mkubwa wa kukumbwa na maradhi ya fluorosis.
Je mnafahamu kuwa chakula kina athari kubwa katika afya ya kinywa na meno ya mtoto wako? Uchaguzi wa vyakula na mipangilio ya ulaji tangu kipindi cha utotoni huweza kuwa na taathira kwa afya ya uhai wa maisha yako yote. Mlo kamili unaojumuisha vyakula vya aina tatu kwa siku (Yaani protini,vitamini na wanga ) unapaswa kushajiishwa. Hatua ya kujumuisha mada za protini katika milo hiyo husaidia watoto kutohisi njaa haraka, na hivyo kumfanya mtoto kukosa hamu ya kukimbilia kula vyakula visivyo na manufaa kama vile vyenye sukari nyingi. Wataalamu wa meno wa watoto wanasema kuwa miendo bora ya ulaji chakula pamoja na usafi wa kinywa unaotakikana si tu kuwa humuepusha mtoto kuoza na kuharibika kwa meno yake, bali pia humfanya mtoto kimwili kuwa katika afya njema.

Watoto wanaozaliwa na uzito mdogo hubaleghe mapema


Kuna ushahidi kuwa watoto wanaozaliwa na uzito mdogo, hufikia baleghe mapema. Jarida la ripoti za lishe za Marekani limearifu kwamba, kuongezeka kwa haraka uzito wa mtoto katika umri wa miaka miwili ya mwanzo, pia kunapeleka kubaleghe mapema mtoto huyo. Kubaleghe mapema pia kumekuwa kukihusishwa na ongezeko la hatari ya kupatwa na kensa za matiti na korodani. Hii si mara ya kwanza utafiti kuonyesha kwamba uzito mdogo wakati wa kuzaliwa unaweza kusababishwa mtoto kukua mapema. Wataalamu wanasema kuwa, kueleweka vyema sababu zinazotokea mapema katika maisha na kupelekea hatari ya kupatwa mtu ugonjwa wa kensa, kunaweza kusaidia katika kuchukuliwa stratejia za kuzuia ugonjwa huo mapema.
Miongoni mwa sababu zinazosababisha mtoto kuzaliwa akiwa na umri mdogo ni:
• Matatizo ya fuko la uzazi
• Rubella
• Mama kuwa na ugonjwa wa Ukimwi
• Mama kutumia pombe kwa wingi wakati wa ujauzito
• Mama kuvuta sigara wakati wa ujauzito
• Mama mjamzito kuwa na magonjwa sugu
• Shinikizo la damu wakati wa ujauzito
• Mama mjamzito kukosa lishe bora
• Mama mjamzito kutumia madawa ya kulevya
• Kuwepo maji mengi kwenye fuko la uzazi.
• Mama mjamzito kuwa na kifafa cha mimba (Preeclampsia)
• Fuko la uzazi kuvunjika kabla ya muda wake
• Mama mjamzito kuwa na magonjwa ya mfumo wa mkojo (U.T.I)
• Matatizo ya urithi
• Mama mjamzito kuwa na matatizo ya figo

Sunday, December 6, 2009

Kuvuta sigara mara baada ya kuama kunaongeza hatari ya kensa ya mapafu


Wanaovuta sigara mara tu baada ya kuamka asubuhi, husababishwa kiwango cha juu cha nikotini kukusanyika katika damu zao, zaidi ya wale wanaofuta sigara baadaye, suala ambalo huwafanya wakabiliwe na hatari kubwa zaidi ya kupatwa na kensa ya mapafu. Kuvuta sigara baada ya kupata kifungua kinywa, huunguza kiwango hicho cha nikotini katika damu. Uchunguzi umeonyesha kwamba, wafutaji sigara wa mapema asubuhi, huongeza kiwango kikubwa cha nikotini katika damu zao, bila kuzingatia kwamba wanavuta sigara ngapi kwa siku. Uchunguzi uliofanywa na Chuo Kikuu cha Tiba cha Penn State umeshauri kwamba, wanaovuta sigara mapema asubuhi wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi ya kupata kensa ya mapafu, hivyo ni bora wasaidiwe kuacha kuvuta sigara. Ingawa sababu inayopelekea kiwango cha nikotini kiwe juu zaidi kwa wafuta sigara kabla ya kula stahtahi haijafahamika, lakini inaonekana kuwa wale wanaovuta sigara kabla ya kula kitu wamebobea zaidi katika uvutaji, ikilinganiswa na wale wanaosubiri na kuvuta sigara baadaye.
Inafaa kujua kuwa: Uvutaji sigara unasababisha kwa asilimia 90 vifo vinavyotokana na kensa ya mapafu. Idadi ya watu wanaopatwa na kensa ya mapafu inaongezeka kila siku duniani na kuzidisha vifo vinavyotokana na saratani nyinginezo.
Kwa kawaida kensa ya mapafu huwapata watu wanapokuwa na umri wa miaka 45, na wakati mtu anapopimwa na kukutwa na ugonjwa huo kwa kawaida huwa tayari umeshasambaa mwilini mwake. Saratani ya mapafu inahusiana moja kwa moja na uvutaji sigara. Hatari ya kupatwa na kensa ya mapafu inaambatana moja kwa moja na idadi ya sigara mtu anazovuta.

Kutumia simu ya mkono, hakuna uhusiano wowote na saratani ya ubongo


Japokuwa kumekuwa na imani kwamba kutumia simu ya mkono kwa muda mrefu kunaongeza hatari ya kupatwa na kensa ya ubongo, lakini utafiti mpya umekanusha madai hayo. Huko nyuma uchunguzi ulionyesha kwamba kukaririwa sumaku umeme za redio zinazotoka katika simu za mkono, kunasababisha hatari kubwa ya kupatwa na kensa. Lakini kwa mujibu wa utafiti uliochapishwa katika Jarida la Taasisi ya Kensa, hakujakuwa na mabadiliko yoyote kuhusiana na ugonjwa wa kensa ya ubongo tangu simu za mkono zilizpogunduliwa katika muongo wa 1990.
Wataalamu wanasema kwamba, kuna ushahidi wa kisayansi unaosema kuwa, kutumia simu za mkono kwa miaka isiyozidi 10 hakuongezi uwezekano wa kupatwa na saratani, na utafiti huo unaunga mkono suala hilo. Hata hivyo wataalamu wameshauri kuwa, uchunguzi na ufuatiliaji wa muda mrefu unatakiwa kufanywa, kwani uvimbe wa ubongo kwa kawaida unachukua muda mrefu sana hadi unapotokea.
Si vibaya kujua kuwa, utafiti huo umetolewa baada ya kuchunguzwa kesi 59,684 za kensa ya ubongo zilizookea katika miaka 30 tangu mwaka 1974 hadi 2003 kati ya watu wazima milioni 16.

Saturday, December 5, 2009

Usafi na Utunzaji wa Meno ya Watoto ....sehemu ya kwanza


Utunzaji wa meno ya watoto unahitaji uangalizi mkubwa kama ilivyo kwa watu wazima, na upuuzaji wa suala hilo unaweza kuwa na madhara ya muda mrefu maishani. Hii ndio maana madaktari wa meno wanashauri kuwa, ni vyema meno ya watoto yakaanza kusafishwa tangu pale linapochomoza au kuota jino la awali kinywani na ikiwezekana hata kabla ya hapo. Baadhi ya wataalamu wanashauri wazazi kutumia kitambaa na maji safi kusafishia meno ya mtoto, huku akiwa ameketi katika hali ya utulivu. Itafahamika kuwa bacteria au vijidudu maradhi huishi kwenye sehemu ile ya jino iliyofunikwa na utando wa vyakula uliong'ang'ania kwenye jino. Bacteria hao hukutana na chakula na kusababisha asidi na hatimaye hutengeneza tundu au mmomonyoko katika meno. Utando huo unapaswa kuondolewa kila siku wakati unapopiga mswaki ili kuhakikisha kuwa meno na fizi zako ni safi na salama. Wazazi wanapaswa kuzingatia usafi wao wa kinywa pamoja na wa watoto wao. Vijidudu hivyo maradhi vinapatikana ndani ya mate na kwa hivyo ni rahisi kuenezwa kutoka kwa mzazi hadi kwa moto wakati wa kubusiana au kushumiana na kupitia uchangiaji wa vyombo vya chakula. Wazazi au walezi wanapaswa kubeba jukumu la kusimamia afya ya vinywa cha watoto wao hadi hapo watakapofikia umri wa kati ya mia minane au tisa. Kwani wataalamu wanasema kuwa katika kipindi hicho, watoto huwa hawana uwezo wa kujisimamia katika kuboresha usafi wa meno unaotakikana. Mtoto anaweza kuanza kusafisha meno yake kwa kutumia mswaki vile inavyotakikana chini ya usimamizi wa wazazi au walezi akiwa na umri wa miaka saba.
Usafi wa kinywa na meno unapaswa kuanzishwa hata kabla ya mtoto hajaanza kuota meno. Fizi za watoto wachanga na wale wa chekechekea zinaweza kusafishwa kwa kufutwa kwa utaratibu kwa kutumia shashi au gauze, au hata kitambaa kisafi chenye unyevunyevu. Kitendo hicho huchangamsha pia fizi za mtoto na kusaidia kupunguza baadhi ya maumivu ambayo huwapata watoto wakianza kuota meno. Madaktari wa meno wanasema kuwa, mara meno ya mtoto yanapochomoza, yanapaswa kusafishwa kwa mpangilio angalau mara mbili kwa siku, baada ya kifungua kinywa na kabla ya kulala, yaani usiku, bila ya kusahau ulimi.

Thursday, December 3, 2009

Dalili za mshituko wa moyo… sehemu ya mwisho


Leo tutazungumzia dalili za mshitiko wa moyo na hivyo kukamilisha mada ya mshituko wa moyo.
Baadhi ya wakati mshituko wa moyo hutokea kwa dalili zilizo wazi na kwa haraka sana. Lakini mara nyingi mshituko wa moyo hutekea polepole huku mtu akipata mauvimu ya wastani na kutokujisikia vyema. Mara nyingi watu wanaopatwa na hali kama hiyo huwa hawana uhakika na kile kinachotokea na husubiri kwa muda mrefu kabla ya kuomba msaada au kumuona daktari. Zifuatazo ni dalili ambazo hutekea pale mtu anapopatwa na mshituko wa moyo.
• Maumivu katika kifua: Mara nyingi mtu anapopatwa na mshituko wa moyo huhisi maumivu sehemu za kifua hasa sehemu za katikati ya kifua ambayo huweza kuisha baada ya dakika kadhaa au mara nyingine maumivu hayo huisha na kurudia tena. Mtu huhisi kana kwamba kifua kinabana, kimejaa na kinauma.
• Maumivu katika sehemu za juu za kiwiliwili: Mtu anaweza akajihisi maumivu sehemu za mikono, mgongo, shingo, taya na tumbo.
• Kukosa pumzi au kushindwa kupumua: Hali hii huweza kutokea ikichanganyika na maumivu ya kifua au bila maumivu hayo.
• Dalili nyinginezo: Dalili nyinginezo ni pamoja na kutoka kijacho chembemba (cha baridi), kujisikia kichefuchefu pamoja, kichwa kuwa chepesi na kizunguzungu.
• Moyo kwenda mbio. Kuhisi mapigo ya moyo yanapiga zaidi kuliko kawaida.
Unashauriwa iwapo utajiskia mumivu ya kifua, hasa pamoja na mchanganyiko wa moja wa dalili tilizotaja hapo huu, usisubiri zaidi ya dakika na haraka mpigie simu daktari au wasiliana na kituo cha afya ili upatiwe msaada. Au haraka elekea hospitali mwenyewe. Muda unaofaa wa kutibiwa mshituko wa moyo ni saa moja tangu wakati hali hiyo ilipotokea. Kutibiwa mapema dalili za mshituko wa myo hupunguza hatari ya kuharibika seli za moyo. Hata kama huna uhakika dalili unazohisi ni za mshituko wa moyo, ni bora umuone daktari na ufanyiwe uchunguzi.
Utafiti waliofanyiwa wanawake 515 ambao walipata mshituko wa moyo umeonyesha kuwa, wengi wao waliripotiwa kuwa na dalili za kujihisi kuchoka, kutokulala vyema, kushindwa kupumua, kujisikia maumivu baada ya kula na wasiwasi. Asilimia 70 ya wanawake hao walihisi dalili zisizopungua moja kabla ya kupatwa na mshituko wa moyo.

Monday, November 30, 2009

Binadamu anaweza kusikia kwa kupitia ngozi!


Huku masikio yakiwa hayachukuliwa tena kuwa ni njia pekee ya kusikia mwanadamu, uchunguzi mpya umeonyesha kuwa ngozi pia inaweza kusaidia katika kuleta kusikia. Chunguzi za huko nyuma zilionyesha kuwa, ishara za macho kama vile mzungumzaji kutikisa kichwa zinaweza kuwa kuathiri namna mtua navyosiakia kitu. Na pia inajulikana kuwa zaidi ya masikio suala zima la kusikia sauti hufanywa pia kwa kupitia mifupa ya kichwa. Uchunguzi mpya hata hivyo umehitimisha kwamba kuna masuala mengineyo zaidi ya ishara za kusikia na macho ambazo zinaathiri suala zima la kusikia. Kwa mujibu wa utafiti huo uliochapishwa katika Jarida la Nature, binadamu wanaweza kutafisiri sio tu ishara zilizotolewa kwa macho, bali pia huweza kutafisri taarifa wanazohisi kupitia ngozi zao wakati wanaposikia jambo. Wanasayansi wana matumaini kwamba ugunduzi wao huo utafungua njia ya kuimarishwa vifaa vya mawasiliano kwa ajili ya watu wasiosikia vyema.

Saturday, November 28, 2009

Jinsi ya kuhakikisha tunapata lishe bora na salama hata wakati wa Eid


Eid ni wakati ambapo familia zinakusanyika pamoja kula na kupeana zawadi na kusherehekea sikukuu hiyo adhimu. Kwa kawaida chakula kina nafasi muhimu wakati wa sherehe hizo. Sikukuu ya idil Adh-ha husherehekewa kwa mnasaba wa kumalizika kipindi cha Hijja ambapo Waislamu huenda kuzuru nyuma ya Mwenyezi Mungu katika mji mtukufu wa Makka. Katika sherehe hiyo kwa kawaida wanyama huchinjwa na kutolewa sadaka, ambapo nyama hugawanywa kwa ndugu na marafiki pamoja na masikini. Kwa kawaida chakula kinachopikwa katika siku ya iddi kinatofautiana kutoka nchi hadi nchi na jamii moja na nyingine. Lakini suala la muhimu ni kujitahidi kupata lishe iliyo salama na bora wakati wa kusherehekea sikukua ya Eid. Vyakula vinavyopikwa siku ya idi vinaweza kuwa salama lakini kwa kuwa ni wakati wa sherehe, ni rahisi kusahau kula vyakula ambavyo huweza kuhatarisha afya zetu. Ingawa ni siku ya sikukuu lakini Kona ya Afya inakutaka uwe mwangalifu kuhusiana na kile unachokula na kuipikia familia yako, huku ukijitahidi kupata chakula bora na salama. Hivyo ifuatayo ni njia ya kuifanya lishe yako ya Eid iwe salama:
• Jiepushe kula vyakula vyenye chumvi nyingi na mafuta mengi, na ni bora utumie viungo ambavyo pia vina faida tele mwilini.
• Ni bora utumie mafuta ya mimea (vegetable oli) badala ya kutumia siagi au mafuta ya mgando wakati wa kutayarisha msosi wa iddi. Epuka kutumia mafuta mengi kuliko kawaida, kwani mafuta mengi sio utamu wa chakula, bali ni hatari kwa afya yako.
• Wakati unaponunua nyama au vitoweo vinginevyo, hakikisha unanunua nyama salama, ambayo haijakaa sana na isiyokuwa na mafuta mengi. Iwapo ina mafuta jitahidi uondoe sehemu zenye mafuta kabla ya kupika.
• Hakikisha unaitayarishia na kuipikia familia yako na wageni mbalimbali mlo kamili wakati wa sikukuu. Sio wali na nyama pekee, pilau na ndizi tu, bali jitahidi kuwepo na mboga mboga na matunda pia. Halikadhalika jiepushe kupika kwa wingi vitu vyenye sukari nyingi.
• Ili kuhakikisha vitamini na madini zinabakia katika chakula unachopika, mboga mboga zisipikwe kwa muda mrefu na vilevile ili kuepuka minyoo na magonjwa mengineyo, hakikisha mboga na matunda vinaoshwa vyema.
• Wakati wa kupika chai ya maziwa wa vitindamilo vinginevyo (desserts) hakikisha unatumia maziwa yasiyo kuwa na mafuta mengi au low fat milk.
• Ili kuepuka kupika vyakula vya kukaanga na vyenye mafuta mengi, unaweza ukaoka vyakula hivyo badala ya kuvikaanga na ukapata ladha nyingine na kuwa bora zaidi kwa afya yako nay a familia yako kwa ujumla.
• Kunawa mikono na kuhakikisha usafi unazingatiwa, ni miongoni mwa mambo muhimu wakati w akutayarisha na kupika vyakula kwa ajili ya sikukuu.
Naam kina mama na kina dada, eid ni wakati wako mwingine ambao mbali ya kuonyesha ufundi wako wa kupika vyakula vitamu na vya kila aina kwa ajili ya wale uwapendao na wageni mbalimbali, hakikisha pia unazingatia afya ya walaji na kutunza afya kwa ujumla.
Eid Njema!

Eid Mobarak!


Nawatakia Eid njema wadau.
Msisahau kuzitunza vyema afya zenu.

Watu milioni 25 wamefariku dunia duniani kote kutokana na UKIMWI


Taarifa ya pamoja ya Shirika la Afya Duniani (WHO) pamoja na shirika la UNAIDS imesema kwamba, idadi ya watu waliofariki dunia duniani kote kutokana na ugonjwa wa Ukimwi imefikia milioni 25. Kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyotolewa hivi karibuni, inakadiriwa kwamba watu wengine milioni 33.4 wanaishi na virusi vya HIV duniani. Ripoti hiyo aidha imesema kwamba, karibu watu milioni 60 wakiwemo watu 25 milioni waliofariki dunia, wameambukizwa virusi vya HIV tangu ugonjwa huo ulipoanza. Ingawa idadi ya watu walioambukizwa ugonjwa wa HIV imeongeza, lakini takwimu za watu wanaofariki kutokana na ugonjwa huo, zimepungua ikilinganishwa na huko nyuma.
Matumizi ya dawa za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi au anti-retroviral drugs, yanaaminika kuwa yamepunguza kwa asilimia 10 vifo vinavyotokana na magonjwa yanayoambatana na ugonjwa wa Ukimwi katika miaka mitano iliyopita.
Ripoti hiyo pia imesema kwamba, bara la Afrika bado ni sehemu yenye maambikizo makubwa zaidi ya virusi vya Ukimwi ikilinganishwa na sehemu nyinginezo duniani na kwamba ugonjwa huo unasababisha nusu ya wakinamama wanojifungua kufariki dunia katika bara hilo.

Monday, November 23, 2009

Sababu kuu zinazomfanya mtu aweze kupata mshituko wa moyo!..sehemu ya 2


Kwanza tutazungumzi baadhi ya sababu zisizoweza kuzilika zinazosababisha mshituko wa moyo. Nazo ni kama ifuatavyo:-
Kuongezeka umri: Asilimi 83 ya watu wanaokufa na magonjwa ya moyo ni wale waliofikia umri wa miaka 65 na kuendelea. Umri unapokuwa mkubwa, wanawake ambao kwa kawaida hawapatwi sana na ugonjwa moyo, nao pia huanza kukabiliwa na hatari ya magonjwa hayo ukiwemo mshituko wa moyo.
Jinsia ya kiume: Wanaume wanakabiliwa na hatari zaidi ya kupatwa mashituko wa moyo kuliko wanawake, ambapo hupata ugonjwa huo katika umri mdogo. Wanawake baada ya kukatika hedhi au menopause, nao pia huanza kukabiliwa na hatari hiyo lakini si kwa kiasi kikubwa kama wanaume.
Urithi: Watoto ambao wazazi wao wana na magonjwa ya moyo au walipatwa na mshituko wa moyo nao pia wanakabiliwa na hatari ya kupaatwa na magonjwa hayo. Waamerika Weusi wanapatwa na shinikizo la damu zaidi wakilinganishwa na watu wenye asili ya Caucasian au wazungu. Magonjwa ya moyo pia hutokea sana kwa watu wenye asili ya Mexico, India, Hawaii na Asia. Watu ambao familia zao zina historia ya magonjwa ya moyo wanakabiliwa na hatari ya kupatwa na mshituko wa moyo mara mbili zaidi kuliko wengine, kwani mtu hawezi kuchagua umri wake, jinsia na asili yake.
Zifuatazo sasa ni baadhi ya sababu zinazoweza kuepukika zinazosababishwa mshituko wa moyo:-
 Kuvuta sigara: wavuta sigara wanakabiliwa na hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo mara 2 hadi 4 zaidi ya watu wasiovuta sigara. Uvutaji sigara ni sababu kubwa inayojitegemea inayoweza kusababisha mshituko wa moyo kwa wagonjwa wenye maradhi ya moyo. Kuvuta sigara hadhani au mbele ya wengine kunawafanya watu hao nao wakabiliwe na hatari hiyo magonjwa ya moyo.
 Kiwango kikubwa cha mafuta katika damu au High Blood Cholesterol: Kila kiwango cha mafuta kinapoongezeka katika damu ndio uwezekano wa kupatwa na magonjwa ya moyo nao unavyoongezeka. Iwapo mtu atakuwa na sababu nyinginezo kama ufutaji sigra, shinikizo la damu na kadhalika, basi mtu huyo ana uwezekano mkubwa zaidi wa kupata shinikizo la moyo. Kiwango cha mafuta katika damu pia kinathiriwa na umri, jinsi, urithi na lishe.
 Shinikizo la damu: Shinikizo la damu huongeza ufanyajikazi wa moyo, suala linalopelekea mishipa ya moyo iwe minene na migumu. Pia huongeza hatari ya kupata mshituko wa moyo, mshituko wa ubongo, figo kutofanya kazi na moyo kushindwa kufanya kazi. Shinikizo la damu linapokuwa pamoja na unene wa kupindukia, uvutaji sigara, kiwango cha juu cha mafuta kwenye damu au kisukari, humfanya mtu apatwe kwa urahisi na mshituko wa moyo.
 Kutoushughulisha mwili: Kuishi maisha yasiyokuwa ya kushughulika kifizikia ni miongoni mwa sababu za kupatwa na ugonjwa wa moyo. Shughuli za kawaida husaidia kuzuia magonjwa ya moyo na kuongezeka kiwango cha mafuta katika damu. Unapoushughulisha mwili wako zaidi ndivyo unavyojisaidia zaidi kiafya. Kushughulisha mwili husaidia kudhibiti kisukari, unene wa kupindukia, kiasi kikubwa cha mafuta katika damu na hata kupunguza shinikizo la damu.
 Unene wa kupindukia au Obesity: Watu wenye unene wa kupindukia wana mafuta mengi mwilini na iwapo mafuta yamejikusanya katika nyonga na kiuno wanaweza kukabiliwa na hatari ya kupata mshituko wa moyo. Unene mkubwa huufanya moyo ufanye kazi zaidi. Pia huongeza shinikizo la damu na kiwango cha mafuta katika damu. Halikadhalika unene humsababisha mtu apatwe na kisukari.
Sababu nyinginezo ni pamoja na
 Mtu kuwa na mawazo na fikra kila mara, kwani wataalamu wanasema kuwa kuna uhusiano kati ya kuwa na mawazo na fikra na magonjwa ya moyo. Kwani mtu mwenye mawazo mengi kwa kawaida huwa na ghadhabu, huenda akavuta sigara na mengineyo ambayo huweza kupelekea ugonjwa wa hatari.
 Kunywa sana pombe: Kunywa sana pombe husababisha shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na kupelekea mshituko wa moyo. Pia huongeza kiasi cha mafuta katika damu, kensa na magonjwa mengineyo na hata husababisha moyo kupiga hovyo. Vilevile huchangia katika kusababisha unene wa kupindukia, ulevi wa kupindukia, kujiua na ajali.

Saturday, November 21, 2009

Kitunguu swaumu kinazuia influenza!



Kitunguu swaumu tangu kale kimekuwa kikijulikana kama 'dawa ya kushangaza' na kutumiwa na watu wengi katika kutibu mafua na influenza. Miongoni mwa faida za kitunguu swaumu ni kuzuia kupatwa na magonjwa mbalimbali na maambukizo ya virusi. Hivyo kitunguu swaumu hujulikana kama antibiotiki ya asilia. Uchunguzi umeonyesha kwamba kula kitunguu swaumu kunapunguza kushadidi ugonjwa wa influenza na hata kuzuia kupatwa na ugonjwa huo. Vilevile kula kila mara kitunguu swaumu, huzuia kupatwa na magonjwa ya moyo, kwani kitunguu swaumu huzuia damu isigande kwenye mishipa ya damu.
Halikadhalika kitunguu swaumu ambacho pia ni kiungo muhimu cha chakula kina potassium, na hivyo watu wenye ugonjwa wa shinikizo la damu wanashauriwa kula vyakula vilivyopikwa kwa kitunguu swaumu.
Si vibaya kujua kuwa katika uchunguzi uliochapishwa mwaka 2001, imeelezwa kwamba, kitunguu swaumu kina athari kubwa na nzuri pale kinapochanganywa na baadhi ya dawa nyinginezo katika kutibu Ukimwi au HIV.
Haya shime jamani… kuanzia leo vyakula visikose kuungwa na kitunguu thomu, iwapo unaogopa kupatwa na influenza kama mimi!

