Monday, April 5, 2010

Yawezekana kuokoa maisha ya wenye HIV kwa kutumia dawa zisizo ghali

Wachunguzi wa masuala ya tiba wamesema kwamba, bado hakuna jitihada zinazofanywa za kuokoa maisha ya maelfu ya watu wanaoishi na virusi vya HIV kwa kutumia dawa rahisi na zisizo ghali. Wamesisitiza kwamba kuwapa dawa za anti-biotics kama vile co-trimoxazole wale ambao tayari wamegunduliwa kuwa na virusi vya Ukimwi kunaweza kupunguza idadi ya vifo vya wagonjwa hao mwanzoni tu wanapopata ugonjwa huo.

Uchunguzi huo uliochapishwa katika Jarida la Tiba la Lancet umegundua kuwa, kuwapa waathirika wa Ukimwi anti-biotics kunapunguza nusu ya vifo vya wagonjwa hao. Shirika la Afya Duniani WHO) tayari limeamuru kutolewa matibabu hayo lakini wataalamu na madakatari wanasema kuwa watu wengi bado hawapewi dawa hizo. Jitihada nyingi zimekuwa zikifanywa tu kuhakikisha kwamba wale walioathirika na Ukimwi wanapatiwa dawa za kuongeza maisha za antiretroviral ambazo zina athari kubwa katika kuwaongeza maisha. Hata hivyo, wagonjwa wengi wa Ukimwi katika wiki za mwanzo baada ya kugundulika kuwa wana ugonjwa huo, wanakabiliwa na hatari kubwa ya kushambuliwa na magonjwa mbalimbali kutokana na kudhoofu mfumo wao wa kinga wa mwili. Hivyo wataalamu wanasema kwamba, kuongezwa dawa kama vile co-trimoxazole ambazo ni anti-biotic zisizo ghali na ambazo hupatikana kwa urahisi, katika matibabu yao ya muda mrefu kunaweza kuwanusu na kifo.


Takwimu zimeonyesha kuwa, zaidi ya robo ya waathiriwa wa Ukimwi waliopewa dawa za kuongeza maisha za antiretroviral katika nchi za chini ya Jangwa la Sahara walifariki dunia katika mwaka wa kwanza wa matibabu. Lakini uchunguzi uliofanywa na Lancent umeonyesha kwamba, kati ya Waganda 3,179 wenye virusi vya Ukimwi, waliopewa dawa hizo pamoja na kuongezewa anti-biotic katika mpango wao wa matibabu, dawa hizo ziliwapunguzia vifo kwa asilimia 59 katika wiki 12 za kwanza, na kwa asilimia 44 kati ya wiki 12 na 72 za matibabu.
Hata hivyo imeonekana kwamba dawa hizo za anti-biotics hazipatikani katika maeneo mengi ya nchi za Uganda na Zimbabwe ambako kuna wathirika wengi wa Ukimwi.
Pia imeonekana kuwa kutumiwa dwa hizo za nyongeza kuna faida nyingine ya ziada ambayo ni kuepusha maambukizo ya ugonjwa wa Malaria kwa asilimia 15.

No comments: