Saturday, October 2, 2010

Marekani yaomba msamaha kwa kuwafanyia majaribio ya Kaswende wananchi wa Guatemala

Marekani imeomba msamaha kuhusiana na kuwaambukiza kwa makusudi ugonjwa mbaya wa kaswende, wafungwa, wanawake na wagonjwa wa akili wa Guatemala katika majaribio yaliyofanywa na watafiti wa serikali ya Marekani katika miaka ya 1940. Katika jinai hiyo ililofanywa kwa lengo la kujaribu dawa mpya ya penisilini, wafungwa waliambukizwa kaswende kwa makusudi na baadaye kutibiwa kwa dawa hiyo. Hillarry Clinton Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani amesema kuwa jaribio hilo lililosababisha maambukizo ya ugonjwa huo wa zinaa kati ya mwaka 1946 hadi 1948 nchini Guatemala ni kinyume cha maadili hata kama tukio hilo lilitokea miaka 64 iliyopita.
Rais Alvaro Colom wa Guatemala amelalamikia vikali jinai hiyo ya Wamarekani akisema ilisababisha maambukizo ya kaswende kwa mamia ya wananchi wa nchi hiyo na kwamba ni jinai dhidi ya binadamu. Kaswende ni ugonjwa wa zinaa unaoweza kusababisha matatizo ya moyo, upofu, matatizo ya akili na hata kifo.

Wednesday, September 29, 2010

Samahanini Wadau

Tafadhalini sana wadau naomba kama mtu ana swali la haraka anitumie kupitia email yangu ambayo ni sthugs4j@yahoo.com . Hii ni kutokana na baadhi ya wadau kuuliza maswali yao yanayohitaji ufafanuzi wa haraka katika comments za makala zilizopita, sasa kuna baadhi ya wakati hata sipati muda wa kucheck comments za makala zilizopita, na hivyo kushidwa kujibu katika wakati unaotakiwa.
Samahani sana....Shally.

Saturday, September 18, 2010

Huraa! Maambukizo mapya ya Ukimwi yapungua Afrika!


Umoja wa Mataifa umetangaza kwamba nchi zilizoko chini ya Jangwa la Sahara barani Afrika zinaongoza kwa kupungua maambukizo mapya ya virusi vya Ukimwi. Kitengo cha Umoja wa Mataifa kinachoshughulia masuala ya Ukimwi (UNAids) kimesema kuwa nchi 22 ambazo ziko katika eneo hilo la chini ya Jangwa la Sahara lenye maambukizo makubwa zaidi ya Ukimwi duniani zimeshuhudia kupungua maambukizo ya ugonjwa huo kwa asilimia 25!. Kupungua maambukizo hayo kumetokana na watu kuelewe vizuri na kuchukua tahadhari juu ya ugonjwa huo pamoja na kutumiwa vyema njia za kujikinga. Hata hivyo Umoja wa Mataifa umesema kwamba maambukizo mapya ya Ukimwi yameongezeka huko mashariki mwa Ulaya, katikati mwa bara Asia, na miongoni mwa wanaume mashoga katika nchi zilizoendelea. Mkurugenzi Mtendaji wa UNAids Michel Sibide amesema kwamba, dunia inapiga hatua kubwa katika kufikia utekelezwaji wa Malengo ya Sita ya Maendeleo ya Milenia (MDG6) ya kupambana na kupunguza maambukizo ya HIV/Aids hadi kufikia mwaka 2015. Shirika hilo aidha limesema kuwa, kuwa watu milioni 5.2 wanapatiwa matibabu ya Ukimwi duniani kote, suala ambalo limesaidia kuhakikisha kwamba watu wachache zaidi wanakufa kutokana na virusi vya ugonjwa huo hatari ikilinganishwa na huko nyuma.
Haya shime jamani tuendeleze kwa nguvu zote mapambano dhidi ya Ukimwi!

Monday, September 13, 2010

Sababu ya kukoroma na jinsi ya kuzuia hali hiyo


Kukoroma ni tatizo linalowapata watu wengi wakati wanapolala ambalo linaweza kuwatokea watu wa kila umri ingawa hutokea mara nyingi kwa wanaume au watu wanene. Kukoroma huzidi kwa kadri umri unavyoongezeka na asilimia 54 ya watu wazima hukoroma baadhi ya wakati huku asilimia 25 ya wengine wakiwa na tabia ya kukoroma kila wakati. Kukoroma baadhi ya wakati kwa kawaida sio tatizo kubwa na mara nyingi huleta tu karaha kwa mtu anayelala karibu na mkoromaji. Hata hivyo kukoroma huko sio tu kwamba huharibu usingizi wa anayekoroma bali pia huwasumbua na kuwakeresha wanaolala karibu na mkoromaji. Wale wenye tabia ya kukoroma, hukoroma kila wanapolala na mara nyingi huchoka wanapoamka, na watu wa aina hii hushauriwa kumuona daktari na kushauriwa kuhusiana na tatizo hilo. Lakini kabla hatujaendela mbele ni bora tujue kukoroma hasa ni nini au hutokea vipi?
Mtu huwa anakoroma pale kunapokuwa na kitu au sababu yoyote itakayoziba kuingia au kutoka kwa hewa mdomoni na katika pua. Kuta za koo hutikisika wakati wa kupumua na matokeo yake ni sauti inayosikika ya kukoroma. Kuingia au kutoka kwa hewa huweza kuzuiwa na sababu mbalimbali kama vile:
• Kuziba tundu za pua kusiko kamili ambako husababisha nguvu zaidi zitumike katika kupitisha hewa kwenye pua wakati mtu akiwa amelala. Kitendo hicho hupelekea nyama laini za pua na koo zijikusanye na kusababisha mkoromo. Kuna baadhi ya watu wanakoroma tu kipindi cha allergy (allergy season) au wanapatwa na matatizo ya sinus. Baadhi ya matatizo kama vile kupinda pua (deviated septum) au ukuta unaotenganisha tundu za pua na polyps za pua pia huweza kufanya pua zizibe na kusababisha kukoroma. Watu wengi wanaofanya operesheni za pua pia hupatwa na tatizo la kukoroma.
• Kuwa na misuli dhaifu katika koo na ulimi. Misuli au nyama za koo na ulimi zinapokuwa dhaifu sana hulegea na kuanguka upande wa nyuma wa sehemu inayopita hewa. Suala hilo hutokea pale mtu anapolala fofofo au kuwa na usingizi mzito na kusababisha kukoroma.
• Kuwa na misuli minene ya koo. Hii ni kwa wale watu wanene ambao hata nyama zao za koo pia hunenepa na kupanuka na suala hilo husababisha kukoroma, Pia watoto wenye tonsesi kubwa na adenoids baadhi ya wakati hukoroma.
• Kuwa na kilimi kikubwa ni mojawapo ya sababu zinazosababisha kukoroma. Kilimi kirefu kinaweza kuzuia koo na pale kinapotikisika wakati hewa inapita kwa msukumo husababisha kukoroma.
• Sababu nyinginezo zinazoweza kumsababishia mtu akorome anapolala ni kuwa na umri mkubwa au uzee, imeshuhudiwa kuwa watu wa makamo na wazee hukoroma, kwani misuli na nyama za koo huanza kuzeeka na kulegea kadri umri unayoongezeka. Vilevile wanaume wanakoroma zaidi kuliko wanawake hii ni kutokana na wanaume kuwa na njia nyembamba zaidi ya hewa kuliko wanawake. Kukoroma pia kunaweza kuwa ni tatizo la kurithi. Pombe, kuvuta sigara na matumizi ya baadhi ya dawa pia husababisha misuli ya koo ilegee na hivyo hupelekea mtu akorome. Kulala vibaya pia husababisha kukoroka kama vile kulala kichalichali, kwani hufanya nyama za koo zilegee na kuziba hewa.



Je, Dawa ya kukoroma ni nini?
Swali hilo limeuliwa sana na mimi katika kulijibu ningependa kusema kuwa, kujua sababu inayosababisha mtu akorome na kuitatua au kuiondoa sababu hiyo ndiko kunakotibu kukoroma. Sote tunajua adha inayotokana na kukoroma, na sauti hiyo inavyosumbua hasa iwapo anayekoroma ni mtu wako wa karibu kama vile mumeo, mwenzi wako au yoyote yule inayekubidi ulale naye karibu au katika kitanda kimojana hata chumba kimoja. Kukoroma pia huathiri usingizi wa mkoromaji kwani anayekoroka humbidi aamke mara kadhaa usingizini akijua au bila kujua kutokana njia zake za hewa kufunga kwa sekunde kadhaa ambapo usingizi pia hukatika. Wanaokoroma pia hushindwa kulala vizuri suala linalopelekea asubuhi wawe wamechoka na kutofanya majukumu yao vyema, na pia wale wanaolala nao karibu hupatwa na matatizo kama hayo. Vilevile tunapaswa kujua kuwa kukoroma kuna athari za kiafya za muda mrefu kwa mtu anayekoroma hivyo si jambo la kufanyia mzaha na ni tatizo ambalo linapaswa kushughulikiwa na kutatuliwa.
Wataalamu wanatuambia kuwa ili kujua kukoroma kwako kunasababishwa na nini ni bora ushirikiane na mwenzi wako au yoyote unayelala naye ili akuchunguze pale unapolala na kujua jinsi mwili wako unavyokuwa pale unapokoroma. Ni bora aandae orodha na kuchunguza yafuatayo:
1. Kufunga mdomo na kukoroma kunaonyesha kuwa kuna matatizo ya ulimi.
2. Kufungua mdomo na kukoroma kunaonyesha unaweza kuwa na tatizo katika misuli au nyama za koo.
3. Kukoroma unapolala kichalichali kunaonyesha kuwa pengine kwa kubadilisha namna unavyolala kukoroma nako kunaweza kwisha.
4. Kukoroma wakati unapolala kwa kila mlalo kunaonyesha kwamba tatizo lako ni kubwa na pengine kunahitajia tiba kubwa zaidi.




Iwapo umebadilisha namna unavyolala na haikusaidia, unashauriwa ujaribu yafuatayo:
 Punguza uzito
 Safisha njia yako ya hewa. Kuwa na pua iliyoziba hufanya kupumua kuwe kugumu na kusababisha kukoroma. Unaweza kufanya hivyo kwa kutumia dawa za kusaidia kupumua kwa urahisi (nasal decongestants) zinazopatikana kwa urahisi katika maduka ya dawa.
 Wacha kuvuta sigara.
 Lala mapema na pata usingizi wa kutosha kila mara huku ukijiepusha na kuchoka sana. Kunyanyua kichwa kwa nchi 4 huweza kupunguza kasi ya kupumua na kusaidia ulimi na taya kwenda mbele hali ambayo hupunguza kukoroma. Fanya hilo kwa tumia mito maalum ya kupunguza kukoroma au lala bila mto.

Wataalamu pia wanasema kwamba unaweza kupunguza kukoroma kwa kutokula baadhi ya vyakula au dawa kabla ya kulala ambavyo huongeza kukoroma. Vitu hivyo ni kama vile
o Kutokula mlo mkubwa kabla ya kulala.
o Kutokula vyakula vinavyotokana na maziwa au maziwa ya soya.
o Kutokunywa pombe kabla ya kulala.
o Kutotumia dawa aina ya antihistamines.
o Kutotumia vyakula au vinjwaji venye kafeini.

Vilevile wanaokoroma wanashauriwa kufanya mazoezi ya koo ambayo ni pamoja na kuimba, kusoma kwa kurudia rudia voweli (a,e,i,o,u) kwa nguvu kwa dakika tatu mara kadhaa kwa siku, kuweka ncha ya ulimi chini ya meno ya mbele na kurudisha ulimi nyuma kwa dakika 3 kila siku au huku mdomo ukiwa wazi pelekea taya yako upande wa kulia na wacha ibakie katika hali hiyo kwa sekunde 30. Huku mdomo ukiwa wazi, kaza misuli ya nyuma ya koo na rudia kitendo hicho kwa sekunde thelathini. Unaweza kutizama kwenye kioo na kuona jinsi kilimi kinavyokwenda juu na chini.
Iwapo kukoroma hakutoisha kwa kutumia njia hizo tofauti zilizoelezwa, usife moyo jaribu kumuona daktari na akupe ushauri wa kitiba kuhusiana na tatizo hilo. Madakatari wataalamu wa magonjwa ya pua, masikio na koo au ENT wanaweza kukusaidia zaidi kutatua tatizo hilo. Siku hizi kuna vifaa mbalimbali vinavyotumiwa mahospitalini ili kuondoa kukoroma kama vile kifaa kinachowekwa kwenye meno, CPAP, kidude kinachowekwa mdomoni au hata kufanyiwa operesheni ili kuondoa tatizo hilo.

Wednesday, September 8, 2010

Mambo ya kuzingatia iwapo unataka kushika mimba


Kuna sababu mbalimbali zinazoweza kumfanya mtu asishike mimba. Sababu hizo zinaweza zikawa zinamhusu mwanamke, mwanamume au wakati mwingine kutojulikana kabisa hali hiyo imesababishwa na nini. Wataalamu wanasema kwamba kwa miaka 20 iliyopita matatizo yanayohusu kushindwa kuzaa yameongezeka kwa kiwango kikubwa na asilimia 25 ya watu wanaotaka kubeba mimba na kuzaa mtoto wanakabiliwa na tatizo hilo. Ni kweli kuwa kwa kawaida watu wengi hubeba mimba na kujaaliwa mtoto pale tu wanapofanya tendo la ndoa. Lakini jambo hilo halitokeo kwa watu wote na ingawa kwa baadhi ya watu kila kitu huonekana kwenda sawa lakini pia hushindindwa kubeba mimba. Utafiti unaonyesha kwamba katika kila familia au 'couples' 5 zinazojamiiana katika wakati muafaka wa ovulation ni moja tu ndio hufanikiwa kupata mtoto, huku karibu wanawake 9 kati ya 10 wakifanikiwa kushika mimba baada ya kujaribu kutafuta mtoto kwa mwaka mmoja mzima bila kuzuia mimba. Hivyo basi nawaomba wale ambao wamekuwa wakifanya jitihada za kufuata maelekezo ili waweze kushika mimba lakini hawakufanikiwa, wasife moyo kwani ipo siku jitihada zao hizo zitazaa matunda.
Mambo ya kuzingatia iwapo unataka kushika mimba…
• Kwanza kabisa ni kuhakikisha kuwa kabla ya yote unamona dokta wako au unakwenda hospitalini na kufanyiwa vipimo ili kujua kama afya yako iko salama au la kwa ajili ya kushika mimba. Baadhi ya vipimo vinavyoshauriwa kufanywa ni pamoja na
1. General examination au uchunguzi wa jumla.
2. Kipimo cha kensa au Pap smear.
3. Kipimo cha magonjwa ya zinaa (STD) kama vile Chlamydia ambao wanaweza kuathiri uwezo wako wa kushika mimba.
4. Kipimo cha damu cha kuangalia kama una upungufu wa damu, Rh na kinga yako ya mwili dhidi ya ugonjwa wa Rubella.
5. Kipimo cha mkojo cha kuchunguza iwapo una ugonjwa wa kisukari. Ugonjwa wa kisukari huweza kumzuia mtu asishike mimba hata iwapo mzunguko wake wa mwezi uko sawa, anapata Ovulation na kidhahiri anaonekana hana tatizo lolote.
6. Kama una paka nyumbani au unakula sana nyuma (red meat) pengine si vibaya pia kupima kipimo cha Toxopmasmosis infection.
7. Kuyajua na kuzingatia baadhi ya mambo yanayoathiri kushika mimba ambayo ni pamoja na:-
• Ingawa unene unaweza kumzuia mtu asishike mimba lakini kufanya mazoezi sana na kuwa na uzito mdogo sana wa zaidi ya kilo 50 huweza pia kumsababisha mtu asishike mimba. Mazoezi ya kupindukia pia huathiri homoni mwiilini.
• Kuwa na fikra nyingi na msongo wa mawazo 'stress' huweza pia kauthairi uwezo wa mtu wa kushika mimba.
• Kutokula vizuri na kutopenda kula kwani humkosesha mwanamke au hata mwanamme baadhi ya virutubisho muhimu vinavyotakiwa kwa ajili ya kufanikisha suala la kushika mimba (nitazungumzia vyakula vinavyosaidia kushika mimba baadaye)
• Sigara, marijuana na pombe ni miongoni mwa vitu ambavyo vinaweza kuathiri uwezo wa kubeba mimba. Mwanamke anayetaka kubeba mimba anashauriwa aache kunywa pombe na kuvuta sigara. Mwanamume pia anashauriwa kuacha kuvuta sigara kwani sigara huathiri kiwango cha mbegu za kiume za mwanamme.
Yafuatayo ni baadhi ya mambo yanayomsaidia mwanamke kushika mimba:
• Anza kutumia vidonge vya Folic Acid, vidonge hivyo mbali ya faida nyinginezo humkinga mtoto atakayezaliwa na magonjwa ya ubongo. (Neural Tube Defect) kama vile Spinal Bifida na mengineyo. Dozi ni kwa uchache miligramu 0.4 za Folic acid kwa siku, miezi mitatu kabla ya kuanza hata kutafuta mtoto.
• Endelea tu na tendo la ndoa bila kuchoka au kukata tamaa, lakini ni bora nguvu zihifadhiwe kwa siku chache kabla ya Ovulation na siku kadhaa baada ya hapo ili mwanamume aweze kuboreshe na kuhifadhi mbegu zake kwa ajili ya siku hizo, Usikimbie chooni au bafuni baada tu ya kukutana kimwili na mwenzio. Kulala kwa dakika kadhaa baada ya tendo la ndoa huongeza uwezo wa mbegu ya kiume kuweza kuendelea kukutana na yai la kike na hivyo kuongeza uwezekano wa kubeba mimba.
• Jiepushe kunywa kahawa na binywaji vinginevyo venye caffeine. Waataalamu wanasema caffeine huweza kukuongezea matatizo ya kushindwa kushika mimba.
• Jiepushe na kutumia dawa za aina yoyote bila ushauri wa daktari. Dawa zinazonunulika maduka ya dawa bila ulazima wa cheti cha daktari au Over-the-counter drugs inabidi zitumiwe baada ya kushauriana na daktari.
• Usitumie baadhi ya vitu vinavyoufanya uke uwe na hali itakayoua mbegu za kiume au kupunguza majimaji yake. Vitu hivi ni kama spray mbalimbali na tampons zinazotumiwa na wanawake ili kuufanya uke uwe na harufu nzuri. Mafuta ya aina mbalimbali na jeli kwa ajili ya kulainisha sehemu za siri, mafuta ya kula (vegetable oils) glycerin na mate. Vitu kama hivi kufanya Ph ya uke isiwe ya kawaida na huweza kuua mbegu ya kiume, kusababisha baadhi ya magonjwa ya wanawake au kupunguza majimaji ya ukeni ambayo yanatakiwa ili kusafirisha mbegu za kiume.
• Hakisha mwenzi wako hafanyi kazi au hawi katika mazingira yenye mada hatari ambazo hupunguza uwezo wa mbegu za kiume au kutungwa mimba. Kufanya kazi kwenye mazingira ya joto kali sana kama vile mwanaume wanaofanya kazi kwenye matanuri ya kupika mikate, viwanda vya mafuta na miale hatari baadhi ya wakati huwa na matatizo ya kutozaa. Hivyo kabla mwanamke hajaanza kujilaumu kwa nini hashiki mimba, mwanamme wake pia anapaswa kufanyiwa uchunguzi kamili kuhusiana na suala hilo. Pengine ni suala ambalo wengi hatulijui kwamba katika tiba iwapo mke na mume au mtu na mwenzi wake wana tatizo la kutopata mtoto, wawili hao kwa pamoja hupaswa hufanyiwa vipimo na wala sio mwanamke mwenyewe. Hivyo iwapo unashindwa kushika mimba, hakikisha pia mwenzi wako hana tatizo pia. Wanaume pia kama walivyo wanawake hukabiliwa na matatizo mengi tu yanayosababisha familia kukosa watoto. Matatizo kama vile upungufu wa mbegu za kiume, uchache wa mbegu, kutokuwa na kasi mbegu na mengineyo ni miongoni mwa matatizo kibao ambayo mwanamume anaweza kuwa nayo na kukosa mtoto. Hivyo tabia ya kuwatizama wanawake kwa jicho la lawama katika jamii na kuwanyooshe kidole pale mimba inaposhindikana kushika ni kinyume cha ukweli wa kitiba na uhalisia.
• Usichoke kufuata mzunguko wako wa Ovulation na kufanya tendo la ndoa katika wakati ambao mwili wako (ewe mwamamke) uko katika siku za kuweza kushika mimba.

Monday, September 6, 2010

Wataalamu karibu watakugundua dawa nyingine ya kutibu Malaria


Matokeo ya utafiti wa kimataifa yanaonyesha kwamba wanasayansi karibu watafanikiwa kutengenza dawa yenye athari zaidi ya kutibu ugonjwa wenye kuleta maafa mengi wa Malaria. Dawa hiyo inayoitwa "NITD609" ambavyo inatokana na mada ya 'spinoindolones' imeanza kutengenezwa kwa jitihada mbalimbali za wanasayansi wa Marekani, Singapore, Switzerland, Thailand na Uingereza. Wanasayansi hao wanasema kwamba, dawa hiyo ambayo ni ya kumeza inatofautiana na dawa nyinginezo za Malaria zilizopo madukani kwa kuponya ugonjwa huo haraka, kutokuwa na madhara kwa mtumiaji na kuweza kutibu Malaria kwa kutumiwa dozi moja tu.
Utafiti bado unaendelea kuhusiana na majaribio ya dawa hiyo na kwamba dawa hiyo imeonyesha mafanikio mazuri katika kutibu Malaria baada ya kujaribiwa kwa panya watano waliokuwa wagonjwa bila kuwa na madhara yoyote.
Wataalamu wanasema pia kwamba dawa hiyo ya NITD609 inatofautiana sana na dawa ziliopo za Malaria kwa umbo na kwa kikemia na kwamba ingawa dawa zilizopo zinaweza kutibu ugonjwa huo lakini zimeshindwa kufikia matarajio yanayotakiwa. Wataalamu sasa wanasubiri kuijaribu dawa hiyo kwa binadamu, suala ambalo litaanza baadaye mwakani.
Ingawa sote tunajua lakini si vibaya kukumbusha hapa kuwa watu karibu milioni 500 huugua ugonjwa wa Malaria kila mwaka duniani, ambapo vifo vinavyosababishwa na ugonjwa huo ni karibu milioni moja huku watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano ndio wanaoshambuliwa zaidi na Malaria. Ugonjwa huo umekuwa ukisababisha vifo na matatizo mengi katika nchi zilizo chini ya Jangwa la Sahara barani Afrika kuliko maeneo mengineyo duniani.

Sunday, August 15, 2010

Swaumu na Siha


Kwanza nawatakiwa wadau Waislamu wa Kona ya Afya swaumu njema na kw amanasaba wa mwezi mtukufu wa Ramadhani nimeandika makala hii kuhusiana na umuhimu wa kufunga. natumaini mtafaidika nayo.
Kufunga kumeamriswa katika dini mbalimbali ikiwepo dini tukufu ya Uislamu, Uyahudi na Ukiristo. Mbali na dini mbalimbali kuamuru wafuasi wao wafunge kama moja ya ibada muhimu, wataalamu wengi wa masuala ya tiba wamekuwa wakiamini kuwa kufunga ni miongoni mwa tiba asilia na inaleta faida kubwa kiafya. Kufunga kuna faida tele kwa afya na kwa siha ya mwili. Uislamu unawataka wafuasi wake wawe wenye afya njema, wasafi, walio imara kiimani na kimwili na mwenye nguvu. Bwana Mtume Mtukufu Muhammad (S.A.W) ametilia nguvu hoja hiyo pale aliposema kwamba: "Fungeni mpate siha".
Hii leo pia wataalamu wa masuala ya afya wamethibitisha faida kemkem mtu anazoweza kuzipata mtu kwa kufunga, zinazouinufaisha mwili na akili. Kuna baadhi ya madaktari wanasema kuwa kufunga kunamfaidisha mtu kisaikolojia na kimwili. Mbali na swaumu kumfanya anayefunga awe na stamina ya njaa na aweze kuvumulia matatizo na awe na subra, pia husaidia kupunguza mafuta ya zaida mwilini. Faida za kufunga haziishiii hapo bali pia swaumu ni njia ya kuponya magonjwa mbalimbali yakiwemo yale yanayohusiana na mfumo wa chakula kama vile maumivu ya tumbo sugu, kuvimba utumbo mkubwa, ugonjwa wa ini, kukosa choo na matatizo mengineyo kama vile unene wa kupindulia, kuziba mishipa ya moyo (arteriosclerosis), shinikizo la damu, asthma, diphtheria na kadhalika.
Lakini kabla hajujaendelea na mada yetu hii hebu sasa tueelezee kwa undani kitaalamu jinsi kitendo cha kufunga kinavyoufaidisha mwili.
Kufunga kitaalamu huanza pale mwili unapokosa chakula kwa masaa 12 hadi 24. Kikemia kufunga hakuanzi hadi pale sukari aina ya carbohydrate iliyohifadhiwa mwilini inapoanza kutumiwa kama chanzo cha kuzalisha nguvu. Kufunga huko huendelea madam tu mafuta na carbohydrate iliyohifadhiwa iendelee kunyofolewa na badilishwa kuwa nguvu, bila kutumiwa protini iliyohifadhiwa. Pale protini inapoanza kutumiwa na kubadilishwa kuwa nguvu (suala ambalo hupelekea misuli kupungua) kitaalamu tunasema kuwa mtu ameanza kukabiliwa na ukosefu mkubwa wa chakula mwilini au kwa kimbombo starving.
Faida za kufunga zinaweza kufahamika kwa kujua jinsi mwili unavyofanya kazi wakati chakula kinapokosekana.
 Wakati mwili unapoishiwa na nguvu inayotokana na chakula, huanza kutegemea hazina yake ya chakula kilichohifadhi na kitendo hicho huitwa Autolysis. Autolysis ni kuvunja vunja mafuta yaliyohifadhiwa mwilini ili kutengeneza nguvu, kitendo ambacho hufanywa na ini. Hali hiyo hupunguza mafuta ya ziada mwilini ambayo ndio sababu kuu ya magonjwa mengi kama vile shinikizo la damu, mshituko wa moyo na kadhalika.
 Kufunga pia husaidi kuondoa sumu mwilini. Suala hilo hurahisishwa na kufunga kwani chakula kisipoingia mwilini, mwili hubadilisha mafuta yaliyohifadhiwa kuwa nishati na kupitia kitendo hicho kemikali nyinginezo na sumu zenye madhara kwa mwili pia hutoka katika utumbo, ini, figo, mapafu na ngozi. Hizi ni sumu ambazo hutokana na vyakula tunavyokula na mazingira yetu, na huingia mwilini na kuhifadhiwa pamoja na mafuta.
 Faida nyingine ya swaumu kitiba ni kuupumzisha mfumo wa chakula. Wakati mtu anapokuwa hali, nguvu inayotumiwa na mfumo wa chakula ambao huwa umepumzika huelekezwa kwenye metabolism na mfumo wa kulinda mwili. Kitendo hicho husaidia mfumo wa kulinda mwili uweze kufanya kazi zake vyema zaidi na kupambana na mgonjwa au vile visivyotakiwa mwilini. Pengine hii ndio babu wanyama wanapopata jeraha huacha kula, na wanadamu hupoteza hamu ya kula wanapopatwa na magonjwa kama vile mafua. Kwa sababu mwili huielekeza nguvu yake yote kwenye mfumo wa ulinzi wa mwili ili kupambana na vijidudu. Faida hiyo mtu huipata pia anapofunga.
 Wakati wa kufunga vilevile joto la mwili hupungua kwa kiasi kikubwa. Hii hutokana na kupungua kasi ya metabolism na kusimama kazi nyingi zinazofanywa na mwili. Kwa kupungua kiwango cha sukari au glukosi katika damu, mwili hutumia glukosi inayohifadhiwa kwenye ini. BMR (basal metabolis rate) hupungua ili kuhifadhi nishati mwilini. Pia homoni mbalimbali huzalishwa wakati mtu anapokuwa amefunga zikiwemo homoni za kukua na za kuzuia seli zisizeeke. Hivyo njia mojawapo ya kuzuia uzee na kuwa na maisha marefu ni kufunga.
Kwa kuzingatia maelezo hayo yote tunaweza kusema kuwa, swaumu ina faida kubwa kiafya kwa mwanadamu.

Thursday, August 12, 2010

Ni vipi ubebe mimba ya mtoto wa kike?



Napenda kuchukua nafasi hii kujibu swali la pili la mdau mmojawapo wa Kona ya Afya ambaye ameuliza kuwa, ni vipi anaweza kubeba mimba ya mtoto wa kike. Katika kujibu swali hilo naweza kusema kwamba, ndugu mdau ulimwengu hivi sasa umeendelea sana kiasi kwamba matatizo mengi katika jamii yanatatuliwa kwa msaada wa wataalamu mbalimbali. Mojawapo ni suala la mtu kuzaa mtoto wa kike au wa kiume. Ingawa njia hizo nitakazoziandika hapa pengine hazina uhakika mia kwa mia, lakini wapo watu wengi wamejaribu na zimewasaidia. Hivyo nina matumaini kwa kufuata maelekezo haya ukaweza kupanga na kuzaa mtoto wa kike kama unavyokusudia. Ninachotaka kusisitiza hapa ni kuwa, maendeleo ya elimu hasa katika uwanja wa sayansi na tiba yamekuwa na taathira nyingi katika kupunguza matatizo ya familia kama vile ugumba, kuzaa mtoto wa jinsia inayotakiwa na wazazi, magonjwa ya wanawake, vifo vya wajawazito na kadhalika. Ni ukweli usiopingika kwamba ingawa watu wengi wanazingatia kuzaa mtoto aliye mzima wa mwili na afya bila kujali jinsia ya mtoto huyo, lakini uchunguzi unaonyesha kwamba kuna baadhi ya watu au wazazi wanaopenda kuwa na watoto wa jinsia fulani zaidi. Vilevile imeonekana kuwa wanawake hupendelea kuwa na watoto wa kike huku wanaume wakipenda kuwa na watoto wa kiume. Hata hivyo wazazi ambao tayari wana watoto wa jinsia ya kike au ya kiume hupendelea kuwa na mtoto wa njinsia nyingineyo ili kuwa na watoto wa kiume na wa kike.

Je, ni vipi jinsia ya mtoto huainishwa?
Kinyume na wengi wanavyofikiria kwamba mwanamke au mwili wa mwanamke ndio mwenye jukumu la kuainisha jinsia ya mtoto kwa kuwa yeye ndiye anayebeba mimba, uhakika wa mambo ni kuwa mwanamume ndie mwenye uwezo wa kuainisha jinsia. Kila yai la mwanamke lina chromozu mbili za X. Iwapo manii ya mwanamume au spemu (ambayo in chromozomu X na Y) itakuwa na X na kurutubisha yai la mwanamke lenye X tupu, basi mtoto atakayezaliwa atakuwa mwanamke. Vilevile iwapo spemu ya mwanamume itakuwa na Y na kurutubisha yai la mwanamke, basi mtoto atakayezaliwa atakuwa mwanamume. Hivyo kwa kufahamu suala hilo, ni matumaini yetu kuwa vile visa vya kinamama kuachwa eti kwa kuwa hawakuzaa watoto wa kiume au wa kike vitapungua katika jamii zetu. Mke wako asipozaa mtoto wa jinsia uitakayo, usifikiri kuwa yeye ndio mwenye makosa.
Wakati mwanamume anapomwaga shahawa, spemu kati ya milioni 200 hadi 400 humwagwa katika uke wa mwanamke. Baadhi ya spemu hizo huwa zina chromozomu X na baadhi zina chromozomu Y. Hata hivyo, ni spemu moja tu ambayo hutakiwa kwa ajili ya kurutubisha yai la mwanamke na kuunda mimba. Nadharia mbalimbali zinazotolewa kwa ajili ya kusaidia kuchagua ni jinsia gani unaitaka awe nayo mwanao, zinategemea suala la kuandaa mazingira katika uke na mwili wa mwanamume na mwanamke, yatakayosaidia spemu ya baba yenye chromozomu inayotakiwa irutubishe yai la mama, na hivyo kutungwa mimba ya jinsia inayotakiwa.
Njia ya Dr. Shettles ya kuzaa mtoto wa kike
Njia hii imekuwa ikitumiwa na watu wengi kwa miaka mingi sana na imewasaidia kuweza kuzaa mtoto wa kike. Wengi wanasema kuwa uwezekano wa kufanikiwa njia hii ni asilimia 90. Njia ya Dr. Shettles inategemea msingi kwamba, chromozomu Y (yenye kuwezesha kutungwa mimba ya mtoto wa kiume) ni ndogo na yenye kwenda kwa kasi zaidi ikilinganishwa na chromozomu X (yenye kuwezesha kutungwa mimba ya mtoto wa kike) ambayo ni kubwa na huenda polepole. Pia kwa kutegemea kuwa chromozomu X inaishi muda mrefu zaidi kuliko ile ya Y. Hivyo Dr. Shettles anashauri kuwa iwapo unataka kuzaa mtoto wa kike uhakikishe kuwa:
• Unajamiiana siku 2 au 3 kabla ya Ovulation. Kinadharia spemu za kiume zitakuwa zimeshakufa hadi kufikia siku hasa ya Ovulation na kuziacha spemu za kike zikiwa hai tayari kurutubisha yai na kuunda mtoto wa kike.
• Anashauri pia wanawake wajizuie kufikia kileleni (orgasm) kwani hali hiyo itaufanya uke uwe na hali ya asidi ambayo ni kwa faida ya spemu ya kike yenye chromozomu X.
• Pia anawashauri wazazi wanapojamiina wawe katika hali ya mwanamke kulala chini na mwanamume juu au missionary position. Kwani anasema kuwa mtindo huo huziwezesha spemu zenye chromozamu X zimwagike karibu na mlango wa uke na kuwa na uwezekano mkubwa wa kuingia ukeni na kutungwa mimba.
Njia ya O+12
Njia hii inayomaanisha Ovulation jumlisha siku 12 ilivumbuliwa na mama mmoja wa Australia aliyekuwa akihangaika kupata mtoto wa kike baada ya kuzaa watoto 6 wa kiume. Mama huyo anawahusia wale wanaotaka kubeba mimba ya mtoto wa kike wajamiiane masaa 12 baada ya Ovulation. Mama huyo alifuata njia ya Dr. Shettles bila mafanikio katika mimba zake za nyuma. Lakini baada ya kugundua njia yake hii mwenyewe mwishowe alibeba mimba na kujifungua mtoto wa kike.



Kuna wengine wanaamini kwamba baadhi ya lishe na vyakula vya aina mbalimbali husaidia kutunga mimba ya mtoto wa kike. Kwa mfano kuna wanaoamini kuwa kula baadhi ya vyakula huufanya uke uwe na hali ya asidi ambayo husaidia Chromozomu Y ife katika uke. Nadharia nyingineyo inayotumiwa katika kuchagua jinsia ya mtoto inasema kwamba, mwanamke anayetaka kubeba mimba ya mtoto wa kike ale vidonge vya virutubisho (supplements) vya Calcium na Magnessium mwezi mmoja kabla ya kubebea mimba. Iwapo unataka kutumia vidonge vya virutubisho ili uweze beba mimba ya mtoto wa kike, ni bora ushauriane na daktari wako kwanza. Hii ni kwa sababu dawa hizo huweza kuingiliana na dawa nyinginezo za magonjwa mbalimbali.
Baadhi ya vyakula vinavyotajwa kuwa vinasaidia katika kutunga mimba ya mtoto wa kike ni.
• Mahindi, nyama, maharagwe, samaki, tunda damu, mayai na maini.

Vyakula hivyo ni vya asidi hivyo huifanya PH ya mwili wako hupungua na kuwa ya acidi. Hali hiyo husaidia kuua spemu za Y na hivyo kusaidia kuzifanya spemu za X ziwe na uwezekano mkubwa wa kurutubisha yai. Hivyo mwanamke anayependelea kubebea mimba ya mtoto wa kike anashauriwa kutokula vyakula vyenye alikali ambavyo ni kama, ndizi, chokleti, juisi ya machungwa, viazi, tikiti maji na vinginevyo.
Pia sio mbaya kutaja baadhi ya imani na itikadi wanazoamini baadhi ya watu kuwa zinasaidia katika kupata mtoto wa kike:
• Fanya mapenzi wakati wa mchana.
• Fanya mapenzi siku shufwa (even days) za mwezi.
• Fanya mapenzi wakati mwezi umekamilika ( full moon days).
• Kula samaki na mboga mboga kwa wingi, na baadaye kufuatiwa na kitinda mlo cha chokleti.
• M-surprise mwenzi wako, kuna wahenga wanaamini wanawake wanaoanzisha wao kufanya mapenzi huzaa watoto wa kike!]
Hivyo kila la kheri wadau, unaweza kuchagua moja ya njia kati ya zilizotajwa hapo juu na kwa kufuata maelekezo ukajaaliwa kuzaa mtoto wa kike.

Wednesday, August 11, 2010

Ni alama gani za mwili wako zitakufahamisha Ovulation imewadia?



Wadau wa Kona ya Afya, niliahidi kuendeleza mada yetu ya namna ya kuzijua siku za kushika mimba kwa kuzungumzia baadhi ya alama za mwili zinazosaidia kutambua ni wakati gani Ovulation imewadia. Alama hizo za Ovulation si ngumu kuzitambua, iwapo utafahamu unatafuta alama gani. Kuna baadhi ya alama za mwili zinazokutahadharisha kwamba Ovulation iko njiani, hivyo kuweza kukusaidia kupanga vyema muda wa kujamiiana kwa ajili ya kupata mamba. Alama nyinginezo zinakufahamisha kwamba Ovulation imewadia au imeshapita. Ingawa alama hizo ziko nyingi na nitazungumzia baadhi ya hizo, lakini usifikiri kwamba unatakiwa utumie zote, kwani kufanya hivyo kunaweza kukuchanganya.
Iwapo hutoona alama zozote za Ovulation au iwapo siku zako za mwezi hazina mpangilio maalum, ni bora umuone daktari ambaye atakusaidia zaidi.
Mabadiliko ya joto lako la Mwili
Tunaweza kusema kuwa Joto lako la mwili au (Body Basal Temperature) ndio alama maarufu inayotumiwa na wanawake wengi ili kufahamisha kwamba Ovulation imewadia pale wanapotaka kubeba mimba. Hii ni kwa sababu joto lako la mwili huongezeka kwa kiasi kidogo na huendelea kuongezeka baada ya Ovulation. Ongezeko hilo la joto husababishwa na homoni ya progesterone, ambayo huongezeka sana punde baada ya Ovulation. Kwa kujipima joto lako la mwili na kuandika chati ya mabadiliko hayo unaweza kufahamu ongezeko hilo la joto lako la mwili. Unahitajia kipimamoto kwa ajili ya kufanikisha suala hilo. Zipo pimajoto maalum kwa ajili hiyo lakini unaweza kutumia pimajoto ya kawaida pia. Hakikisha unapima joto la mwili wako asubuhi baada ya kuamka na uhakikishe huna homa, hukukosa usingizi, hukunywa pombe, si mgonjwa wala huna wasiwasi na fikra nyingi. Ni bora ufanye hivyo kwa mizunguko kadhaa ya siku zako ili uweze kuijua vyema chati ya mabadiliko ya joto la mwili kwa mujibu wa mzunguko wako wa mwezi.



Ingawa njia hii haianishi moja kwa moja kuwa Ovulation imewadia, lakini joto la mwili huongezeka kidogo kabla yakipindi hicho na huongezeka kwa kwa degree 0.4 hadi 0.6 baada tu ya kumalizika Ovulation. Kuongezeka joto kwa kiasi kikubwa baada ya Ovulation huendelea hadi siku utakayopata siku zako ambapo hupungua na mzunguko wako wa mwezi huanza tena. Iwapo utakuwa umepata mimba joto lako la mwili litaendelea hivyo hivyo kuwa juu. Kwa kuwa mabadiliko ya joto hutokea wakati wa Ovulation iwapo unajaribu kubeba mimba, kufuatilia mabadiliko hayo kwa muda usiopungua miezi miwili ni jambo la dharura ili uweze kujua wakati wa Ovulation ambapo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba.
Mabadiliko ya majimaji ya ukeni
Wakati Ovulation inakaribia majimaji ya ukeni hubadilika pia kwa kiasi na hali. Ikiwa hakuna Ovulation majimaji ya ukeni huwa yanayonata au kama kremu au hukosekana kabisa. Wakati Ovulation inakaribia majimaji ya ukeni huongezeka na huwa katika hali ya majimaji na wakati mwingine huwa rangi nyeupe kama ya yai bichi. Iwapo utapima kwa vidole vyako huvutika kwa inchi au zaidi kati ya vidole vyako.
Ni bora nikumbushe hapa kwamba, kuan wakati unaweza kuwa na majimaji ya ukeni yanayofanana na ya wakati wa Ovulation hali ya kuwa huko katika Ovulation. Hali hiyo ni ya kawaida kwa watu wenye PCOS. Kutumia dawa za Clomid au Antihistamin huweza kufanya majimaji ya ukeni yakauke na hivyo kuwa vigumu kutumia njia hii ili kujua ni zipi siku zennye uwezekano mkubwa wa mimba. Njia hii huhesabiwa kuwa yenye itibari zaidi.
Ongezeko la Matamanio
Inaonekana kuwa maumbile nayo hutusaidia kujua ni siku gani tunaweza kubeba mimba! Wataalamu wameonyesha (jambo ambalo pengine wengi wameshalihisi) kwamba wanawake wanapokuwa katika siku zenye uwezekano mkubwa wa kupata mimba, matamanio yao ya huongezeka. Hizo ni siku chache kabla ya kujiri Ovulation, ambapo ndio wakati unaofaa wa kujamiiana iwapo unataka kubeba mimba.
Hata hivyo njia hii si ya kutumainiwa sana kwani baadhi ya hali kama vile msongamano wa mawazo, fikra nyingi na wasiwasi huweza kupunguzaa matamanio. Au mtu anaweza akahisi matamanio katika muda wote wa mzunguko wa mwezi.
Mabadiliko ya Ukeni:
Kama ambavyo majimaji ya ukeni yanavyobadilika wakati wa Ovulation, uke nao (cervix) hubadilika wakati wa kukaribia Ovulation. Wakati huo uke husogea mbele, huwa laini na hufunguka zaidi.
Maumivu kidogo katika Matiti:
Baadhi ya wanawake wakati wanapokaribia Ovulation au baada ya hapo matiti yao huwa na maumivu kidogo. Suala hili huhusiana na mabadiliko ya homini mwili ambazo hujitayarisha kwa ajili ya mimba. Hata hivyo njia hii sio yenye kutegemewa sana kwani maumivu ya matiti huweza kusababishwa na masuala mengine. Pia maumivu ya matiti hutokea kabla ya hedhi au baada ya kutumia baadhi ya dawa za kusaidia uzazi.




Alama nyinginezo
Baadhi ya wanawake huhisi maumivu kidogo ya tumbo ambayo baadhi huyaita Middle Pain. Maumivu hayo kwa kawaida hutokea upande ule yai linapotoka yaani upande wa Ovulation. Maumivu hayo hutokana na mwendo wa yai wakati linapopenya kwenye mirija. Maumivu hayo si ya kuendelea na wala si makubwa na huisha haraka. Hali hiyo huweza kutokea mara kadhaa katika siku za Ovulation. Kuna baadhi ya alama kama vile baadhi ya wanawake huhisi kichefuchefu, gesi, kukojoa mara kwa mara na maumivu wakati wa kujamiina, hali ambayo haitokei kwa watu wengi. Pia kuna baadhi ya vifaa vinavyopaatikana katika madula ya dawa katika baadhi ya nchi ambavyo huweza kukusaidia kujua wakati wako wa Ovuation umewajia, vifaa hivyo hujulikana kama 'Ovulation Kit"
La muhimu ni kufahamu kuwa wanawake hutofautiana katika kupata alama hizi, kwani kuna baadhi wanaweza wakapata baadhi ya alama hizi na wengineo wakapata nyinginezo. Kuuelewa vyema mwili wako ni jambo zuri linaloweza kukusaidia kuzijua siku zako la Ovulation na hivyo kuweza kujua siku zako za kubeba mimba.

Saturday, August 7, 2010

Je, Poda zina madhara kwa watoto?


Baada ya kuwa kimya kwa muda mrefu, Kona ya Afya imeamua kuanza tena kutoa makala kwa ari mpya, ambapo kwanza tunaanzia kwa kuwajibu maswali wadau ambayo yaliulizwa huko nyuma. Hivyo napenda kuwaeleza wale waliouliza maswali yao kuwa, wasifikiri nimeyatupa kapuni bali nitayajibu moja baada ya jingine Mungu akijaalia.
Tukirudi katika swali la mdau aliyeuliza je Poda zina madhara kwa watoto, kwanza tujue poda ni nini?
Poda ya watoto ni unga unga unaotumika ili kuzuia vipele vya nepi kwa watoto na wakati mwingine hutumika kwa ajili ya kuondosha harufu kama deodorant na kwa matumizi mengine ya vipodozi. Poda inaweza kuwa imechanganywa na 'talc' ambapo poda ya aina hiyo huita talcum powder, na wakati mwingine huchanganywa na unga wa wanga. Poda ya Talcum ni hatari iwapo itamezwa na mtoto kwa sababu inaweza kusababisha pneumonia au ugonjwa wa granuloma. Hakuna maelekezo ya moja kwa moja ya madaktari au taasisi zinazohusika kwa mfano WHO kuhusiana na madhara ya poda kwa watoto au kupiga marufuku matumizi ya poda kwa watoto. Lakini kuhusiana na aina ya poda za Talcum baadhi wanasema kwamba, talc ni mada inayoweza kusababisha kensa na magonjwa mbalimbalia kama vile cysts. Pia wanasema kwamba poda aina ya talc ni hatari kwa mtoto iwapo ataimeza au itamwingia mtoto mdomoni. Lakini pia wako wengine wanaosema kuwa hata poda ya wanga nayo ikitumiwa kwa ajili ya kupunguza vipele vya nepi huweza kuzidisha maambukizo ya 'yeast' au fungus. Vilevile kuna wengine wanaosema kwamba kwa kuwa mwili wa mtoto bado ni mchanga na dhaifu, kujiepusha kutumia katika ngozi ya mtoto vitu vinginevyo kama poda au hata mafuta huweza kusababisha mtoto apate allergy hasa iwapo vifaa kama hivyo vitakuwa vimepitwa na wakati au havikuhifadhiwa katika hali nzuri. Lakini la muhimu kabisa ambalo madakatari, wauguzi na wakunga huwahusia wazazi hasa baada ya kuzaliwa mtoto ni kujihadhari iwapo wanatumia poda wahakikishe kuwa poda haingii kwenye kitovu cha mtoto kabla hakijaanguka.
Hivyo ndugu mdau uliyeuliza swali hili, sina jibu la moja kwa moja kwamba poda ina madhara au la, ispokuwa nakuachia mwenyewe baada ya kusoma makala hii uamue utumie poda kwa ajili ya mtoto wako au usitumie.
• Lakini iwapo utataka kutumia poda basi naweza kukushauri tu ni bora unaponunua poda basi na uangalie vyema kabla ya kununua na kuhakikisha kwamba si ya talcum. Na kama utatumia ya wanga basi iwapo mtoto atapata fungus kwa wakati huo usiendelee kutumia poda hadi atakapopona. Kwani kuendelea kutumia poda kunafanya fungus zizidi.
• Pia hakikisga poda haiingia katika kitovu cha mtoto hasa wakati kibichi na kabla yakijaanguka.
• Hakikisha mtoto hamezi poda au poda haimuuingia mdomoni, puani au masikioni.
• Hakikisha unanua aina za poda zinazojulikana vyema kutoka katika mashirika yenye itibari.
• Hakikisha hata kama unanua poda yenye jina linalojulikana lakini usinunue sehemu mbazo poda humwaga chini au huhifadhiwa katika sehemu zisizofaa ambapo huweza kusababisha hali ya awali ya poda ibadilike.
• Zingatia muda wa kuisha matumizi ya poda unayoitumia, expire date.

Thursday, August 5, 2010

Zijue siku zako za kushika Mimba



Nimeamua kuandika makala hii ili kujibu swali la moja wa mdau wa blogi hii ambaye ameuliza kwamba, anahitaji kushika mimba na je, kwa mfano mwezi huu alianza period yake tarehe 17 Juni, ni zipi siku zake za kushika mimba? Ndugu mdau kwanza kabisa nachukua nafasi hii kukuomba samahani kwa kuchelewa kujibu swali lako. Pengine ninapoandika makala hii utakuwa tayari umeshashika mimba, basi kama ni hivyo hakuna tabu bali natumaini swali lako litakuwa limewasaidia wengine ambao pengine wana tatizo kama halo. Pia umeualiza je, ukitaka mtoto wa kike ufanyeje?
Nachukua nafasi hii kwanza kujibu swali lako la kwanza kabla sijaenda kwenye swali lako la pili. Kwani kuelewa vyema swali la kwanza kutasaidia kuelewa swali la pili pia.
Inafaa tufahamu kuwa ili kuweza kujua ni siku zipi za mwezi mwanamke anaweza kushika mimba (to conceive) inabidi tujua kwanza kipindi ambacho mwili wa mwanamke uko tayari kushika mimba au Ovulation Period. Ovulation ni wakati ambao yai lililokua hutoka katika mirija ya ovari katika kizazi cha mwanamke na katika wakati huu uwezo wako wa kushika mimba ni mkubwa. Kwa kawaida mwanadamu huwa na mayai kadhaa katika ovari zake kwa wakati maalum wa mwenzi, ambapo yai kubwa kuliko yote huondoka na kueleka katika tumbo la uzazi kupitia mirija ya ovari. Ovulation haifuati mpangilio maalum kati ya ovari katika kila mwezi na haijulikani ni ovari gani itatoa yai kila mwezi. Wakati yai linapotoka huwa na uwezo wa kurutubishwa au kukutana na mbegu ya kiume na kuanza kutengeneza mtoto kwa muda wa masaa 12 hadi 24, kabla halijapoteza uwezo wake. Iwapo yai litafanikiwa kurutubishwa na mbegu ya kiume kwa wakati maalum na kujikita katika fuko la uzazi basi matokeo yake ni mimba. Na iwapo halitorutubisha yai hilo pamoja na kuta za kizazi huharibika na kutoka nje ya mwili kama damu ya hedhi.
Nimetangulia kueleza haya kama utangulizi kabla ya kuzieleza siku za kushika mimba kwani kuelewa suala hilo kutatusaida kujua umuhimu wa kujua idadi ya siku zetu za mzunguko wa mwezi (Menstrual Cycle) na umuhimu wake katika kushika mimba na hata katika magonjwa ya wanawake. Ili kuelewa vyema siku hizo inatubidi tujue kitu kinachoitwa Kalenda ya Ovulation au kalenda ya kubeba mimba na pia tujua mzunguko wetu wa hedhi una siku ngapi. Mzunguko wa mwezi ni siku ya kwanza unayopata damu yako ya hedhi hadi siku kabla ya kupata tena hedhi nyingine.