UNICEF yasema, Afghanistan ndiyo sehemu mbaya zaidi ya kuzaliwa mtoto duniani


Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF) limesema kuwa nchi ya Afghanistan iliyoharibiwa kwa vita ni sehemu mbaya zaidi duniani ya kuzaliwa mtoto. Shirika hilo limetangaza kwamba, Afghanistan ina idadi kubwa zaidi ya vifo vya watoto duniani ambapo vifo 257 vya watoto hutokea kati ya kila watoto 1,000 wanaozaliwa.
Daniel Toole Mkurugenzi wa Unicef wa kusini mwa Asia amesema kwamba, ripoti yake ya mwaka kuhusiana na watoto duniani imegundua kwamba, Afghanistan ni sehemu hatari kwa wasichana na kwamba kukosekana usalama kumepunguza idadi ya watoto wanaohudhuria shuleni hasa wa kike. Aidha mkurugenzi huyo wa Unicef amelaumu mashambulio ya mara kwa mara ya shule za wasichana ambayo yamesababisha elimu ya wanawake kuporomoka kabisa nchini Afghanistan.

Friday, November 20, 2009

Haya kinadada macho juu!…. Viagra ya wanawake yagunduliwa!


Wataalamu wamegundua bila kutarajia Viagra ya wanawake, wakati walipokuwa wakifanya uchunguzi wa dawa ya kuondoa mfadhaiko wa mawazo au antidepressant. Katika majaribio matatu tofauti, imeonekana kuwa dawa iitwayo flibanserin ina athari ya ajabu katika kuongeza nguvu za kufanya mapenzi kwa wanawake, bila dawa hiyo kuwa na athari yoyote katika kuondoa mfadhaiko wa fikra. Wanasayansi hao wa Chuo Kikuu cha Carolina Kaskazini nchini Marekani wamesema kuwa, katika chunguzi huo usiokuwa wa kutarajiwa, imeonekena kuwa dawa hiyo inaongeza nguvu za kujamiina kwa wanyama wa maabara na binaadamu pia. Wamesema kuwa, ni muhimu kupatikana dawa kama Viagra kwa wanawake, kwani itatumiaka kutibu kutokuwa na matamanio ya kufanya mapenzi au libido kitaalamu, ambayo ni moja ya matatizo sugu ya kijinsia waliyonayo wanawake.

Seli mama zinaweza kutengeneza ngozi mpya kwa walioungua moto


Wataalamu wa Ufaransa wamesema kuwa, wamegundua njia mpya ya kutumia seli mama za kiini tete cha mwanaadamu (human embryonic stem sells) kutengeneza ngozi mpya ambayo inaweza kutumika kwa watu waliongua na moto. Wamesema kuwa, katika uchunguzi wao seli mama imeweza kuota na kuwa ngozi kamili, wiki 12 baada ya kupandwa katika panya wa maabara. Wataalamu hao wameonyesha matumaini yao kwamba, ngozi hiyo inaweza kutatua tatizo la kuangaliwa vibaya na hata kukataliwa wagonjwa walioungua vibaya na moto katika jamii. Wataalamu wa seli mama wamesema kwamba, ugunduzi huo ni mafanikio muhimu.
Kwa zaidi ya miaka 20 sasa wagonjwa walioungua vibaya kwa moto wamekuwa wakitumia teknolojia inayokuza ngozi mpya katika maabara, lakini kwa kutumia seli za ngozi zao wenyewe. Lakini teknolojia hiyo inachukua wiki tatu, suala ambalo linamfanya mgonjwa aliyeungua akabiliwe na hatari ya kupoteza maji ya mwili na kupata maradhi mbalimbali au infection.

Thursday, November 19, 2009

Mapacha wa Baghaladesh waliokuwa wameungana waachanishwa


Timu ya madaktari 16 wa Australia wamefanikiwa kuwatenganishwa watoto mapacha wa Bangladesh waliokuwa wameungana kwa miaka mitatu, katika operesheni iliyochukua masaa 27. Trishna na Krishna ni watoto mayatima wa Bangladesh waliokuwa wameungana katika sehemu za juu za kichwa na kuwa na mishipa ya damu ya pamoja. Madakatari wataalamu wa masuala ya ubongo wa Australiwa katika oparesheni hiyo waliugawa ubongo wa watoto hao kwa tahadhari kubwa na kuwaachanisha. Watoto hao wadogo wa kike walikuwa mahututi walipowasili nchini Australia miaka miwili iliyopita, ambapo tayari walikuwa wameshafanyiwa operesheni kadhaa za utangulizi. Madakatari huko nyuma walisema kuwa kwa kufanyiwa operesheni huo kulikuwa na uwezekano wa asilimia 25 kwamba mmoja kati ya mapacha hao angekufa na asilimia 50 watoto wote hao wawili wanngepatwa na matatizo ya kuharibika ubongo. Lakini Mkuu wa kitengo cha Upasuaji wa hospitali ilipofanywa oparesheni hiyo Dakta Leo Donnan amesema kuwa, watoto hao wanaendelea vyema baada ya kufanyiwa operesheni hiyo, lakini bado wako katika chumba cha uangalizi maalum wakisubiri operesheni nyingine ya kuzishona tena ngozi zao, mifupa na kuongezewa baadhi ya viungo bandia. Oparesheni za kuwatenganisha mapacha walioshikana ni kazi nzito ambayo kwa kawaida huwa hazifanywi katika hospitali mbalimbali duniani. Operesheni hizo zinapofanywa mara nyingi hupelekea vifo vya mapacha hao. Mapacha wanaoungana au Conjoined Twins hutokea kwa uchache katika mimba, mara moja katika kila kesi 200, na huwa katika mapacha wanaoshabihiana au identical twins. Mara nyingi hata kama mimba kama hizo zitatungwa lakini kwa asilimia 40 au 60 watoto hao hufia tumboni, au watoto wanaozaliwa kufariki dunia siku chache baada ya kuzaliwa. Mimba za mapacha wanaoungana kwa asilimia 70 huwa ni za watoto wa kike, sababu ambayo haijulikana.

Monday, November 16, 2009

Kumbuka yafuatayo kabla ya kupaka rangi nywele zako


• Osha nywele zako vizuri kwa shampuu kabla ya kuweka rangi.
• Usiweke kondishena na usitumie shampuu zenye kondishena kwani kondishena itasababishwa rangi isiingie vyema katika nywele.
• Iwapo kichwa chako ni sensitive au nywele zako zimeharibika au kavu, subiri dakika 12 hadi 24 baada ya kuosha ndio upake dawa ya kubadilisha nywele rangi.
• Na wakati unapopaka dawa ya kutia rangi nywele fuata maelekezo vizuri kama yalivyoandikwa.
• Tumia glavu pamoja na taulo, rangi ya nywele inaweza kukuchafua kila mahali, hasa ikiwa katika suala hili wewe si mjuzi.
• Ili kuzuia rangi ya nywele kuingia katika ngozi yako, unaweza kupaka vaselini kuzunguka kichwa, lakini hakikisha haiingia katika nywele kwani inaweza kuingiliana na rangi na kufanya rangi isikole vyema.
• Iwapo rangi itaingia katika ngozi yako, usihofu itaondoka baada ya kuoga mara mbili au tatu. Na wakati unapaka rangi iwapo utaiona imeingia katika ngozi, hapo hapo chukua tishu au karatasi laini na ipake shampuu kidogo na uifute. Itatoka bila matatizo yoyote.
• Tumia kondishena baada ya kuzipaka rangi nywele zako. Ni bora utumie kondishena ambayo ni maalum kwa ajili ya nywele zilizotiwa rangi.

Kinadada wasihofu tena…. kwani rangi za nywele hazisababishi kensa!


Taasisi ya Ujerumani ya kuchunguza hatari za vitu imetangaza kwamba rangi za nywele hazisabishi kensa. Uchunguzi wa taasisi hizo umesema kuwa mada zinazosababishwa kensa hazijashuhudiwa katika rangi za nywele. Hata hivyo taasisi hizo imesema kuwa uchunguzi unatakiwa kufanywa zaidi ili kujua iwapo katika rangi hizo kunatiwa mada ambazo husababisha allergy kwa watumiaji.

Saturday, November 14, 2009

Leo ni Siku ya Kimataifa ya Ugonjwa wa Kisukari



Leo ni Jumamosi tarehe 14 Novemba ambayo ni siku ya kimataifa ya ugonjwa wa kisukari au diabete. Hii ni siku ambayo kampeni za tahadhari hufanywa dunia nzima kuhusiana na ugonjwa wa kisukari. Kwa ajili hiyo Shirika la Afya Dunia (WHO) pamoja na taasisi nyingine za Tiba na Afya duniani, zikishirikiana na madaktari, wataalamu na wadau wa Afya uliwemnguni kote, hutumia siku hii ili kuelimisha na kufunza zaidi jamii kuhusiana na ugonjwa wa kisukari. Taasisi ya Kisukari ya Kimataifa inakadiria kuwa watu milioni 344 duniani wako katika hatari ya kupatwa na ugonjwa wa kisukari aina ya pili, au Type 2 Diabates. Idadi hiyo ni sawa na idadi yote ya wananchi wa Marekani, iwapo utawahesabu wakaazi wa California mara mbili. Taasisi hiyo pia imetangaza kuwa, watu milioni 285 tayari wanasumbuliwa na ugonjwa huo duniani kote.
Kwa mnasaba huo basi Kona ya Afya inachukua fursa hiyo kuelezea ni nini ugonjwa wa kisukari?
Kisukari ni ugonjwa unaotokea pale mwili unaposhindwa kusaga vyema chakula ili kutoa nishati na kusaidia ukuaji wa mwili. Kila tunachokula husangwa na kubadilishwa kuwa glukosi. Glukosi ni aina ya sukari kwenye damu ambayo ndio chanzo cha nishati au kama mafuta kwa ajili miili yetu.
Baada ya chakula kuyeyushwa hushika njia kuelekea katika damu. Seli zetu za mwili hutumia glukosi kama chanzo cha nishati na kukua. Hata hivyo, glukosi haiwezi kuingia katika seli zetu za mwili bila kutumia wenzo unaoitwa insulini. Insulin huwezesha seli zetu za mwili kuchukua glukosi. Insulini ni homoni ambayo inatengenezwa na kongosho au pancreases.
Tukishwa kula chakula, kongosho zenyewe hutoa kiasi cha kutosha cha insulini kinachoweza kuhamisha glukosi iliyoko kwenye damu kwenda kwenye seli, na kwa njia hiyo kiwango cha sukari katika damu hupungua.
Mtu mwenye kisukari ana hali ambayo kiwango cha sukari katika damu yake kiko juu sana au hyperglycemia. Hii husababishwa na moja kai ya hali tatu zfuatazo. Moja ni kwa sababu mwili huwa hauwezi kutoa kiasi cha Insulini inayotakiwa . Mbili ni pale inapokuwa hakuna insulini inayotengenezwa mwilini, na tatu ni pale seli za mwili zinapokuwa hazishughuliswi ipaswavyo na insulini inayotengenezwa na kongosho.
Matokeo ya hali hizo hupelekea kujikusanya sukari kwa wingi katika damu. Sukari hiyo nyingi kwenye damu polepole hutoka nje ya mwili kama mkojo. Hivyo, ingawa damu ina kiasi kikubwa cha sukari, lakini seli za mwili haziwezi kuitumia sukari hiyo ili kukidhi mahitaji muhimu ya kuupatia mwili nishati na nishati na kwa ajili ya kukua.
Kuna aina tatu za Kisukari.
1. Kisukari aina ya kwanza au Diabates Type 1, aina hii hutokea pale mwili unaposhindwa kuzalisha insulini kabisa.
2. Kisukari aina ya pili au Diabates Type 2, aina hii hutokea pale mwili uanapozalisha insulini lakini insulini hiyo ikawa haiwezi kutumika ipaswavyo.
3. Kisukari cha Ujauzito au Gestational Diabates, kisukari cha aina hii hutokea wakati wa ujauzito.
Inafaa kufahamu kuwa kisukari aina ya kwanza na ya pili ni magonjwa sugu, ikimaanishwa kuwa ni ugonjwa unaoendelea na kwa kawaida mara nyingi hautibiki na kumalizika, bali mgonjwa hubakia nao umri wake wote. Lakini kisukari cha wakati wa ujauzito kwa kawaida hutokea tu wakati huo wa mamba, na baada ya mtoto kuzaliwa ugonjwa huo huisha.

