Saturday, June 19, 2010

Kunywa maji kwa mpangilio husaidia kurahisisha utendaji wa mwili



Kila mtu anajua umuhimu wa maji katika miili yetu. Sio kwamba tu mwili wenyewe umejengwa kwa asilimia kati ya 55 na 75 za maji (kwa kutegemea unene wa mtu ambapo watu wembemba wana kiasi kikubwa cha maji mwilini kuliko wanene) bali pia mwili unahitajia maji kwa kiasi kikubwa ili kufanya kazi zake vyema.
Je? Unajua mapafu yako yanahitajia vikombe wiwili vya maji hadi vinne kila siku ili kufanikisha kwa ufanisi kazi yake ya kupumua? Na kiasi hicho huhitajika ziadi wakati wa baridi.
Je, unajua wakati unapotoka jasho kikombe kimoja cha maji hupungua mwilini mwako. Na je, unatambua kwamba iwapo utaoga wakati wa mchana kwa mara karibu tatu kwa siku ni kana kwamba umekunywa vikombe 6 vya maji?
Kunywa maji kwa kiasi cha kutosha husaidia kupunguza uwezekano wa kutokea mawe katika figo, hulainisha viungo na huzuia mafua na kusaidia kupona haraka ugonjwa huo. Vilevile kunywa maji husaidia mtu kupata choo vyema.
Maji ni hitajio la dharura kwa afya zetu, kwani asilimia 60 ya uzito wako ni maji na kila mfumo wa mwili wako hutegemea maji ili kufanya kazi zake. Ukosefu wa maji mwilini humfanya mtu akaukiwe na maji au dehydration, hali ambayo hutokea pale mtu asipokuwa na maji ya kutosha mwilini ya kuuwezesha mwili wake kufanya kazi zake za kawaida. Hata katika upungufu mdogo wa maji mwilini, wakati ambapo asilimia 1 hadi 2 ya uzito wa mwili inapopungua, huweza kumfanya mtu akose nguvu na ajisike amechoka. Miongoni mwa dalili za upungufu wa maji mwilini ni:
• Kukihi kiu sana
• Uchovu
• Kichwa kuuma
• Mdomo kukauka
• Kukosa mkojo au kiasi cha mkojo kuwa kidogo.
• Udhaifu wa misuli
• Kuhisi kizunguzungu


Ni muhimu kujua kwamba mwili hupoteza maji kila siku kwa kutokwa na jasho, iwe jasho hilo umelihisi au haukulihisi, kutoa pumzi nje (exhaling), kukojoa na harakati ya tumbo. (bowel movement). Ili mwili wako uweze kufanya kazi vizuri unahitajia kurudisha maji hayo mwilini kwa kunywa vinywaji mbalimbali na vyakula vyenye maji.
Wataalamu wengi wanakubaliana kuwa mwanadamu anahitajia kunywa vikombe 8 vya maji kwa siku, ili kufidia maji yanayopotae mwilini. Hata hivyo wengine wanashauri kwamba, wanaume wanywe vikombe 13 vya maji kwa siku na wanawake vikombe 8 vya maji, na hiyo ni kutokana na tofauti ya miili yao. Tunashauriwa kuwa badala ya kunywa maji kiholela tunywe kwa mpangilio maalum kwa siku, ili kusaidia vyema katika kazi za mwili.
 Tunashauriwa kunywa vikombe viwili vya maji asubuhi pindi tunapoamka, kwani husaidia kuamsha viungo vya ndani ya mwili.
 Tunashauri tunywe kikombe kikoja cha maji dakika 30 kabla ya mlo, kwani husaidia kupata choo vizuri.
 Tunashuariwa tunywe kikombe kimoja cha maji kabla ya kwenda kuoga, husaisia kupunguza shikizo la damu.
 Na tunashauriwa kunywa kikombe kimoja cha maji kabla ya kulala kwani kufanya hivyo huzuia shinikizo la moyo.
Basi kunywa maji kwa afya yako mdau!

Sunday, June 6, 2010

Kensa kuua watu milioni 13.2 ifikapo mwaka 2030


Maafisa wa Umoja wa Mataifa wametangaza kwamba, watu zaidi ya milioni 13.2 watafariki dunia ifikapo mwaka 2030 kutokana na maradhi ya kensa, idadi ambayo ni mara mbili ya ile ya mwaka 2008. Takwimu hizo za hivi karibuni zinaonyesha pia kwamba, ugonjwa wa saratani mwaka 2008 ulisababisha watu milioni 7.6 waage dunia na kwamba kesi mpya milioni 12.7 za kensa mbalimbali zimegunduliwa mwaka huu. Nchi zinazoendelea zimeripotiwa kuwa na asilimia 56 ya kensa mpya na asilimia 63 ya kensa zote zilizoripotiwa mwaka 2008. Kensa ambazo zilitokea kwa kiasi kikubwa mwaka 2008 ni kensa za mapafu, matiti na kensa ya utumbo, rectum na apendeksi au colorectal cancer. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Kimataifa cha Utafiti wa Kensa( IARC) kesi za ugonjwa wa kensa zitaongezeka mara dufu katika miongo miwili ijayo iwapo hali ya sasa itaendelea hivyo hivyo. Christopher Wild Mkurugenzi wa IARC amesema kwamba, maradhi ya kensa hakuna sehemu yoyote duniani yasipokuwepo, hata katika nchi zilizoendelea na zenye utajiri mkubwa. Amesisitiza kwamba la kusikitisha ni kuwa maradhi ya kensa ambayo mwanzoni yalishudiwa kwa wingi katika nchi zinzoendelea hivi sasa yapo pia katika nchi masikini.