Wataalamu wanatuambia kuwa ili kujua mzunguko huo vyema inatubidi tuchunguze hedhi yetu kwa miezi isiyopungua 6. Lakini kama una haraka na huwezi kuchunguza kwa miezi 6 chunguza kwa miezi mitatu. Unaweza kufanya hivyo kwa kutumia kalenda ya kawaida na kwa kuziwekea mduara kwa kalamu siku zako za mwezi, yaani siku ya kwanza ya kupata damu ya hedhi hadi siku ya mwisho kabla ya hedhi inayofuata. Mzunguko wako wa mwezi ni siku ya kwanza ya hedhi hadi siku ya kabla ya kuanza hedhi nyingine. Kwa mfano iwapo nimepata siku zangu tarehe Pili Julai na nimepata tena siku zangu tarehe 29 Julai, mzunguko wangu ni wa siku 28. Kwa kawaida mzunguko wa siku 28 ndio mzunguko wa kawaida kwa wanawake wengi. Lakini kuna baadhi ya wanawake huwa na mzunguko wa chini ya siku 28 na wengine huwa na mzunguko wa hadi siku 35.
Ni vipi utazijua siku zako za Ovulation
Wakati wa Ovulation katika mzunguko wa mwezi huainishwa na luteal phase, katika mzunguko wako. Unaweza kujua muda wa Ovulation katika mzunguko wako wa mwezi kwa kutoa idadi ya siku za luteal phase. Katika kuhesabu huko utapata mzunguko mfupi na mrefu. Chukua mzunguko mfupi wa mwezi na hesabu idadi ya siku katika mzunguko huo. Toa 18 katika mzunguko huo na utapata idadi fulani. Halafu anza kuhesabu siku yako ya kwanza ya mzunguko wa hedhi katika mwezi unaofuata kwenda mbele hadi kufikia namba ulioyopata, hivyo utaweza kupata siku ambayo una uwezekano mkubwa wa kubebea mimba.
Kwa mfano mzunguko wako mfupi ni siku 29, unatoa 18 katika 29 na unapata 11. Iwapo siku yako ya kuanza hedhi mwezi ujao ni Oktoba 3, ongeza siku 11 kuanzia siku hiyo. Hivyo siku ambayo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba itakuwa Oct. 14.
Halafu chungua idadi ya siku za mzunguko wako mrefu wa hedhi. Toa siku 11 kutoka katika idadi ya siku za mzunguko huo na utapata namba fulani. Halafu tena anza kuhesabu katika mzunguko wako ujao wa hedhi kwenda mbele hadi kufikia siku ambayo una uwezekano wa kupata mimba.
Kwa mfano iwapo mzunguko wako mrefu ni siku 31, toa 11 katika mzunguko huo na utapata 20. Iwapo hedhi yako ijayo inaanza tarehe 3 Oktoba, ongeza siku 20 kuanzia siku hiyo na tarehe 23 Oktoba itakuwa siku yako ambayo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba.
Kwa utaratibu huo utakuwa umepata kipindi cha kati ya Oktoba 14 hadi 23 ambacho ni siku ambazo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba au Ovulation window kwa kimombo.
Ovation huweza kubadilika kidogo katika mzunguko wako wa hedhi kwa sababu Ovulation huweza kucheleweshwa na sababu mbalimbali kama vile wasiwasi au fikra nyingi, ugonjwa, lishe au kufanya mazoezi.


Vipi kipindi cha Ovulation kinaainisha ziku za kubeba mimba?
Kipindi cha kubeba mimba huanza siku 4 hadi 5 kabla ya Ovulation, na humalizika masaa 24 hadi 48 baada ya hapo hii ni kwa sababu muda wa ovulation huweza kuchelewa au kuwahi kutokana na sababu mbalimbali. Pia kwa sababu mbegu ya kiume huwa na uhai kwa siku 4 hadi 5 na yai huweza kuishi kwa masaa 24 hadi 48 baada ya kuingia katika tumbo la uzazi. Hivyo kwa kujua siku hizo humsaidia mwanamke kufahamu kipindi chake cha Ovulation kimewadia na hivyo kuweza kukukutana na mumewe au mwenza wake wakati huo ili aweze kubeba mimba. Pia kujua kipindi hiki na masuala mengineyo kama hali ya joto la mwili ilivyo wakati wa Ovulation huweza kutumika kama njia ya kuzuia mimba. Yaani kutojamiiana katika kipindi hiki huweza kumzuia mtu asipate mimba.
Kwa kuwa kipindi cha Ovulation hakina tarehe maalum na ni siku kadhaa, katika makala ijayo nitaendelea kuzungumzia baadhi ya alama za mwili zinazosaidia kutambua ni wakati gani Ovulation imewadia.
Daima tuzilinde afya zetu!

Monday, August 2, 2010

Nimerudi blogini Wadau na samahani sana kwa kupotea!


Wapenzi wadau wangu wa Kona ya Afya,
Napenda kuchukua nafasi hii kuwajulisha kwamba nimerudi blogini. Pia kuwaomba samahani kwa kusokena kw amuda mrefu kutokana na majukumu, kazi na safari za hapa na pale. Nawaahidi kwamba nitajitahidi kujibu maswali yenu mliyoniuliza na kuirejesha tena blogi yetu katika hali yake ya kawaida.
Nawatakieni Afya Njema!
Shally!

Saturday, June 19, 2010

Kunywa maji kwa mpangilio husaidia kurahisisha utendaji wa mwili



Kila mtu anajua umuhimu wa maji katika miili yetu. Sio kwamba tu mwili wenyewe umejengwa kwa asilimia kati ya 55 na 75 za maji (kwa kutegemea unene wa mtu ambapo watu wembemba wana kiasi kikubwa cha maji mwilini kuliko wanene) bali pia mwili unahitajia maji kwa kiasi kikubwa ili kufanya kazi zake vyema.
Je? Unajua mapafu yako yanahitajia vikombe wiwili vya maji hadi vinne kila siku ili kufanikisha kwa ufanisi kazi yake ya kupumua? Na kiasi hicho huhitajika ziadi wakati wa baridi.
Je, unajua wakati unapotoka jasho kikombe kimoja cha maji hupungua mwilini mwako. Na je, unatambua kwamba iwapo utaoga wakati wa mchana kwa mara karibu tatu kwa siku ni kana kwamba umekunywa vikombe 6 vya maji?
Kunywa maji kwa kiasi cha kutosha husaidia kupunguza uwezekano wa kutokea mawe katika figo, hulainisha viungo na huzuia mafua na kusaidia kupona haraka ugonjwa huo. Vilevile kunywa maji husaidia mtu kupata choo vyema.
Maji ni hitajio la dharura kwa afya zetu, kwani asilimia 60 ya uzito wako ni maji na kila mfumo wa mwili wako hutegemea maji ili kufanya kazi zake. Ukosefu wa maji mwilini humfanya mtu akaukiwe na maji au dehydration, hali ambayo hutokea pale mtu asipokuwa na maji ya kutosha mwilini ya kuuwezesha mwili wake kufanya kazi zake za kawaida. Hata katika upungufu mdogo wa maji mwilini, wakati ambapo asilimia 1 hadi 2 ya uzito wa mwili inapopungua, huweza kumfanya mtu akose nguvu na ajisike amechoka. Miongoni mwa dalili za upungufu wa maji mwilini ni:
• Kukihi kiu sana
• Uchovu
• Kichwa kuuma
• Mdomo kukauka
• Kukosa mkojo au kiasi cha mkojo kuwa kidogo.
• Udhaifu wa misuli
• Kuhisi kizunguzungu


Ni muhimu kujua kwamba mwili hupoteza maji kila siku kwa kutokwa na jasho, iwe jasho hilo umelihisi au haukulihisi, kutoa pumzi nje (exhaling), kukojoa na harakati ya tumbo. (bowel movement). Ili mwili wako uweze kufanya kazi vizuri unahitajia kurudisha maji hayo mwilini kwa kunywa vinywaji mbalimbali na vyakula vyenye maji.
Wataalamu wengi wanakubaliana kuwa mwanadamu anahitajia kunywa vikombe 8 vya maji kwa siku, ili kufidia maji yanayopotae mwilini. Hata hivyo wengine wanashauri kwamba, wanaume wanywe vikombe 13 vya maji kwa siku na wanawake vikombe 8 vya maji, na hiyo ni kutokana na tofauti ya miili yao. Tunashauriwa kuwa badala ya kunywa maji kiholela tunywe kwa mpangilio maalum kwa siku, ili kusaidia vyema katika kazi za mwili.
 Tunashauriwa kunywa vikombe viwili vya maji asubuhi pindi tunapoamka, kwani husaidia kuamsha viungo vya ndani ya mwili.
 Tunashauri tunywe kikombe kikoja cha maji dakika 30 kabla ya mlo, kwani husaidia kupata choo vizuri.
 Tunashuariwa tunywe kikombe kimoja cha maji kabla ya kwenda kuoga, husaisia kupunguza shikizo la damu.
 Na tunashauriwa kunywa kikombe kimoja cha maji kabla ya kulala kwani kufanya hivyo huzuia shinikizo la moyo.
Basi kunywa maji kwa afya yako mdau!

Sunday, June 6, 2010

Kensa kuua watu milioni 13.2 ifikapo mwaka 2030


Maafisa wa Umoja wa Mataifa wametangaza kwamba, watu zaidi ya milioni 13.2 watafariki dunia ifikapo mwaka 2030 kutokana na maradhi ya kensa, idadi ambayo ni mara mbili ya ile ya mwaka 2008. Takwimu hizo za hivi karibuni zinaonyesha pia kwamba, ugonjwa wa saratani mwaka 2008 ulisababisha watu milioni 7.6 waage dunia na kwamba kesi mpya milioni 12.7 za kensa mbalimbali zimegunduliwa mwaka huu. Nchi zinazoendelea zimeripotiwa kuwa na asilimia 56 ya kensa mpya na asilimia 63 ya kensa zote zilizoripotiwa mwaka 2008. Kensa ambazo zilitokea kwa kiasi kikubwa mwaka 2008 ni kensa za mapafu, matiti na kensa ya utumbo, rectum na apendeksi au colorectal cancer. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Kimataifa cha Utafiti wa Kensa( IARC) kesi za ugonjwa wa kensa zitaongezeka mara dufu katika miongo miwili ijayo iwapo hali ya sasa itaendelea hivyo hivyo. Christopher Wild Mkurugenzi wa IARC amesema kwamba, maradhi ya kensa hakuna sehemu yoyote duniani yasipokuwepo, hata katika nchi zilizoendelea na zenye utajiri mkubwa. Amesisitiza kwamba la kusikitisha ni kuwa maradhi ya kensa ambayo mwanzoni yalishudiwa kwa wingi katika nchi zinzoendelea hivi sasa yapo pia katika nchi masikini.

Wednesday, May 26, 2010

DAWA ZA KIUNGULIA ZINASABABISHA MPASUKO WA MIFUPA



Taarifa mpya zinasema kwamba, maafisa wa afya wametahadharisha juu ya kutumiwa kwa muda mrefu dozi kubwa ya dawa za kuondoa kiungulia, (heartburn) na kusisitiza kwamba zinasababisha mifupa kupasuka. Dawa hizo ni zile zinazojulakana kama Proton Pumping Inhibitors (PPI) zinazozuia kiungulia na ambazo hutumiwa kudhibiti kiwango cha asidi katika tumbo na pia kutibu ugonjwa wa GERD au gastroesophageal reflux disease. Taarifa hizo zilizotolewa na Kitengo cha Kusimamia Vyakula na Dawa cha Marekani (FDA) zinasema kwamba, dawa hizo za kingulia huongeza uwezekano wa kupasuka mifupa ya nyonga (hip), mikono na ute wa mgongo kwa watu wazima, hasa iwapo dawa hizo zitatumiwa kwa mwaka mmoja au zaidi, au kwa dozi kubwa.
Joyce Korvick Mkurugenzi wa masuala ya usalama wa kitengo cha FDA anasema kwamba, kwa kuwa dawa hizo zinatumiwa sana na watu wengi, ni muhimu kwa watu wote kufahamu madhara yanayoweza kusababishwa na dawa hizo. Maafisa hao pia wamewataka madaktari kuwaandikia tu dawa hizo wagonjwa ambao hali zao ni mbaya mno, na kusisitiza kuwa faida ya dawa hizo pale zinapotumiwa mara chache ni zaidi ya hatari inayozisababisha.
Huko nyuma pia wataalamu walisema kwamba, dawa hizo za kutibu kiungulia zinahusiana na ongezeko la hatari ya maambukizo ya bacteria aina ya C. difficile anayesababisha ugonjwa wa kuharisha.
Dawa hizo ni kama zile za Emsomeprazole, Dexlansoprazole, Lansoprazole, Emprazole/Sodium Bicarbonate, Pantoprazole, Rabeprazole na Rabeprazole.
Ndugu mdau kama wewe ni miongoni mwa wanaotumia dawa hizo, basi jihadhari kabla ya hatari!

Sunday, May 23, 2010

WHO YATAHADHARISHA JUU YA UNENE WA WATOTO


Mawaziri wa Afya Duniani huku wakitahadharisha juu ya ongezeko la idadi ya watoto wenye unene wa kupindukia, wamesema kwamba watajaribu kupunguza kutumiwa vyakula holela (junk food) kwa kupiga marufuku matangazo ya vyakula hivyo. Mawaziri hao wa nchi 193 duniani ambazo ni wanachama wa Shirika la Afya Duniani (WHO) wametoa muongozi kwa ajili ya mashirika ya kuuza vyakula na vinywaji visivyokuwa na ulevi kwa ajili ya watoto.
Viwanda vya vyakula na vinjwaji vimetakiwa kuongeza udhibiti katika aina zote za mauzo ya vyakula kwa watoto, na wauzaji vyakula wadogo wadogo pia wametakiwa kuacha kuzalisha na kuuza vyakula ambavyo si vizuri kwa afya ya watoto. WHO imesema kwamba, vyakula vyenye kiasi kikubwa cha mafuta, sukari na chumvi vinachangia katika kuleta magonjwa sugu kama vile kisukari, maradhi ya moyo na kensa za aina mbalimbali, magonjwa ambayo yanasababisha vifo kwa asilimia 60 duniani kote.
Timoth Armstrong Mkuu wa Kitengo cha Magonjwa Sugu na Ustawi wa Afya cha WHO amesema kwamba, unene wa kupindukia kwa watoto unaongezeka duniani. Kiwango cha ongezeko hilo katika nchi zilizoendelea ni kikubwa zaidi kwa sababu ya mabadiliko ya kasi ya lishe pamoja na jinsi mwili unavyoshughulishwa.
Yafaa kujua kuwa, tangu mwaka 1980, unene wa kupindukiwa umeongezeka mara dufu kwa watu wazima na mara tatu kwa watoto. Shirika la Afya Duniani linakadiria kuwa, watoto milioni 42 wenye umri wa chini ya miaka mitano wana uzito uliozidi, huku milioni 35 kati yao ni wale wanaoishi katika nchi zilizoendelea kiuchumi. Shirika hilo limeshauri kwamba, inabidi wazazi wapunguze kuwaachia watoto wao kuangalia televisheni, na mashuleni na katika sehemu za michezo za watoto kusiwe na vyakula holela na vinywaji vyenye sukari nyingi.