Friday, November 13, 2009

Mshituko wa Moyo ( Heart Attack) au Myocardial Infarction….sehemu ya kwanza



Mshituko wa moyo unatokea wakati mzunguko wa damu katika misuli ya moyo unapozuiwa. Iwapo mzunguko huo wa damu hautoendelea haraka, kitendo hicho huifanya misuli ya moyo kuharibika kwa kukosa oksijeni na huaza kufa. Mshituko wa moyo kwa lugha ya tiba unajulikana kama 'Myocardial Infarction' inayomaanisha "Myo".. muscles au msuli, 'cardio'…. Heart au moyo, "infrct"….death of tissue from lack of oxygen au kufa tishu kwa kukosa oksijeni.
Kama vilivyo viungo vingine mwilini hasa misuli, moyo nao huhitajia damu. Bila damu seli za moyo hudhoofika suala ambalo hupelekea mtu kuhisi maumivu. Shinikizo la damu hutokea pale mshipa mmoja wa damu au zaidi inaposhindwa kusafirisha damu yenye oksijeni katika moyo, kutokana na kuziba mishipa hiyo. Mishipa ya damu inaweza kuziba kutokana na:
1. Kuta za mishipa ya damu inayopeleka damu kwenye moyo (coronary arteries) kuwa nene.
2. Chembechembe za mafuta kukusanyika katika mishipa ya damu.
3. Kudhoofika na kukonda mishipa ya damu.
4. Mishipa ya damu mara inaposinjaa na kushikana au spasm.
5. Kujitokeza donge la damu katika mishipa ya damu.

Lakini ni wakati gani mtu anakabiliwa na hatari ya kupata mshituko wa moyo?
• Kuongeza umri au umri mkubwa
• Unene wa kupindukia
• Kuvuta sigara
• Shinikizo la damu
• Maisha yasikuwa na harakati na kujishughulisha (sedentary lifestyle)
• Kiwango cha juu cha mafuta katika damu ( High Blood Cholesterol)
• Kisukari
• Kuwa na mawazo, wasiwasi na fikra nyingi.
• Baadhi ya magonjwa ya moyo.
• Kufanyiwa operesheni ya moyo.
• Kuwa na ndugu ambao wana matatizo ya moyo.
• Wanaume.
……msikose kuungana nami katika sehemu ya pili ambapo tutajadili kwa undani sababu hizo na mengineyo.

Thursday, November 12, 2009

Ongezeko la vifo vya UKIMWI nchini Afrika Kusini


Waziri wa Afrika wa Afrika Kusini amesema kwamba kiwango cha watu wanaofariki duniani nchini humo kimeongezeka mara mbili katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kutokana na kuenea ugonjwa wa Ukimwi. Aaron Motsoaledi ameilaumu serikali iliyopita ya nchi hiyo wa Rais Thabo Mbeki akisema kwamba ilisababisha kupanda sana kiwango cha vifo nchini humo katika kipindi cha baina ya mwaka 1997 hadi 2008. Amesema karibu watu laki tatu walifariki dunia nchini Afrika Kusini mwaka 1997 ambapo mwaka 2007 idadi hiyo ilipanda na kufikia karibu watu laki 7 na 56 elfu. Waziri huyo wa afya wa Afrika Kusini ameongeza kuwa, kutokana na kuongezeka idadi ya vifo nchini humo, serikali ya hivi sasa imeamua kufanya marekebisho ya kimsingi katika siasa zake ili kupambana na ongezeko la ugonjwa hatari wa Ukimwi nchini humo. Idadi kubwa ya wahanga wa Ukimwi nchini Afrika Kusini ni vijana. Waziri wa Afya wa nchi hiyo anasema kwamba karibu asilimia 75 ya vifo vya watoto wadogo nchini humo vilitokea mwaka 2007 kutokana na ugonjwa wa Ukimwi. Hatua ya Waziri Aaron Motzoaledi ya kulaumu ongezeko la wahanga wa Ukimwi katika kipindi cha Urais wa Thabo Mbeki, kwa mara nyingine kunaonyesha hitilafu za wazi zilizopo baina ya Rais huyo wa zamani na Rais Jacob Zuma wa hivi sasa wa Afrika Kusini kuhusiana na namna ya kupambana na Ukimwi nchini humo. Itakumbukwa kwamba katika kipindi cha Urais wake, Thabo Mbeki alitilia shaka hata uhakika uliothibitishwa kielimu kwamba Ukimwi unasababishwa na virusi vya HIV. Hata Manto Msimang Waziri wa Afya wa serikali ya Thabo Mbeki aliwataka watu wenye virusi vya HIV nchini humo watumie mboga mboga badala ya dawa za kupambana na virusi hivyo. Alitoa mwito huo katika hali maelfu ya wananchi wa Afrika Kusini walikuwa wakiendelea kufa kwa Ukimwi kutokana na ukosefu wa madawa. Hivi sasa na licha ya kuwa Afrika Kusini ina mradi mkubwa zaidi wa kupambana na Ukimwi duniani lakini bado inatathminiwa kwamba karibu watu milioni moja wanahitajia kutibiwa ugonjwa huo nchini humo.

Wednesday, November 11, 2009

Vyakula vinavyosaidia mwili kujilinda na maambukizo ya homa ya mafua ya nguruwe



Kula karoti, uyoga, komamanga na chai ya kijani ( green tea) kunasaidia kuulinda mwili katika kukabilina na kupatwa na ugonjwa wa homa ya mafua ya nguruwe.
Kama mnavyojua kila siku zinavyokwenda, ndivyo idadi ya watu wanaopatwa na influenza aina ya H1N1 inavyoongezeka duniani kote, basi tunapaswa kujua namna ya kuilinda miili yate ili kuepuka kupatwa na ugonjwa huo. Wataalamu wameelezea vyakula kama vile karoti, uyoga, komamanga na chai ya kijani huufanywa mfumo wa kulinda mwili kuwa na uwezo wa kukabiliana na virusi hivyo hatari vinavyosababishwa hama ya mafua ya nguruwe.
 Karoti zinaonekana kufaa sana katika suala hilo kwani zina mada ya beta carotine husaidia mwili katika kukabiliana na ugonjwa huo. Imeonekana kuwa kila betacarotine inavyokuwa mwilini kw aingi ndivyo seli za kulind amiwli zinavyoongezeka.Basi tutumie karoti katika vyakula vyetu ikibidi kila siku. Tunaweza kutengeneza saladi, juice ya karoti au hata maji ya karoti na maziwa.
 Uyoga nao vile vile huimairisha kinga ya mwili na ni chakula kinachoupatia mwili protini pia. Tunaweza kupika uyoga kama mboga au kuutumia katika saladi, sosi au kuuchanganya katika vyakula vinginevyo kama vile pizza n.k.
 Komamanga ni tunda ambalo linasifika sana kwa kuwa na uwezo wa anti oxidanti ambapo anti oxidant huzuia radikali huru ambazo ni hatari sana kwa mwili wetu. Uwezo huo humepekea mwili kukabilina na magonjwa mbalimbali ukiwepo ugonjwa wa homa ya mafua ya nguruwe. Kama huwezi kupata tunda la Komamanga sokoni, basi unaweza kutumia juisi ya kamamanga.
 Chai ya kijani (Green Tea) ina aina mojawapo ya anti oxidanti inayojulikana kama Catechin ambayo huweza kuongeza seli za kulinda miwli. Wataalamu wanasema kuwa Catechin huvipavya virusi vya homa ya mafua ya nguruwe visiweze kusambaa mwbilini.Tusisahau pia kuwa mojawapo ya faida za chai ya kijani ni kuwa husadia kuongeza umri wa mtu na kuimarisha mfumo wa kulinda mwili.