Thursday, May 20, 2010

Chanjo ya Ndui kuzaidia kupambana na virusi vya HIV


Kutotumiwa chanjo ya ndui katika baadhi ya nchi duniani kunaaminika kuwa kumesaidia katika kueneza maambukizo ya virusi vya HIV, hasa kwa kuzingatia kuwa ugonjwa huo umeongeza sasa siku hizi. Chanjo ya ndui polepole ilianza kutotolewa katika baadhi ya nchi duniani na ugonjwa wa ndui kutokomezwa katikati mwa karne ya 20. Utafiti uliochapishwa katika jarida la BMI Immunology umeonyesha kwamba, chanjo ya ndui ilikuwa ikipunguza maambukizo ya virusi vya HIV, hasa mwanzoni ugonjwa huo ulipogunduliwa duniani. Lakini kuacha kutolewa chanjo hiyo na wataalamu wa Afya, kunaweza kuwa ndio sababu iliyopelekea ongezeko la maambukizo ya ugonjwa wa Ukimwi yaongezeke. Wataalamu waliofanya utafiti huo wanasema kwamba, kuna sababu kadhaa zilinazoweza kutolewa kuhusiana na kasi ya ongezeko la Ukimwi barani Afrika, baadhi ya sababu hizo ni vita, kurudiwa kutumiwa sindano bila kuondolewa vijidudu (unstrelizized needles) pamoja na chanjo za ndui za mwanzo ambazo zilikuwa na vijidudu. Hata hivyo, wataalamu hao wamesema kuwa, sababu zote hizo zimekanushwa au hazitoshi kuelezea sababu ya ongezeko kubwa la maambukizo ya HIV duniani hasa barani Afrika.
Chanjo ya ndui inapunguza uwezekano wa virusi vya HIV kuzaana mara kadhaa katika seli za damu. Pia chanjo hiyo huleta mabadiliko ya muda mrefu katika mfumo wa kulinda mwili, hubadilisha tafsiri ya recepta ya CCR5, ambayo iko juu ya seli za chembechembe nyeupe za damu zinazotumiwa na virusi vya ndui pamoja na HIV.
Wataalamu wanamini kwamba chanjo ya ndui itaweza kutumiwa katika kupambana na ugonjwa wa Ukimwi katika miaka ijayo ya hivi karibuni, lakini pia wamesisitiza kwamba uchunguzi zaidi unapaswa kufanywa ili kuhdibitisha zaidi suala hilo.


Ugonjwa wa ndui ni miongoni mwa magonjwa ambayo yaliitikisa dunia katika miaka ya huko nyuma. Lakini kugunduliwa chanjo ya ndui ambapo kwa kupatiwa chanjo ya ugonjwa huo mara moja mtu huweza kuwa na kinga dhidi ya ugonjwa huo kwa maisha yake yote, kulipunguza maambukizo ya ugonjwa huo na hatimaye ugonjwa huo ukang'olewa kabisa karibu katika nchi zote duniani. Ndugu mdau, kama huna uhakika kama umepatiwa chanjo ya ndui, basi angalia katika moja ya mabega yako na kama utakuta kovu dogo la duara, basi ujue kuwa una kinga ya ndui. Nawahusia wakina mama wanaowazaa watoto wao siku hizi wahakikishe kwamba wanapatiwa chanjo ya ndui, kwani kama inavyoelezwa mbali ya kumzuia mtoto wako asipate ugonjwa wa ndui maishani, pia hupunguza maambukizo ya ugonjwa wa Ukimwi. Haya tena wadau lakini wewe unafikiri ni sababu gani hasa inayopelekea ongozeko la maambukizo ya Ukimwi katika jamii zetu?..... tueleze maoni yako ili tusaiidiane katika kuifunza jamii na kupambana na ugonjwa hatari wa Ukimwi.

Sunday, May 16, 2010

Kupewa watoto sukari kabla ya chanjo kunapunguza maumivu


Watafiti wa Canada wamesema kuwa, kuwapa watoto sukari kabla ya kupewa chanjo kunapunguza maumivu. Watafiti wa Chuo Kikuu cha Toronto wamesema kwamba watoto wachanga wakipewa matone machache ya maji ya sukari, kabla ya chanjo hawatolia au watapunguza kulia. Hayo yamesemwa baada ya watoto 1,000 wachanga kupewa maji ya glukosi kabla ya kupigwa sindano na kupunguza kulia kwa asilimia 20. Utafiti huo umechapishwa katika jarida la Mafanikio ya Magonjwa ya watoto na umetokana na matokeo ya majaribio 14 yaliyofanywa kuhusiana na suala hilo. DaktaArme Ohlsson aliyeongoza timu ya utafiti huo amesema kwamba umefanywa kwa watoto wasiozidi mwaka mmoja. Pia watatifi hao wamesema kwamba, matone machache tu au nusu kijiko cha maji ya glukosi au sackrosi pia hupunguza muda wa mtoto kulia. Pia wamewashauri maafisa wa afya wawape watoto sakrosi na glukosi kabla ya kuwapatia chanjo. Wamesema kwa kuwa vyakula vitamu vina uwezo wa kupunguza maumivu ndio sababu watoto wanapopewa glukosi kabla ya chanzo huwa hawalii.

Wednesday, May 12, 2010

Kuchoka wakati wa ujauzito na namna ya kujiepusha

Wapenzi wadau natumaini hamjambo! kumekuwa na baadhi ya wadau wanaoniandikia na kuomba ushauri mbalimbali kutokana na matatizo waliyonayo. Nawashukuru sana kwa kuwa wanafuatilia yale yanayojiri katika blogi hii na kupata ingawa machache kuhusiana na afya zetu. Pia nawashukuru kwa kuniwezesha nami kuzungumzia mada mbalimbali kutokana na maswali yenu munayoyauliza. Kwa wale wenye maswali na matatizo mbalimbali tafadhali sana niandikieni kwa kupitia email yangu ambayo ni sthugs4j@gmail.com. Kwani wale wanaoandika maswali yao katika sehemu ya maoni, baadhi ya wakati huwa siyaoni katika muda unaotakiwa na hivyo hunifanya nichelewe kuwajibu. Wote mnashukuriwa. Leo tutazungumzia suala la kujihisi uchovu wakati wa ujauzito ambalo limeulizwa na mmoja wa wadau wanaofuatilia kwa karibu kona ya afya nami nalijibu swali lake kama ifuatavyo.

Wanawake wengi kwa kawaida huwa wanahisi uchovu wakati wa ujauzito. Uchovu, kulegea mwili na kuishiwa na nguvu ni jambo la kawaida katika kipindi hicho. Hii ni kwa sababu mwili katika kipindi hiki unatumia nguvu za kiada ili kuunda kiumbe kipya. Pia wakati huu mwili hutengeneza damu kwa wingi zaidi ili kufikisha chembechembe za chakula kwa mtoto, suala ambalo huufanya mwili ufanye kazi ya ziada na hata viungo vingine muhimu kama vile moyo na vinginevyo. Uzito wa mtoto nao unaoongezeka katika mwili wa mama mjamzito siku baada ya siku, ni sababu nyingine inayomfanya mama mjamzito ajihisi kuchoka. Kuchoka au kiushiwa na nguvu ni tatizo la kawaida hasa katika miezi mitatu ya mwanzo ya mimba. Katika miezi hiyo ya mwanzo ya mimba tatizo hilo husababishwa na mabadiliko ya homoni za mimba mwilini hasa progestrogen na wakati mwingine hali hiyo huongezwa na kichefuchefu na kutapika. Hali hiyo ya mchoko inatarajiwa kuisha inapoingia miezi mitatu ya pili ya mimba. Lakini pia kuna wengine ambao hali hiyo ya kuchoka huendelea nayo hadi wakati wa kujifungua. Kushindwa kulala vizuri kutokana na kwenda mara kwa mara msalani, au kukosa uzingizi kutokana na ongezeko la ukubwa wa tumbo mwishoni mwa ujauzito, ni miongoni mwa masuala ambayo humfanya mama mjazito ajisikie mchovu na akose nguvu siku nzima.
Vilevile mabadiliko ya kifizikia na kisaikolojia ya wakati wa ujauzito humfanya mama mjamzito awe na morali ya chini na kuhisi uchovu wa kimwili na hata kiakili. Sababu nyinginezo zinaweza kutokana na kazi mbalimbali anazofanya mama huyo au pia ukosefu wa lishe inayofaa na ya kutosha kwa ajili ya mwili wake, ambao unahitajia nguvu ya ziada hasa kwa ajili ya uumbaji wa ukamilifu wa mtoto aliye tumboni.
La muhimu analoshauriwa mama mjamzito ni kutoogopa na kutotishwa na hali hiyo, kwani inatokana na baadhi ya mabadiliko yanayotokea katika mwili wake. La muhimu ni mama mjamzito kufuata ushauri unaotakiwa ili kukabilina na hali hiyo.
Zifuatazo ni njia za kukabiliana na uchovu wakati wa ujauzito.
• Kwanza kabisa mama mjamzito anatakiwa ale vyema. Mama mjamzito anatakiwa ale chakula bora na kamili, chenye kalori 300 au 500 za ziada ikilinganishwa na mtu asiye mjamzito kwa siku. Lakini awe mwangalifu na ni bora akigawe chakula chake katika sehemu ndogo ndogo 5 au 6 (suala hili tumelizunguzia kwa undani katika makala iliyopita ya kiungulia wakati wa ujauzito, tafadhali pitia makala hizo). Anaweza akawa akibeba matunda na mboga mboga kama asusa (snacks) kwa ajili ya kula kila anapohisi njaa popote pale awapo. Lakini ni bora ajiepushe na vyakula vyenye sukari nyingi na caffeine, kwani vyakula hivyo huyeyuka haraka mwilini na kumfanya ahisi njaa mapema.
• Mama mjamzito ahakikishe kuwa hana upungufu wa damu. Na kama anao basi atumie dawa za kuongeza damu zinazotolewa na madaktari, au ale vyakula vinavyoongeza damu. Hii ni kwa sababu ukosefu wa madini ya chuma mwilini unaosababisha ukosefu wa damu, ni miongoni mwa sababu zinazomfanya mama mjamzito ahisi kuchoka. Mtu mwenye ukosefu wa damu (Anemia) huhisi kubanwa na pumzi, ongezeko la mapigo ya moyo, udhaifu, kupauka na kizunguzungu. Onana na daktari iwapo una dalili kama hizo.



• Mama wajawazito wanashauri kujipumzisha nyakati za mchana. Ni bora mama mjamzito apumzike kwa kadri anavyoweza wakati wa mchana, baada ya chakula cha mchana au hata kabla ya nyakati za magharibi. Ikiwa unafanya kazi, basi pumzika mara kwa mara japo kwa muda mfupi ili kufanya mwili upate nguvu.
• Mama wajawazito wanashauriwa kujitahidi kulala mapema, hasa kama ikiwa inakubidi uamke mara kadhaa usiku kutokana na sababu mbalimbali, kama vile kwenda msalani, kula au kutokana na maumivu.
• Kufanya mzoeni husaidia kupunguza uchovu na kuna faida kemkem wakati wa ujauzito. Kahusiana na suala hilo soma makala zilizotangulia.
• Mama mjamzito anatakiwa anywe maji ya kutosha. Ukosefu wa maji mwilini huchangia kumfanya mama mjamzito ahisi uchovu.
• Usifanye kazi nyingi kutwa nzima, na kama inawezekana ni bora usaidiwe kazi hizo hasa za nyumbani na watu wengine katika familia kama vile watoto, mume ndugu, jamaa na marafiki.
• Usikilize mwili wako. Pale unaposikia njaa basi kula na pale unapojisikia uchovu jitahidi upumzike.
• Pata ushauri wa daktari iwapo unahisi uchovu wa kupindukia au unachoka kila mara, ili uwe na uhakika kuwa hakuna tatizo au hatari inayoweza kuhatarisha maisha yako na ya mtoto.