Monday, November 9, 2009

Kula nyanya kwa Afya yako!


Pengine wengi tunafikiri nyanya hazina umuhimu sana kwa mwili, lakini labda kwa kujua yanayopatikana ndani yake, tukabadilika mawazo yetu. Nyanya si kiungo cha chakula tu kinachotoa ladha nzuri kwenye mchuzi na kachumbari lakini pia zina faida kubwa kwa mwili.
Nyanya inaupatia mwili wetu faida zifuatazo.
• Vitamin C, A na K
• Pottasium
• Manganese
• Ufumwele
• Cromium
• Vitamini B1 na B6
• Chuma
• Kopa
• Vitamin B2 na B3
• Magnesium
• Folate, Phosphorous
• Protini ingawa kwa kiasi kidogo.
• Tryptohan, Folate na Molybdenum.

Kweli inabidi kwa kujua hivyo, tusiidharua nyanya tena!

Sunday, November 8, 2009

Unene wa kupindukia, ndio chanzo cha kesi 100,000 za kensa nchini Marekani



Unene wa kupindukia au Obesity unaaminiwa kuwa ndio sababu ya kutokea zaidi ya kesi 100,000 za kensa kila mwaka nchini Marekani, huku unene pia ukiwa unamletea mtu hatari ya kupatwa na magonjwa mengi kama vile kisukari na hata homa ya mafua ya nguruwe. Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Kitengo cha Utafiti wa Kensa cha Marekani, unene unasababisha aina mbalimbali za kensa, zikiwepo kesi 33,000 za kensa ya matiti, unene ambao unaweza kutokana na lishe isiyofaa, kukosekana harakati pamoja na kuwa na mafuta mengi mwilini.
Taarifa hiyo pia imesema kwamba, tatizo la kuwa na unene wa kupindukia lina athari kubwa tatu katika aina saba za saratani. Imeonekana ushahidi wa kuwepo uhusiano kati ya unene au obesity na kensa za mfumo za koo, kongosho, figo, matiti na utumbo.
Wataalamu wanasema kuwa, mafuta mengi mwilini huongeza kiwango cha homoni aina ya steroids na homoni nyinginezo ambazo zinahusiana na kutokea kensa. Seli za mafuta ni maarufu kwa kutengeneza ostrogen, ambayo imeonekana kuwa inashajiisha ukuaji wa seli katika kensa ya matiti. Halikadhalika mafuta mengi mwilini hupunguza uwezo wa kinga ya mwili na kuongeza mada za oxidative ambazo hupelekea kuharibika DNA na mwishowe kusababisha saratani.
Inakadiriwa kuwa asilimia 49 ya kesi za saratani ya kizazi ambayo ni aina maarufu zaidi ya kensa za mfumo wa uzazi, na asilimia 35 ya kesi za saratani ya koo nchini Marekani zinahusiana na unene wa kupindukia.
Inafaa kuashiria hapa pia kuwa, asilimia 34 ya Wamarekani wenye umri wa miaka 20 na kuendelea wana unene wa kupindukia au Obesity.

Saturday, November 7, 2009

Soda za kupunguza uzito (Diet Soda) husababisha matatizo ya figo


Wakati soda za kupunguza uzito au diet soda zin pendwa na kutumiwa sana hasa na watu wanaohofia suala la uzito wa miili yao na kiasi cha kalori wanazokula, uchunguzi mpya umeonyesha kuwa oada hizo zinasababisha matatizo ya figo.
Wataalamu wa Marekani wametangaza kwamba, kunywa soda mbili au zaidi za diet kwa siku, kunazidisha mara mbili uwezekano wa kupata matatizo ya figo. Katika uchunguzi huu, asilimia 30 ya wanawake wanaokunywa soda hizo mbili au zaidi kwa siku, wameonekana kuwa wamepatwa na matatizo ya figo yanayojulikana kama GFR au Glomerular Filtration Rate ambapo ugonjwa huo huzifanya figo zipoteze uwezo wake wa kuchuja vyakula.
Wataalamu hao pia wameongeza kuwa, kula chumvi nyingi nako kunapelekea figo zishindwe kufanya vyema kazi zake.

Tibu chunusi kwa kutumia limau!


Limau kulina tindikali aina ya citric ambayo inasaidia kuponya chunusi. Vilevile tunda hilo lina Vitamin C ambayo ni muhimu katika kuifanya ngozi iwe na afya wakati alkali inayopatikana katika limau nayo husaidia kuua vijidudu vinavyosababisha chunusi.
Kunywa juisi ya limau kama chakula cha kwanza asubuhi kunaaminika kusadia kuboresha ngozi.
Jinsi ya kutengeneza nyumbani mchanganyiko wa limau kwa ajili ya kutibu chunusi:
• Kwa kutumia pamba paka maji ya limau katika sehemu yenye chunusi na wacha kwa usiku kucha.
• Safisha kwa maji safi asubuhi inayofuata.
• Ingawa unaweza ukahisi kuwashwa wakati unapopatumia mchanganyiko huo juu ya ngozi mara ya kwanza, lakini baadaye hali hiyo huzoeleka.
Au

1. Changanya maji ya limau ulioyakamu kutoka katika kipnde kimoja cha limao na changanya na maji ya waridi (rose water) au asali nyepesi kwa kiwango hicho hicho.
2. Paka mchanganyiko huo katika sehemu za ngozi zenye chunusi na subiri kwa muda usiopungua nusu saa mpaka saa lizima.
3. Baadye osha kwa maji.
Mchanganyiko huu unapaswa kupakwa mara mbili kwa siku, bora utumiea asubuhi na jioni.
Muhimu: kutumia mchanganyiko huu hakuna madhara na ni wa asilia, lakini iwapo chunusi zinazidi au kuna vidonda vinavyoambatana na chunusi ni bora upate uchauri wa daktari kwanza.