Saturday, May 8, 2010

Kula zabibu usipatwe na ugonjwa wa moyo


Wadau msichoke na mimi kuzungumzia ugonjwa wa moyo, au nisiseme mimi, bali niseme wataalamu ambao kila siku wamekuwa wakifanya majaribio na kutuelewesha vyakula au njia zinazotuepusha na ugonjwa huu. Hii ni kwa sababu ugonjwa wa moyo kweli ni tishio duniani kote. Ni wiki iliyopita tu mfanyakazi mwenzangu ambaye nilikuwa naye kazini hadi nyakati za mwisho za kazi, siku ya pili nakuja kazini naambiwa kafariki dunia kwa mshituko wa moyo. Masikini baba wa watu!!, huku akiwa anayetegemewa na familia, akiacha mke na mtoto ameondoka kama utani tena kwa kufumba na kufumbua. Baada ya kutoka kazini alikaa juu ya kochi na kujiegemeza akisubiri atengewe msosi, lakini hapo hapo aliaga dunia. Msosi ulipotengwa na mkewe kumuamsha ale akidhani labda amepitiwa na usingizi, aliona haamki tena, na ndipo walipomkimbiza hospitalini. Huko waliambiwa ameshakufa zamaaani kutokana na mshituko wa moyo!.
Sasa hali ni hii, na hivi karibuni uchunguzi mpya umeonyesha kwamba kula zabibu au vyakula vyenye zabibu ndani yake kunapunguza shinikizo la damu, husaidia moyo kufanya kazi zake vyema na kupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliotolewa kenye mkutano wa Majaribio ya Bayolojia huko California, zabibi zina uwezo wa kupunguza shinikio la damu, husaidia mwili uweze kuvumilia sukari (glucose tolorance) na kupunguza kiwango cha mafuta aina ya triglycerides mwilini ambayo ni chanzo cha matatizo ya moyo.

Wataalamu wanasema zabibu pia zinaweza kupunguza uvimbe, uharibivu unaotokana na free radicals zinazozalishwa mwilini na shinikizo la moyo.
Kwa ujumla zabibi zinazuia hali inayoitwa Metabolic Syndrome suala ambalo linatokana na mada za phytochemicals zilizoko kwenye matunda hayo.
Metabolic Syndrome ni mchanganyiko wa matatizo ya kitiba ambayo yanaongeza uwezekano wa kupatwa na maradhi ya mishipa ya damu pamoja na kisukari.
Hivyo wataalamu wanatushauri tule zabibi au kuongeza zabibu katika vyakula wanavyokula kila siku, ili tujikinge na ugonjwa wa Metabolic Syndrome, ugonjwa wa moyo na kisukari aina ya pili.
Haya shime tule zabibu kwa ajili ya afya zetu!.

Friday, May 7, 2010

Kweli lishe bora inaongeza umri…. Afa akiwa na miaka 114!


Mwanamke wa Kijapan aliyevunja rikodi ya Dunia ya Guinness kwa kuwa mtu mzee zaidi duniani amefariki dunia siku kadhaa zilizopita, akiwa na umri wa miaka 114 na siku 357. Mwanamke huyo aitwaye Kama Chinen alikuwa akiishi katika kisiwa cha Okinawa na alifariki dunia Mei 2, ambapo aliishi na kushuhudia karne tatu!. Inasemekana kuwa bibi huyo aliishi muda mrefu kwa kuwa lishe yake ilikuwa chai ya kijani, supu ya miso, mboga mboga, wali na samaki freshi. Bi. Chinen sio makazi pekee wa eneo hilo la Japan aliyeishi muda mrefu, kwani ripoti zinasema kuwa watu wengi wanaoishi eneo hilo huishi maisha marefu na ni kutokana na lishe yao. Japan ndio nchi inayoongoza kwa kuwa na kiwango kirefu zaidi cha maisha ya watu (Highest Life Expactancy) huku Okinawa ukiwa mji ulio na watu wengi wenye umri mrefu, suala ambalo linatokana na lishe bora na hali ya hewa ya kisiwa hicho.
Kwa mujibu wa utafiti, mji wa Okinawa una kiasi kidogo sana cha watu wenye magonjwa ya kensa, na hiyo inatokana na watu kula vyakula vyenye mafuta kidogo, kalori chache, ufumwele kwa wingi na mboga mboga na matunda kwa kiasi kikubwa. Pia suala lingine ni kujishughulisha kwao na wala sio kukaa tu.

Wednesday, May 5, 2010

Kukosa usingizi kunasababisha vifo vya mapema


Imetahadharishwa kwamba kulala usingizi wa chini ya masaa 6 kila usiku kunaweza kusababisha mtu apatwe na kifo cha mapema. Watafiti wamesema kuwa watu ambao kwa kawaida huwa wanalala masaa hayo machache wengi wao hupatwa na vifo vya mapema kwa asilimia 12 zaidi ya wale wanaolala kawaida kwa masaa 8. Vifo ambavyo hutokea katika umri wa baada ya miaka 25. Pia imeonyeshwa kwamba kulala zaidi ya masaa 9 pia kunapelekea vifo vya mapema ingawa kulala huko kunaweza kukawa na uhusiano na matatizo ya kiafya. Utafiti huo umetolewa kwa kuchunguzwa uhusiano uliopo kati ya kifo na usingizi kwa kutegemea chunguzi 16 zilizofanywa kwa kuwahusisha watu milioni 1 na nusu katika nchi za Uingereza, Marekani , Ulaya na Mashariki mwa Asia.
Profesa Francesco Cappiccio aliyeongeza utafiti huo wa chuo kikuu cha Warwick cha Uingereza anasema jamii za hivi sasa zilizoendelea zimekuwa taratibu zikipunguza muda wa kulala, na tatizo hili linawapata sana watu wanaofanya kazi masaa mengi. Amesema suala hili linaonyesha kwamba hayo yote yanatokana na mashinikizo ya kimaisha yanayowapelekea watu wafanye kazi masaa mengi na kuchukua shift nyingi za kazi. Amesema kwamba, kuporomoka kwa afya kunaambatana na kulala masaa mengi zaidi. Wataalamu wanasema kuwa, watu wanapaswa kufahamu kwa nini hasa usingizi ni suala muhimu sana kwa afya nzuri. Usingizi ni kama karatasi ya litmus inayoonyesha afya na hali ya mwili na akili ya mtu kwani usingizi unaathiriwa na magonjwa na hali mbalimbali ikiwemo msongamano wa mawazo au depression, anasema mtaalamu huyo. Inashauriwa kuwa tusilale masaa machache wala mengi bali tulala kwa masaa ya wastani ambayo ni masaa 8.

Monday, May 3, 2010

Madaktari waboronga katika upasuaji Afrika Kusini na kuhatarisha maisha


Gazeti moja nchini Afrika Kusini limefanya uchunguzi na kuripoti kuwa, madakitari wa upasuaji nchini humo wanafanya kazi isiyo ya kuridhisha na yenye kuhatarisha maisha ya wagonjwa wanaokwenda kupasuliwa. Gazeti la Sunday Independent limesema kuwa, uchunguzi wao umedhihirisha kuweko malalamiko ya waliopasuliwa, wengine wakilazimika kurudi kufanyiwa upasuaji mwingine, wanapogundua vifaa fulani vimeachwa mwilini mwao. Gazeti hilo limemnukuu msemaji wa Waziri wa Afya wa Afrika Kusini Fidel Hadebe akisema, amepokea ripoti kwa mhasiriwa mmoja aliyedai kuwa, mikasi ilibakia tumboni mwake alipofanyiwa upasuaji. Aidha uchunguzi wa gazeti hilo umeonyesha kuwa, sababu ya kushuhudiwa hali kama hizo uhaba wa matabibu nchini humo, jambo linalopelekea madaktari wachache walioko, kuboronga katika kazi zao katika juhudi zao za kuhakikishwa wanawafanyia upasuaji wagonjwa wengi.

Sunday, May 2, 2010

Kula aina mbalimbali za matunda kuna faida zaidi kiafya



Uchunguzi mpya umeonyesha kwamba watu wanaweza kukabiliana kirahisi na magonjwa mbalimbali kwa kula matunda ya aina mbalimbali na mboga mboga badala ya kuongeza idadi ya matunda na mboga mboga hizo. Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliotolewa katika Kongamano la Majaribio ya Kibiolojia huko Anahein California, baadhi ya matunda na mboga mboga yana faida kubwa ya lishe kuliko mengineyo. Uchunguzi huo umeeleza kwamba,ingawa karoti inaaminiwa kuwa ni chanzo kikubwa cha beta-carotene lakini kula viazi vitamu badala ya karoti kunaweza kuupatia mwili beta-carotene mara dufu kuliko karoti. Papai nalo lina beta-cryptoxanthin mara 15 zaidi ya machungwa. Halikadhalika mboga aina ya Kale huupatia mwili mada ya lutein/zeaxanthin mara tatu zaidi ya spinachi. Pia imeelezwa kuwa stroberi na rasberi zina ellagic asid mara tatu zaidi huku kikombe kimoja cha maji yanayotokana na mmea uotao majini wa watercress ikiwa na mada ya isothiocyanate sawa na inayopatikana katika vijiko vine vya chai vya haradali au mustard. Bi. Keith Rabdolph aliyeongeza uchunguzi huo anashauri kwamba, watu wajitahidi kujua umuhimu wa vyakula wanavyokula na kujua pia ubora na faida za matunda na mboga mboga wanazokula kwa afya ya miili yao.

Wednesday, April 21, 2010

Wanamichezo hawapati ugonjwa wa moyo


Utafiti mpya umeonyosha kuwa, kufanya mazoezi kwa muda mrefu hakuhusiana na kuongeza hatari ya kupata ugonjwa wa moyo. Huko nyuma kulikuwa na tafiti zilizoonyesha wasiwasi wa afya ya mishipa ya moyo kwa baadhi ya wanamichezo wa Olimpiki. Tafiti hizo zilisema kwamba, kupanuka kwa mioyo ya wanamichezo kunakoitwa kitaalamu “athlete’s heart” huufanya moyo kuwa dhaifu sana na kushindwa kuvumilia mazoezi mazito.
Lakini kwa mujibu wa uchunguzi uliochapishwa kwenye Jarida la Marekani la Kitengo cha Magonjwa ya Moyo, mazoezi mazito hayana hatari kwa afya ya moyo.
Kiwango cha damu inayosukumwa katika miili ya wanamichezo hakibadiliki wakati wa mazoezi. Mbali na kupanuka kidogo baadhi ya sehemu za moyo, misuli ya moyo hubakia sawa wakati wa mazoezi. Wanasayansi wamehitimisha kwamba, mioyo ya wanamichezo ina afya nzuri na inaweza kuvumilia kirahisi mazoezi ya kiwango cha juu. Pia wamesema kwamba, baadhi ya dawa kama vile erythropoietin (EPO) zinazotumiwa na wanamichezo hao ili kuzipa nguvu chembe chembe nyekundu za damu, kunaufanya utendaji kazi wa moyo udhoofu, suala ambalo limekuwa likiwatokea wanamichezo hao na wala sio mazoezi mazito ya mwili wanayoyafanywa.

Sunday, April 18, 2010

Unataka kuacha sigara ?..... fuata njia zifuatazo!


 Je, unataka kuacha kuvuta sigara? Sawa, nakubaliana na wewe lakini unajua kwa nini unataka kuacha tabia hiyo ambayo umeizoea kwa muda mrefu?. Kwa sababu haitoshi tu utake kuacha kuvuta sigara bila kuwa na sababu muhimu inayokusukuma uache suala hilo. Kwa hivyo kwanza anza kujiuliza kwa nini unataka kuacha sigara. Kujua sababu kutakusaidia katika kutekeleza lengo lako vyema. Je, unaacha sigara kwa kuwa unataka kuilinda familia yako isipate madhara ya sigara unazovuta? Je, unataka kuacha sigara kwa kuwa umeogopa kupata kensa ya kifua? Au je, ungependa kuonekana kijana zaidi? Tafuta sababu muhimu ambayo itaizidi hamu yako ya kuvuta sigara.


 Jua kuwa ni jambo gumu kuacha tabia uliyoizoea kwa muda mrefu mara moja. Haitowezekana utupe kipande chako cha sigara yako mara moja na kutangaza kuwa umeacha kuvuta. Suala hilo ni gumu kwani asilimia 95 ya watu wanaojaribu kuacha sigara kwa mtindo huo hushindwa, inabidi upate ushauri na tiba mbadala ili kukusaidia kuacha kuvuta sigara, hii ni kwa sababu sigara inaleta uraibu wa nicotine, na ubongo unaizoea mada hiyo hivyo kuacha kuvuta husababisha uhisi dalili za kukosekana nicotine katika ubongo.
 Jaribu kutumia vitu vingine badala ya nicotine. Hii ni kwa sababu unapoacha sigara na kukatisha nicotine mwilini hukufanya usijisikie kama umechanganyikiwa, uhisi msongamano wa mawazo na kutotulia. Suala hilo linaweza kusaidiwa kwa kupata tiba mbadala ya kusaidi kuondo hisia hizo. Wataalamu wanashauri kutumia ubani wa nicotine (nicotine gum), pipi za nicotine na baadhi ya plasta za kubandika mwilini zenye kusaidia kuacha sigara bila kuhisi madhara ya kukosa nicotine. Kutumia vitu hivyo wakati ukiwa bado unafuta sigara hakushauriwi.



 Ikiwa hutaki kutumia vitu vingine vyenye nicotine wakati umeacha sigara, mwombe daktari wako akuandikie vidogo ambavyo vinavyoondoa athari za mwili kuzoea nicotine wakati unapoacha sigara.
 Usijiamulie peke yako na kwa siri, bali itangazie familia yako, waambie marafiki zako na wafanyakazi wenzako kwamba umeacha sigara! Kukupa moyo kwao kutakufanya uweze kufanikisha lengo lako hilo kwa urahisi zaidi. Pengine unaweza kujiunga na vikundi vya wanaoacha kuvuta sigara au kwenda kwa mshauri ili akusaidie suala hilo.




 Jizuie usipatwe na msongamano wa fikra na mawazo mengi. Hii ni kwa sababu moja ya sababu inayowafanya watu wavute sigara ni kwa kuwa nicotine huwafanya wajihisi hisia nzuri mwilini na mwili kulegea. Utakapoacha sigara itakubidi utafute njia za kukabiliana na stress. Ni bora ukipata masaji ya mwili kila mara, usikilize mziki mwororo, huku ukijizuia na yake yatakayo kufanya upate mawazo na msongamano wa fikra na ikiwezekana fanya yoga na mazoezi ya kulegeza mwili.
 Jiepushe na pombe na vitu vinginevyo vinavyoweza kukushawishi uvute sigara tena. Pombe ni miongoni mwa vishawishi vikubwa vya kukufanya uvute sigara. Hivyo kama wewe ni mnywaji ni bora inabidi uache kunywa hasa wakati huu unaotaka kuacha sigara. Kama kahawa pia inakufanya usijikie kuvuta, iacha na unywe chai badala yake. Na kama huwa unavuta baada ya mlo, basi tafuta kitu kingine cha kufanya kama vile kupiga mswaki au kutafuna ubani baada ya kula.


 Baada ya kuvuta sigara yako ya mwisho, tupa vidude vyote vya kuhifadhia majivu ya sigara na viberiti. Fua nguzo zako zote zinazonuka sigara na safisha kapeti lako na nyuma yako kwa ujumla. Tumia marashi ya kuondoa harufu ili kuondoa harufu ulioizoea ya sigara nyumbani kwao. Hii ni kwa ajili ya kukusaidia usihisi harufu yoyote itakayokukumbusha kuvuta sigara.
 Jaribu tena na tena! Usitosheke kwa kuacha kuvuta mara moja na kushindwa. Wavutaji wengi huacha sigara mara kadhaa kabla ya kufanikiwa. Fikiria kila mara azma yako ya kuacha kuvuta sigara na jipe moyo na mwishowe utafanikiwa.


]
 Kuushughulisha mwili na mazoezi kunaweza kukusaidia kupunguza hamu ya sigara na dalili zinazofuata baada ya kuacha kuvuta. Utakaposhawishika na kutaka kunyoosha mkono wako ili uchukue sigara, vaa viatu vyako na uende ukatembee kidogo, kacheze mpira au fanya mazoezi yoyote kama vile kukimbia na mengineyo.
 Usijaribu kujinyima chakula wakati unapoacha sigara. Badala yake kula wa wingi matunda, mbogamboga na maziwa. Uchunguzi uliofanywa na Chuo Kikuu cha Duke umeonyesha kwamba, vyakula hivyo vinakufanya uhisi ladha ya sigara ni mbaya.




 Jiwekee zawadi nono na jipongeze. Kuacha sigara mbali na kukufaidisha kiafya hukusaidia pia kujiwekea fedha zako ambazo ungezipoteza bure kwa kununua sigara. Jipongeze kwa kutumia sehemu ya fedha hizo kujinunulia zawadi.
 Acha sigara kwa afya yako! Tambua kuwa kuacha sigara kutakupatia faida kemkem kiafya kama vile kupunguza shinikizo la damu, kupunguza mapigo ya moyo. Siku moja tu baada ya kuacha sigara, kiwango cha Carbon monoxide cha damu yako kitarejea katika hali ya kawaida. Baada ya miezi mitatu hadi minne, hatari ya shinikizo la moyo hupungua na mapafu yako huanza kufanya kazi kama kawaida. Miongoni mwa faida za kuacha sigara ni hupunguza hatari ya kupata magonjwa ya moyo, mshituko wa moyo, kensa ya mapafu pamoja na saratani nyinginezo.

Friday, April 16, 2010

Aspirin hutibu migreni


Wakati mauamivu makali ya kichwa au migraie yamekuwa yakitibiwa kwa dawa kali za maumivu, uchunguzi mpya umegundua kuwa dozi moja tu ya aspirini inaweza kuwaopunguzia maumivu walio na ugonjwa huo. Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Cochrane Library, kunywa dozi moja ya aspirini ya kati ya miligramu 900 hadi 1000 kunaweza kupunguza mauvimu makali ya migraine kwa masaa mawili. Hata hivyo utafiti huo umesema dawa hizo zinaweza kuwafaa baadhi ya watu na zisiwafae wengine na kwamba hiyo ni kutokana na tofauti ya genetiki. Kunywa dozi kubwa ya asprini kumeripotiwa kuwa na athari ya kupunguza kichefuchefu, kutapika na hata hali ya kutoweza kuvumilia mwanga na sauti (photophobia na phonophobia) hali ambazo hujitokeza kwa wale wanaopatwa na migraine.
Lakini wataalamu wamewashauri wale wanaosumbuliwa na maumivu ya kichwa ya migraine wajiepushe kutumia vidonge hivyo kwa muda mrefu kwani aspirini zinaweza kuleta athari mbaya kama vile matatizo ya tumbo.

Vifo vya kinamama vimepungua duniani

Takwimu za mwisho zinaonyesha kwamba idadi ya vifo vya kimamama vimepungua duniani kutoka nusu milioni mwaka 1980 hadi chini ya vifo 350,000 mwaka 2008. Vifo vya kinamama vinavyotokana na ujauzito au Maternal ni vifo vya kina mama vinavyotokea wakati wa ujauzito au katika siku 42 mwishoni mwa ujauzito. Vifo hivi hutokana na sababu yoyote unayohusiana na ujauzito au masuala mengine yanayoambatana na hali hiyo.


Idadi hiyo ya vifo imekuwa ikitumika kutambua na kuonyesha kiwango cha hali ya huduma za afya katika maeneo mbalimbali duniani.
Kwa mujibu wa uchunguzi ulioshapishwa na jarida la The Lacent, idadi ya kinamama wanaofariki dunia kutokana na matatizo ya ujauzito imepungua kwa zaidi ya asilimia 35, katika kipindi cha miaka 30 iliyopita. Hii ni katika hali ambayo nchi kama vile China, Misri, Ecuador na Bolivia zimefanikiwa kufikia malengo ya kimataifa ya kupunguza idadi ya wanawake wanaofariki dunia kutokana na matatizo ya ujazito, huku nchi za Marekani na Norway zikiripotiwa kushuhudia ongezeko la vifo hivyo. Wengi wanasema kwamba, sababu kuu iliyopelekea ongezeko la vifo hivyo katika nchi hizo mbili ambazo ni tajiri na zenye huduma bora ya tiba ni kuongezeka magonjwa miongoni mwa kinamama wajawazito pamoja na kinamama kubeba mimba katika umri mkubwa.

Vilevile imeripotiwa kwamba kwenye nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika katika kila wanawake watano wajawazito mmoja kati yao ana virusi vya HIV. Ugonjwa ambao umesababisha vifo vya watu 61,400 katika mwaka 2008. Asimilia 80 ya vifo vya kina mama wajawazito hutokea katika nchi 21 duniani ambapo India, Pakistan, Nigeria, Afghanistan, Ethiopia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo zinachangia zaidi ya nusu ya idadi yote hiyo ya vifo vilivyoripotiwa.

Wednesday, April 7, 2010

Cheka unenepe na uishi maisha marefu


Utafiti mpya umeonyesha kwamba, kuna uhusiano kati ya kucheka na kuishi maisha marefu.
Utafiti huo uliochapishwa katika Jarida la Saikolojia la Sayansi umeonyesha kwamba, watu wenye tabasamu pana linalojulikana kama "Dunchenne smile, huishi maisha marefu. Ernest L. Abel aliyeongoza utafiti huo amesema kwamba, watu ambao wanaonyesha hisia zao na kuziakisi kwa tabasamu pana, kimsingi huwa ni watu wenye furaha zaidi ya wale wenye kutabasamu kidogo. Hivyo watu hao hufaidika na suala hilo na kwa kawaida huishi maisha marefu.
Wataalamu wanasema kwamba watu wenye kutabasamu sana kwa kawaida huwa wana furaha, wana shaksia madhubuti, ndoa zao hudumu zaidi, wana ufahamu mzuri zaidi wa mambo na huashiriana vyema na watu wengine.

Monday, April 5, 2010

Yawezekana kuokoa maisha ya wenye HIV kwa kutumia dawa zisizo ghali

Wachunguzi wa masuala ya tiba wamesema kwamba, bado hakuna jitihada zinazofanywa za kuokoa maisha ya maelfu ya watu wanaoishi na virusi vya HIV kwa kutumia dawa rahisi na zisizo ghali. Wamesisitiza kwamba kuwapa dawa za anti-biotics kama vile co-trimoxazole wale ambao tayari wamegunduliwa kuwa na virusi vya Ukimwi kunaweza kupunguza idadi ya vifo vya wagonjwa hao mwanzoni tu wanapopata ugonjwa huo.

Uchunguzi huo uliochapishwa katika Jarida la Tiba la Lancet umegundua kuwa, kuwapa waathirika wa Ukimwi anti-biotics kunapunguza nusu ya vifo vya wagonjwa hao. Shirika la Afya Duniani WHO) tayari limeamuru kutolewa matibabu hayo lakini wataalamu na madakatari wanasema kuwa watu wengi bado hawapewi dawa hizo. Jitihada nyingi zimekuwa zikifanywa tu kuhakikisha kwamba wale walioathirika na Ukimwi wanapatiwa dawa za kuongeza maisha za antiretroviral ambazo zina athari kubwa katika kuwaongeza maisha. Hata hivyo, wagonjwa wengi wa Ukimwi katika wiki za mwanzo baada ya kugundulika kuwa wana ugonjwa huo, wanakabiliwa na hatari kubwa ya kushambuliwa na magonjwa mbalimbali kutokana na kudhoofu mfumo wao wa kinga wa mwili. Hivyo wataalamu wanasema kwamba, kuongezwa dawa kama vile co-trimoxazole ambazo ni anti-biotic zisizo ghali na ambazo hupatikana kwa urahisi, katika matibabu yao ya muda mrefu kunaweza kuwanusu na kifo.


Takwimu zimeonyesha kuwa, zaidi ya robo ya waathiriwa wa Ukimwi waliopewa dawa za kuongeza maisha za antiretroviral katika nchi za chini ya Jangwa la Sahara walifariki dunia katika mwaka wa kwanza wa matibabu. Lakini uchunguzi uliofanywa na Lancent umeonyesha kwamba, kati ya Waganda 3,179 wenye virusi vya Ukimwi, waliopewa dawa hizo pamoja na kuongezewa anti-biotic katika mpango wao wa matibabu, dawa hizo ziliwapunguzia vifo kwa asilimia 59 katika wiki 12 za kwanza, na kwa asilimia 44 kati ya wiki 12 na 72 za matibabu.
Hata hivyo imeonekana kwamba dawa hizo za anti-biotics hazipatikani katika maeneo mengi ya nchi za Uganda na Zimbabwe ambako kuna wathirika wengi wa Ukimwi.
Pia imeonekana kuwa kutumiwa dwa hizo za nyongeza kuna faida nyingine ya ziada ambayo ni kuepusha maambukizo ya ugonjwa wa Malaria kwa asilimia 15.

Sunday, April 4, 2010

Dawa ya kensa ya tezi kibofu (prostate cancer) yaonyesha matumaini zaidi

Dawa ya kensa ambayo tayari inatumiwa na wagonjwa wenye uvimbe wa tezi za kibofu imeonekana kuwa ina uwezo wa kuzuia ugonjwa huo usiendelee zaidi. Katika uchunguzi wa kimataifa imeonekana kuwa, wanaume waliopewa dawa hiyo ijulikanayo kama Dutasteride katika jaribio la kitiba, wameripotiwa kupungukiwa na hatari ya kupata ugonjwa wa kensa ya tezi kibofu (prostate cancer) kwa asilimia 23. Wanaume wote hao walikuwa wana uwezekano wa kupatwa na ugonjwa huo maishani.

Wataalamu wamepokea kwa furaha matokeo hayo lakini wamesema kwamba bado utafiti wa muda mrefu unatakiwa kufanywa kuhusiana na dawa hiyo.
Huko nyuma pia wataalamu waligundua pia dawa nyingine kama hiyo iitwayo Finasteride inapunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa kensa ya tezi kibofu lakini baadaye wakaona kuwa inaongeza uwezekano wa kutokea matezi makubwa ya kensa hiyo. Hivyo wamesisiza kwamba inahitajia muda mrefu ili kujua iwapo dawa hiyo haina madhara kabisa.
Inafaa kujua kuwa ugonjwa wa kensa ya tezi kibofu au prostate cancer huwapata wanaume hasa wanapofikia umri wa miaka 50 na wengine katika miaka ya 70. Nchini Marekani pekee mwaka 2005 inakadiriwa kwamba watu 230,000 walipatwa na ugonjwa huo na kusababisha vifo vya watu 30,000. Wanaume wenye matatizo ya shinikizo la damu wanaelekea kupatwa zaidi na kensa ya prostati.

Dalili za ugonjwa wa kenda ya korodani ni:
Kushindwa kukojoa.
Kuona ugumu wakati wa kukojoa.
Kushindwa kuzuia mkojo hasa usiku.
Mkojo kutoka kwa shinda, kuhisi maumivu wakati wa kukojoa.
Kuona damu imechanganyika na mkono na kuhisi maumivu upande wa chini wa kiuno na upande wa juu wa mapaja.
Lakini dalili zote hizo zinaweza kusababishwa na uvimbe wa tezi kibofu ambao hausababishwi na saratani.
Wanaume walio na dalili hizo wanatajwa kumuona daktari na kupata ushauri zaidi.